Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Mapato yatokanayo na Tanzanite yaongezeka baada ya ukuta kujengwa
Mapato ya serikali kutokana na madini ya Tanzanite yameongezeka mara nne zaidi katika kipindi cha miezi mitatu tangu ukuta ulipojengwa kuzunguka migodi, Waziri Mkuu wa Tanzania amewaambia wabunge.
Kassim Majaliwa amesema kati ya mwezi Januari na Machi, Serikali ilipata kiasi cha dola za Marekani zaidi ya 316,000.
Amesema kuwa hiyo ni zaidi ya mara nne ya kiasi ambacho serikali ilikuwa ikipata mwaka jana kutotokana madini
Taarifa hiyo imetolewa siku kadhaa baada ya Rais wa Tanzania, Dokta John Magufuli kuzindua ukuta wa umbali wa Km 24 kuzunguka mgodi unaozalisha Tanzanite mjini Mirerani kaskazini mwa Tanzania
Waziri Majaliwa alisema kabla ya kuwepo ujenzi wa ukuta uliofayika mwezi Novemba mwaka jana, takriban asilimia 40 ya madini ilikuwa ikiibiwa.
Ukuta ulijengwa na jeshi la taifa hilo na kugharimu dola za marekani milioni 3.5 kiasi kilichogharamiwa na serikali.
Hivi karibuni,Tanzania imeweka sheria kali kuhusu uchimbaji na usafirishaji ili kupata mapato zaidi, sera ambayo wachumi wanasema itapunguza kasi ya uwekezaji nchini.
Wakati Tanzania ikijivunia hatua hiyo kuhusu faida ya ukuta huo mpya,wachambuzi wa mambo wanasema ni mapema mno kuainisha faida zake na kuwa hatua nyingi zapaswa kuchukuliwa kuzuia wizi.