Urusi na Ukraine: Fahamu changamoto tano zinazoukabili muungano wa kijeshi wa Nato

Wanajeshi wa Canada

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Wanajeshi wa NATO

Mkutano wa kilele wa Nato wa wiki hii mjini Madrid unakuja wakati muhimu katika historia ya miaka 73 ya muungano huo. Uvamizi wa Russia nchini Ukraine umeelezwa kuwa mshtuko mkubwa zaidi kwa nchi za Magharibi tangu mashambulizi ya 9/11 mwaka 2001. Nato ndio muungano pekee wa kijeshi wenye uwezo wa kuilinda Ulaya dhidi ya uvamizi zaidi wa Urusi, lakini je, ina mkakati?

Chini ya miaka mitatu iliyopita, Rais wa Ufaransa Macron alitangaza Nato kuwa " iliyokufa". Hata hivyo tangu wakati mizinga ya Urusi ilianza kuanguka Ukraine, mwitikio wa nchi za Magharibi umekuwa wa umoja , kasi na nguvu. Imeimarishwa tena kwa madhumuni mapya - kuimarisha mipaka na kusambaza silaha.

Katika mkesha wa mkutano wa kilele mjini Madrid, Katibu Mkuu wa Nato Jens Stoltenberg alitangaza kile alichokiita "mabadiliko katika ulinzi wa muungano", kuimarisha ulinzi kwenye mipaka yake ya mashariki na kuongeza nguvu yake ya dharura na wanajeshi 300,000.

Muungano huo unakabiliwa na changamoto nyingi, kuanzia kuyumbishwa kwa nchi za Balkan hadi mashambulizi ya mtandaoni, ukuaji wa kijeshi angani na nini cha kufanya kuhusu kuongezeka kwa nguvu za kijeshi za China. Kwa mara ya kwanza, mkutano huu wa Nato utashughulikia kile inachokiita "changamoto ambazo Beijing inaleta kwa usalama wetu, masilahi na maadili," Bw Stoltenberg alisema. Haya hapa ni baadhi ya masuala muhimu zaidi ambayo yanaweza kuwa kwenye meza wiki hii.

1. Kuepuka kusambaa kwa vita vya Ukraine

Nato inakabiliwa na kitendo cha kusawazisha. Muungano wa kijeshi wenye nguvu zaidi duniani, unaojumuisha nchi 30 wanachama, tatu kati yao zikiwa na silaha za nyuklia (Marekani, Uingereza na Ufaransa), hautaki kuingia vitani na Urusi. Rais Putin amekumbusha mara kwa mara nchi za Magharibi kwamba ana silaha za nyuklia

Kwa hivyo changamoto kubwa kwa muda wa miezi minne iliyopita, na inayobakia hadi sasa ni jinsi ya kuisaidia Ukraine kujilinda dhidi ya uvamizi huu bila kuingizwa kwenye mapigano yenyewe.

Nato imekuwa ikitumika silaha nyingi za kijeshi Ukrainee

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Nato imekuwa ikitumika silaha nyingi za kijeshi Ukraine

Vizuizi vya mapema vya nchi za Magharibi kuhusu kutoikasirisha Moscow kwa kutuma silaha nzito huko Kyiv vimefutiliwa mbali baada ya habari za kutisha za uhalifu wa kivita wa Urusi na ukatili kuibuka, zikiungwa mkono na data za satelaiti.

Mkutano wa kilele wa Madrid utahitaji kuweka kiwango cha msaada wa kijeshi ambao nchi za Nato zinaweza kutoa na kwa muda gani.

Kwa sasa, Moscow inashinda huko Donbas, eneo kubwa la watu wanaozungumza Kirusi la mashariki mwa Ukraine, ingawa kwa gharama kubwa ya maisha na uharibifu wa mali. Matarajio ni kwamba Urusi itajaribu kushikilia mafanikio haya, labda kuyamega kwa njia sawa na Crimea mnamo 2014.

Kwa kukosekana kwa mkataba wa amani, Nato itakabiliwa na changamoto mpya baadaye. Je, ni kuendelea kuihami Ukraine wakati inajaribu kurejesha ardhi ambayo Moscow sasa inaona kuwa kisheria sehemu ya Shirikisho la Urusi? Kremlin imeashiria silaha za Magharibi zinazogonga ardhi ya Urusi zinavuka mstari mwekundu hivyo hatari za mzozo kulipuka zitaongezeka sana.

2. Kudumisha umoja juu ya Ukraine

Iwapo Urusi ingeshambulia eneo la Donbas bila kuivamia Ukraine nzima kwa pande tatu, basi inawezekana tusingeona umoja huo katika majibu ya nchi za Magharibi. Duru sita za vikwazo vya Umoja wa Ulaya zinaathiri vibaya uchumi wa Urusi na Ujerumani imefuta kwa sasa bomba la mabilioni ya dola la Nord Stream 2 ambalo lingepeleka gesi ya Urusi kaskazini mwa Ujerumani.

Lakini kuna mgawanyiko katika muungano huu wa Magharibi juu ya umbali wa kuadhibu Urusi na ni maumivu gani ambayo uchumi wa Magharibi unaweza kuchukua. Haya yataonekana wazi huko Madrid.

Ujerumani imeshutumiwa kwa kujikokota juu ya kukabidhi silaha ilizoahidi huku Hungary, inayoongozwa na waziri mkuu mwenye uhusiano wa karibu na Rais Putin, ikikataa kuacha kununua mafuta ya Urusi. Pia mataifa ambayo yanahisi kutishiwa zaidi na Moscow, ambayo ni Poland na mataifa ya Baltic, yanasukuma mstari mgumu zaidi na uimarishaji zaidi wa Nato kwenye mipaka yao.

3. Kulinda nchi za Baltiki

 Ujerumani yaongoza katika nato

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Ujerumani ni miongoni mwa mataifa yanayoongoza muungano wa wanajeshi wa NATO
Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Eneo hili lina uwezo wa kuwa kitovu kikubwa kati ya Nato na Urusi. Mwezi huu Urusi ilitishia hatua baada ya Lithuania kuzuia baadhi ya bidhaa zilizowekewa vikwazo na Umoja wa Ulaya zinazosafirishwa katika ardhi lake kuelekea eneo la Urusi la Kaliningrad huko Baltic.

Waziri Mkuu wa Estonia Kaja Kallas ameikashifu Nato kwa kutokuwa tayari kwa uvamizi wa Urusi kuvuka mpaka. Mkakati wa sasa unalenga kujaribu kuchukua tena eneo la Estonia baada tu ya Urusi kuwa tayari kuvamia. "Wanaweza kutufuta kwenye ramani," anasema.

Estonia, Latvia na Lithuania zote zilikuwa sehemu ya Umoja wa Kisovyeti. Leo, ni mataifa huru na yote katika Nato.

Kuna vikundi vinne vya vita vya kimataifa vilivyowekwa katika nchi hizi tatu, pamoja na Poland, kama sehemu ya kile kinachoitwa usalama mapema. Uingereza inaongoza kile kilicho Estonia, Marekani inaongoza nchini Poland, Ujerumani katika Lithuania na Canada kile cha Latvia.

Viongozi wa Baltic sasa wanataka angalau mgawanyiko wa vikosi vya Nato vilivyowekwa katika kila nchi kama kizuizi kikubwa. Huenda hii ikawa mada yenye mjadala mzito mjini Madrid.

4. Kuruhusu Finland na Sweden kujiunga

Finland na Sweden, zote zikiwa zimechanganyikiwa vikali na uvamizi wa Urusi kwa taifa huru, zimeamua kuwa wanataka kuacha msimamo wao wa kutoegemea upande wowote na kujiunga na Nato. Muungano unawakaribisha kwa mikono miwili, lakini si rahisi hivyo. Uturuki, ambayo ni mwanachama tangu 1952, imekuwa ikizuia kuongezwa kwao kwa misingi kwamba nchi hizi mbili zinawahifadhi Wakurdi wanaotaka kujitenga ambao Uturuki inawaona kama magaidi.

Lakini kwa sababu Finland ni Sweden ni muhimu sana kwa Nato, kila juhudi itafanywa kutafuta njia ya kuzunguka pingamizi la Uturuki. Mara tu watakapojiunga, Bahari ya Baltic itakuwa "ziwa la Nato," linalopakana na nchi nane wanachama, na ulinzi wa anga uliounganishwa na mfumo wa makombora.

Ikiangalia mbali zaidi, Nato itahitaji kuamua kama itawahi kunuia kupokea wanachama wapya kama vile Georgia na Moldova, pamoja na hatari zote zinazohusiana na kuchochea Kremlin ambayo tayari ina mkanganyiko.

Ramani inayoonesha Urusi ikilinyakuwa eneo la Crimea
Maelezo ya picha, Ramani inayoonesha Urusi ikilinyakuwa eneo la Crimea

5. Kupanda kwa haraka kwa matumizi ya ulinzi

Hivi sasa, wanachama wa Nato wanalazimika kutumia asilimia 2 ya Pato lao la kila mwaka katika ulinzi, lakini sio wote wanafanya hivyo. Takwimu za hivi karibuni za zinaonyesha wakati Marekani ilitumia asilimia 3.5 katika ulinzi na Uingereza ilitumia asilimia 2.2, Ujerumani ilitumia asilimia 1.3 pekee huku Italia, Kanada, Hispania na Uholanzi zote zikiwa zimepungukiwa na asilimia 2 ya malengo yao. Urusi ilitumia asilimia 4.1 ya Pato la Taifa katika ulinzi.

Wakati Donald Trump alipokuwa Rais wa Marekani, alitishia kuiondoa nchiyake kutoka kwa muungano ikiwa nchi zingine wanachama hazingechangia zaidi. Hii ilikuwa na athari fulani, lakini uvamizi wa Ukraine umekuwa na athari zaidi. Siku tatu tu baada ya kuanza, Ujerumani ilitangaza kuwa itatenga Euro bilioni 100 ya ziada kwa ulinzi na hatimaye kuongeza kiwango chake cha juu zaidi ya asilimia . Wiki hii, mkuu wa Nato alitangaza kuwa nchi tisa kati ya 30 wanachama zimefikia au kuvuka lengo la asilimia 2, wakati 19 zina mipango ya kufikia mwaka 2024.

Wakuu wa kijeshi wa nchi za Magharibi na wachambuzi wamekubaliana kwa kauli moja kutaka kuongezwa kwa haraka kwa matumizi ya ulinzi ikiwa Urusi itazuiwa kutokana na uchokozi zaidi. Lakini kupunguzwa kwa ulinzi mfululizo katika miongo ya hivi karibuni kumesababisha maswali juu ya ikiwa Nato bado ina wingi wa kutosha kuzuia uvamizi wa Urusi wa siku zijazo.

wa najeshi wa NATO

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Wanajeshi wa Uingereza wakishiriki katika mazoezi ya kijeshi

Ingawa matumizi ya ulinzi wa Uingereza yaliongezwa hivi majuzi, pia kumekuwa na upotevu mkubwa katika ununuzi. Nguvu ya sasa ya Jeshi la Uingereza ni askari 82,000 ikiwa ni pamoja na wale walio katika mafunzo, lakini baada ya kupunguzwa idadi hii huenda ikashuka hadi 72,500. Cha kusikitisha zaidi, Urusi na Uchina ziko mbele ya Magharibi katika kutengeneza makombora ya hypersonic ambayo yanaweza kusafiri kuelekea shabaha yao kwa zaidi ya mara tano ya kasi ya sauti na kwa njia isiyotabirika ya ndege.

Haya yote yanakuja wakati bei ya chakula na mafuta ikipanda kwa kasi duniani kote, kwa hivyo bajeti tayari ni ngumu. Kutenga pesa zaidi kwa ajili ya ulinzi kunaweza kukosa uungwaji mkono ndani ya nchi wakati kuna mahitaji mengine mengi ya juu ya matumizi ya serikali.

Lakini wakuu wa kijeshi wanaonya kwamba ikiwa Nato haitaimarisha usalama wake sasa, basi gharama ya uvamizi zaidi wa Urusi katika siku zijazo itakuwa kubwa zaidi.