Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Jinsi nchi za Afrika zilivyogawanyika kuhusu mzozo wa Israel na Palestina
Viongozi wa Mataifa ya Africa wametoa wito kwa pande kinzani katika mzozo wa Israel ana Palestina kuzitisha makabiliano makali yaliozuka tarehe 7 mwezi Oktoba , wakati wapinganaji wa Palestina Hamas walipoanzisha mashambulkizi ya kushtukiza dhidi ya Israel
Mwitikio huo haujafanana kabisa huku Zambia, Kenya na Ghana zikilaani kwa uwazi zaidi Hamas na kuiunga mkono Israel, na Sudan, Djibouti na Afrika Kusini zikiwa wazi kuhusu uungaji mkono wao kwa Wapalestina.
Licha ya Israel kuongeza uwepo wake wa kidiplomasia barani humo katika muongo mmoja uliopita na mipango ya nchi kadhaa za Afrika kuhamisha balozi zao kutoka Tel Aviv hadi Jerusalem, Israel haijaimarisha kikamilifu uungaji mkono wake barani Afrika katika mzozo huu wa hivi punde.
Umoja wa Afrika ulisisitiza katika taarifa kwa lugha ya Kifaransa na Kiingereza kwamba makabiliano hayo yalichangiwa na "kunyimwa haki za kimsingi za watu wa Palestina, hasa ile ya taifa huru".
"Mwenyekiti anaziomba kwa dharura pande zote mbili kukomesha uhasama wa kijeshi na kurejea, bila masharti, kwenye meza ya mazungumzo ili kutekeleza kanuni ya nchi mbili kuishi bega kwa bega, ili kulinda maslahi ya watu wa Palestina na watu wa Israel. ," Mwenyekiti wa Tume ya AU Moussa Faki aliongeza.
Israel hapo awali ilitaka kushiriki katika mikutano ya AU kama mwangalizi, na hivyo kuzua taharuki.
Rais wa Uganda Yoweri Museveni pia alitoa wito kwa pande zinazozozana kurejea kwenye "suluhu ya mataifa mawili" katika taarifa yake ya tarehe 7 Oktoba, ambapo alisema anajutia ghasia hizo.
Bw Museveni alimkaribisha Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu mnamo 2016 na 2020 katika juhudi za kuboresha uhusiano kati ya nchi hizo mbili.
Kiongozi huyo wa Uganda pia alisimamia kuhalalisha uhusiano kati ya Israel na Sudan mwaka 2020.
Hata hivyo, wizara ya mambo ya nje ya Sudan iliunga mkono Wapalestina kufuatia makabiliano mapya.
"Sudan inafuatilia kwa wasiwasi matukio hatari yanayoendelea hivi sasa katika Palestina inayokaliwa kwa mabavu. Sudan inaunga mkono upya haki halali ya watu wa Palestina kuwa na taifa lao huru. Inataka kuzingatiwa kwa maazimio ya kimataifa na ulinzi wa raia wasio na hatia," taarifa iliyochapishwa kwenye ukurasa wa Facebook wa shirika la habari la serikali Suna ilisema.
Afrika Kusini yatoa wito wa "kusitishwa kwa mapigano mara moja"
"Kanda hiyo inahitaji sana mchakato wa amani unaoaminika ambao unatoa wito wa wingi wa maazimio ya awali ya Umoja wa Mataifa ya suluhisho la serikali mbili na amani ya haki na ya kina kati ya Israel na Palestina," Idara ya Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano ( Dirco) ilisema kwenye ukurasa wake rasmi wa Facebook tarehe 7 Oktoba.
Wakati huo huo, Nigeria ilionya kwamba "mzunguko wa ghasia na kulipiza kisasi umechukuliwa kusaidia tu kuendeleza mzunguko usioisha wa maumivu na mateso kwa raia, ambao wanabeba mzigo mkubwa wa kila vita".
Rais wa Kenya William Ruto alizitaka pande zinazozozana kupunguza kasi huku "maafa yakiendelea kuongezeka".
"Kenya inashikilia kwa dhati kwamba hakuna uhalali wowote wa ugaidi, ambao ni tishio kubwa kwa amani na usalama wa kimataifa. Vitendo vyote vya kigaidi na misimamo mikali ni ya kuchukiza, ya jinai na haikubaliki, bila kujali mhusika au nia zao," alisema.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Zambia Stanley Kakubo aliunga mkono Israel katika taarifa yake kulaani mashambulizi ya Hamas.
"Tunalaani vikali mashambulizi ya hivi majuzi dhidi ya Israel, ambayo kwa masikitiko makubwa yamesababisha watu kupoteza maisha. Tunalaani bila shaka vitendo vyote vya uchokozi na ghasia, na tunaendelea kusisitiza ulazima wa kutafuta njia za kidiplomasia kutatua migogoro ya kimataifa," alisema.