Wajue nyota 11 wa soka wasio na mikataba ambao bado wako sokoni

Chanzo cha picha, Getty Images
- Author, Neil Johnston
- Nafasi, BBC
- Muda wa kusoma: Dakika 5
Dirisha la usajili la majira ya kiangazi limefungwa na vilabu vya Ligi Kuu England vimetumia mamilioni ya pauni kuimarisha vikosi vyao.
Lakini timu ambazo zilikosa kutimiza malengo yao, bado zina nafasi ya kuwaleta wachezaji huru, wachezaji ambao hawana mkataba na wanaweza kusaini klabu yoyote.
BBC inakutajia baadhi ya wachezaji ambao bado wako sokoni.
Kipa - Keylor Navas

Chanzo cha picha, Getty Images
Keylor Navas, 37, alitangaza kuondoka Paris St-Germain mwezi Mei na aliripotiwa kujiunga na Monza ya Italia kwa uhamisho wa bure wakati mkataba ulipoisha.
Kipa huyo wa zamani wa Costa Rica alitumia miaka mitano Real Madrid na mingine mitano PSG. Pia alicheza mechi 17 za Ligi Kuu England wakati wa mkopo huko Nottingham Forest msimu wa 2022-23.
Beki wa kulia - Serge Aurier

Chanzo cha picha, Getty Images
Beki wa zamani wa Tottenham na Nottingham Forest Serge Aurier, 31, alicheza pamoja na nyota wa zamani wa Crystal Palace, Wilfried Zaha huko Galatasaray mwishoni mwa msimu uliopita kabla ya kuondoka msimu wa joto.
Beki huyo wa Ivory Coast mwenye uzoefu mkubwa ni mshindi mara mbili wa Ligue 1 akiwa na Paris St-Germain.
Beki wa kati - Joel Matip

Chanzo cha picha, Getty Images
Joel Matip, 33, aliiaga Liverpool msimu wa joto baada ya misimu minane.
Aliisaidia klabu hiyo kushinda Ligi Kuu England na Ligi ya Mabingwa Ulaya chini ya Jurgen Klopp baada ya kujiunga na Liver akitokea Schalke kwa uhamisho wa bure.
Matip tangu wakati huo amekuwa akihusishwa na vilabu kadhaa ikiwemo West Ham.
Beki wa kati - Mats Hummels

Chanzo cha picha, Getty Images
Mshindi wa Kombe la Dunia la 2014 nchini Ujerumani, Mats Hummels aliichezea Borussia Dortmund fainali ya Ligi ya Mabingwa mwezi Juni waliposhindwa na Real Madrid kwenye Uwanja wa Wembley.
Ilikuwa ni mechi ya mwisho ya mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 35 katika klabu hiyo. Hummels, ambaye ameicheza pia Bayern Munich, amekuwa akihusishwa kuhamia Roma.
Beki wa kushoto - Brandon Williams

Chanzo cha picha, Getty Images
Brandon Williams, 24, alikuwa na umri wa miaka 19 alipoifungia Manchester United katika sare ya 3-3 katika Ligi Kuu England dhidi ya Sheffield United mwaka 2019.
Williams, alikuwa na United tangu akiwa umri wa miaka tisa, aliachiliwa msimu wa joto baada ya mechi 51 za kikosi cha kwanza.
Kwa sasa yupo huru na hana klabu mpya.
Winga - Victor Moses

Chanzo cha picha, Getty Images
Victor Moses, 33, anatafuta klabu mpya baada ya kuondoka Spartak Moscow.
Moses alicheza mechi 220 za Ligi Kuu England kwa vilabu vitano, vikiwemo Chelsea na Liverpool.
Alikaa Chelsea kwa miaka tisa kati ya 2012 na 2021 baada ya kujiunga kutoka Wigan kwa pauni milioni 9.
Kiungo wa kati - Adrien Rabiot

Chanzo cha picha, Getty Images
Adrien Rabiot, 29, aliondoka Juventus mwishoni mwa kandarasi yake akiwa amecheza mechi 212 na timu hiyo ya Serie A baada ya kusajiliwa kutoka Paris St-Germain mwaka 2019.
Mchezaji huyo wa zamani wa chuo cha michezo cha Manchester City, amekuwa akihusishwa na Manchester United. Rabiot aliichezea Ufaransa katika fainali ya Kombe la Dunia 2022 walipopoteza kwa mikwaju ya penalti dhidi ya Argentina.
Kiungo wa kati - Andre Gomes

Chanzo cha picha, Getty Images
Andre Gomes, 31, aliondoka Everton, ambayo ilimnunua kwa pauni milioni 22 mwaka 2019, na mkataba wake umeisha baada ya msimu wa 2023-24.
Wasifu wa mchezaji huyo wa kimataifa wa Ureno unajumuisha kuichezea Barcelona, Valencia na Lille.
Ripoti zinasema Gomes huenda akahamia Marekani kucheza MLS lakini bado hana klabu.
Mshambuliaji - Robert Skov

Chanzo cha picha, Getty Images
Robert Skov, 28, aliwahi kuelezwa kuwa ni mbadala wa Gareth Bale kwa Denmark. Mshambuliaji huyo anahusishwa na Tottenham. Alicheza Kombe la Dunia 2022 lakini anabaki bila klabu baada ya miaka mitano nchini Ujerumani akiwa na Hoffenheim.
Skov alicheza zaidi ya mechi 100 za Bundesliga, akifunga mara 11.
Mshambuliaji - Anthony Martial

Chanzo cha picha, Getty Images
Manchester United ilitangaza mwezi Mei, kuwa Anthony Martial ataondoka klabuni hapo baada ya kufunga mabao 90 katika mechi 317 alizocheza.
Mshambulizi huyo wa Ufaransa ana umri wa miaka 28 na bado hana klabu.
Ripoti nchini Ufaransa, zinasema Lille, ambayo itamenyana na Liverpool katika Ligi ya Mabingwa msimu huu, inavutiwa na Martial na wanashughulikia dili la kuinasa saini yake.
Mshambuliaji - Memphis Depay

Chanzo cha picha, Getty Images
Memphis Depay, 30, aliisaidia Uholanzi kufika nusu fainali ya Euro 2024.
Anawindwa na klabu mpya baada ya kukosa nafasi msimu 2023/24 akiwa na Atletico Madrid, kwa sababu ya jeraha.
Mchezaji huyo wa zamani wa Manchester United alikaa kwa miezi 18 Barcelona na pia amewahi kucheza Ufaransa katika klabu ya Lyon.
Imetafsiriwa na Rashid Abdallah na kuhaririwa na Seif Abdalla












