'Waarabu na Waislamu wote wako wapi? Mumewaacha watu wa Palestina wateseke'

A woman in the cooking gas queue in Deir al-Balah who raged at being abandoned
Maelezo ya picha, Mwanamke huyu anayepanga foleni kuchukua gesi ya kupikia katikati mwa Gaza anashutumu ulimwengu kwa kuwatelekeza Wapalestina.
    • Author, Adnan El-Bursh
    • Nafasi, BBC Arabic
    • Akiripoti kutoka, Deir al-Balah, Gaza

"Waarabu na Waislamu wote wako wapi? Wako wapi watetezi wote wa haki za binadamu? Mumewaacha watu wa Palestina wakiteseka, wakilala njaa na kuangamizwa."

Mwanamke mwenye umri wa makamo aishambulia dunia katika foleni ya gesi ya kupikia huko Gaza.

Anapiga kelele kwa hasira hewani, kukata tamaa na kuchanganyikiwa yakidhirika katika uso wake.

"Tumekuwa tukingoja kwenye foleni ili kujaza mtungi mmoja wa gesi tangu asubuhi na mapema. Nilifanya sala yangu ya asubuhi nikiwa nimesimama."

Hundreds queue for cooking gas in the central Gazan city of Deir al-Balah on Tuesday, 28 November

Chanzo cha picha, Hani Kali/BBC

Maelezo ya picha, Mamia wakiwa kwenye foleni ya kutafuta gesi ya kupikia katikati mwa mji wa Gazan wa Deir al-Balah

Ananiambia amehamishwa kutoka Beit Hanoun kaskazini, kilomita 2 tu kutoka mpaka na Israeli.

"Siwezi kuelezea uharibifu. Familia nzima imefutwa kutoka kwa kumbukumbu za raia. Waliuawa chini ya nyumba zao.

"Gaza imeharibiwa kabisa. Utuhurumie."

Sasa anaishi na familia yake katika shule ya Umoja wa Mataifa katika mji wa Deir al-Balah katikati mwa Gaza.

A young man sitting on a cooking gas cylinder in Deir al-Balah

Chanzo cha picha, Hani Kali/BBC

Maelezo ya picha, Watu wanahangaika kutafuta njia ya kujikimu
Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Baada ya Hamas kushambulia Israel tarehe 7 Oktoba, na kuua watu 1,200 na kuchukua mateka zaidi ya 200, Israel ilianza mashambulizi ya anga na kisha kufanya uvamizi wa ardhini.

Takriban Wapalestina 14,800 wameuawa kufikia sasa, kulingana na wizara ya afya inayosimamiwa na Hamas.

Ukanda wa Gaza ni makazi ya watu 2.4m na Umoja wa Mataifa unasema 1.8m wamekimbia makazi yao baada ya Israeli kuwaamuru kuhamia kusini.

Kuna mamia kwenye foleni ya gesi ya kupikia. Vijana wameketi kwenye mitungi ya gesi huku wakisubiri. Hali ni ya wasiwasi. Watu wamechoka.

Tangu kusitishwa kwa mapigano tarehe 24 Novemba, hadi malori 200 ya misaada yamekuwa yakiingia Ukanda wa Gaza kwa siku, karibu nusu ya yale yaliyoingia kabla ya vita.

Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanasema kuwa yameweza kupeleka baadhi ya misaada kaskazini ambapo jeshi la Israel lipo, lakini kuna uhaba mkubwa kila mahali.

Mwanaume mwingine kwenye foleni anakubali kuzungumza nami.

“Huwezi kukuta kikombe cha chai wala pakiti moja ya biskuti, juzi watu walikuwa wakigawana mkate wakiwa wamelala barabarani.

"Mvua tuliyoshuhudia jana na baridi tuliyopitia. Watu walilala hapa. Mungu atusaidie."

The queue for cooking gas in Deir al-Balah in central Gaza

Chanzo cha picha, Hani Kali/BBC

Maelezo ya picha, Watu wana hasira na woga kwani wanalazimika kupanga foleni hadi siku tatu kutafuta mafuta ya kupikia

Israel ilisitisha uwasilishaji wote wa mafuta mwanzoni mwa mzozo na kisha kuruhusu kwa kiasi kidogo, kwa sasa jumla ya lita 140,000 kila siku mbili, kulingana na afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani.

Serikali ya Israel inasema mafuta ya ziada yanaweza kutumiwa na Hamas, shirika la kigaidi lililopigwa marufuku katika Umoja wa Ulaya, Uingereza na Marekani.

Mohammed al-Qidrah anasubiri kwa utulivu kwenye foleni ya gesi ya kupikia.

"Tumekuwa hapa kwa siku tatu. Tulikuja hapa siku mbili zilizopita na kutoka 03:00 hadi sasa, hatujaweza kujaza mtungi wetu.

"Hatuwezi kupata mafuta, unga au kitu chochote. Unahitaji kusimama katika mstari kwa kila kitu na unahangaika kuipata."

Marekani inatuma ndege tatu za misaada nchini Misri zikiwa zimebeba vifaa vya matibabu, chakula cha msaada na bidhaa za majira ya baridi, ambazo zitasambazwa na Umoja wa Mataifa huko Gaza.

A Palestinian man and his children sort freshly picked olives on a farm during a ceasefire in Khan Younis in the southern Gaza Strip on 28 November 2023

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Wapalestina wanajaribu kuokoa mabaki ya mavuno yao ya mizeituni wakati wa muda wa kusitishwa mapigano kusini mwa Gaza.

Shirika la Afya Ulimwenguni linaonya kuwa watu wengi zaidi watakufa kutokana na magonjwa kuliko watakavyouawa katika shambulio la bomu ikiwa miundombinu ya afya haitarejeshwa.

Wakati huo huo, muungano wa misaada unaoongozwa na Umoja wa Mataifa unasema asilimia 60 ya majengo ya Gaza yameharibiwa .

Wakati muda wa usitishaji vita ukiendelea, kuna dalili kwamba maisha yanarejea Gaza ambako mabaki ya zao la mzeituni mwaka huu yanavunwa.

"Tunapaswa kutumia fursa hii, hakuna muda," mkulima wa Kipalestina Fathy Abu Salah ameliambia shirika la habari la Reuters. Anaishi Khan Younis kusini.

"Vita hivi vilituangamiza, hakuna uzalishaji wowote. Mavuno mengi yaliharibika," anaongeza.

Palestinians wait to get their olives pressed at an oil mill during a ceasefire in Khan Younis in the southern Gaza Strip on 28 November 2023

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Mafuta yana haba sana lakini Wapalestina wanajizatiti kusindika baadhi ya zao la mzeituni

Ukosefu wa umeme umesababisha kutegemewa kwa mafuta kuendesha mitambo kwenye mashine ya mizeituni.

"Kutafuta mafuta ni shida ambayo kila mtu anakabiliwa nayo," anasema mkulima wa mizeituni na mfanyakazi wa vyombo vya habari Mohamed Wafy.

"Mara tu tulipopata mafuta, tuliweza kufungua mashine ya mizeituni, hata kama inafanya kazi kwa kiwango cha chini kabisa," anasema.

Imetafsiriwa na Yusuf Jumah