Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Vikosi vya Urusi vinashambulia eneo lote la mapambano mashariki mwa Ukraine

Vikosi vya Moscow vinashambulia kwa mabomu maeneo ya Ukraine baada ya kufanya mashambulizi mapya katika eneo la Donbas mashariki mwa nchi hiyo.

Moja kwa moja

  1. Watakao tuma 'picha za ngono za wanafunzi' kukabiliwa na kifungo cha miaka 14 Nigeria

    Raia wa Nigeria wameonywa kuwa kutumiana picha za ngono za watoto ni kosa litakalosababisha kifungo cha miaka 14 jela, hii inakujabaada ya video inayodaiwa kuwahusisha watoto wa shule kusambaa nchini humo.

    Wanafunzi kutoka shule za kifahari za Chrisland walikuwa katika safari ya kwenda Dubai mwezi uliopita wakati tukio hilo linalodaiwa kurekodiwa kutokea.

    Mama wa mtoto wa miaka 10 aliyerekodiwa katika video hiyo anasema binti yake alilazimishwa kushiriki.

    Serikali katika jimbo la Lagos imeamuru kufungwa kwa shule hiyo ili "kesi inayodaiwa kuwa ya unyanyasaji wa kingono" iweze kuchunguzwa.

    Katika video iliyotumwa kwenye mitandao ya kijamii, mama huyo anadai binti yake alileweshwa na wanafunzi wa kiume na kushutumu mamlaka za shule kwa kuficha tukio hilo.

    Shule za Chrisland, ambazo zinaendesha shule binafsi kadhaa za msingi na sekondari katika jiji la Lagos, zimekanusha kufanya makosa yoyote, zikisema inatekeleza jukumu lake la kutunza kwa uzito na itatoa ushirikiano kwa uchunguzi wowote.

    Kwa mujibu wa shule hiyo, watoto walikuwa wakicheza mchezo wa "Ukweli au kuthubutu" (Truth or Dare) uliohusisha wanafunzi watano kati ya 76 waliohudhuria Michezo ya Shule ya Kimataifa kati ya Machi 8 na 14.

    Ilisema iliwajulisha wazazi wao juu ya "utovu huo wa nidhamu" na wanafunzi hao wamepewa karipio kwa mujibu wa kanuni za shule.

    Lakini mama wa mtoto huyo mwenye umri wa miaka 10 anasema hakuambiwa uzito wa kile kilichotokea mwanzoni, lakini aligundua baadaye wakati mzazi mwingine alipomtahadharisha kuhusu kanda hiyo ya video, ambayo tangu wakati huo imekuwa ikisambazwa sana kwenye mitandao ya kijamii.

    Alipomhoji binti yake, aligundua kuwa binti yake alikuwa ameambiwa asizungumze kuhusu kilichotokea.

    Kwa mujibu wa mama yake mtoto wake sasa amesimamishwa shule.

  2. Waethiopia wakusanyika katika ubalozi wa Urusi kujiandikisha kwa vita

    Makumi ya vijana wa Ethiopia wanaendelea kukusanyika katika ubalozi wa Urusi mji mkuu Addis Ababa, Jumanne kufuatia uvumi wa kuajiriwa kwa wanajeshi kupigana nchini Ukraine.

    Lakini msemaji wa ubalozi huo, Maria Chernukhina, alisema hakuna uajiri unaofanywa nchini Ethiopia.

    Alisema watu hao walikuwa wanaonyesha mshikamano na Urusi.

    "Tuna wageni wengi katika ubalozi huu wanaokuja kuunga mkono Urusi," aliambia BBC.

    "Baadhi yao wanatuambia wako tayari kusaidia kwa njia yoyote wanayoweza. Lakini sisi sio wakala wa kuajiri," Bi Chernukhina aliongeza.

    Baathi ya vijana hao wa Ethiopia katika ubalozi huo walionekana wakiwa na hati zao za kibinafsi.

    Kijana aliyekuwa akisubiri mlangoni aliambia BBC kwamba anatafuta mshahara mzuri kama mwanajeshi au kuajiriwa katika kazi nyingine yoyote inayopatikana.Pia napenda Urusi," alisema.

    Wengine walisema wamesikia fununu za mishahara mikubwa nchini Urusi.

    Ethiopia ilikuwa miongoni mwa nchi zilizokosa kikao cha Umoja wa Mataifa cha kupigia kura azimio kuhusu uvamizi wa Urusi nchini Ukraine.

    Unaweza pia kusoma

    • YA MSINGI:Mzozo wa Ukraine: Kwanini Urusi inaivamia Ukraine na Putin anataka nini?
    • UFAFANUZI:Mzozo wa Ukraine: Swift ni nini na kwa nini kuipiga marufuku Urusi ni muhimu sana?
    • UCHAMBUZI:Mzozo wa Ukraine: Putin humsikiliza nani?
    • KWENYE RAMANI:Uvamizi wa Ukraine: Shambulio la Urusi kwenye ramani
    • ZELENSKY:Volodymyr Zelensky: Mfahamu rais wa Ukraine aliyeacha umaarufu wake wa TV na kuingia kwenye siasa
    • PUTIN:Vladimir Putin: Rais wa Urusi aliyeagiza shambulio Ukraine
    • SILAHA:Mzozo wa Ukraine:Makombora ya stinger na silaha nyingine kali zinazotumiwa Ukraine
  3. Walimu wa Kenya wataka adhabu ya viboko kurejeshwa shuleni

    Walimu wa Kenya wanasema adhabu ya viboko inapaswa kurudishwa madarasani ili kukabiliana na utovu wa nidhamu wa wanafunzi.

    Kenya iliharamisha adhabu ya viboko shuleni mwaka wa 2001. Sheria ya Watoto inalinda watoto dhidi ya aina zote za unyanyasaji.

    Lakini walimu wakuu wa shule za upili wanasema marufuku hiyo inadhoofisha mamlaka yao shuleni.

    "Sera ya usimamizi wa nidhamu ni kazi ngumu na [inafanya] kuwa vigumu kwa shule yoyote au bodi ya usimamizi kuchukua hatua zozote za kinidhamu," alisema Kahi Indimuli, mkuu wa chama cha walimu wakuu.

    Waalimu wakuu wanakutana wiki hii katika kongamano la kila mwaka na watajadili kuongezeka kwa machafuko shuleni.

    Shule kadhaa za sekondari za serikali ziliteketezwa mwishoni mwa mwaka jana, huku matukio mengi yakilaumiwa kwa wanafunzi.

    Mnamo Februari, Waziri wa Elimu George Magoha alionya walimu dhidi ya kuwachapa viboko wanafunzi shuleni, lakini hapo awali alidokeza mabadiliko ya sera ya kukabiliana na ongezeko la visa vya utovu wa nidhamu shuleni.

  4. Habari za hivi punde, Tunahitaji silaha zaidi - Mbunge wa Ukraine asema

    Oleksiy Goncharenko, mbunge wa Ukraine, ameomba silaha zaidi kutoka mataifa ya Magharibi:

    "Ikilinganishwa na [jeshi] la Afghanistan, ambalo lilipokea $80bn (£61.5bn) ya vifaa, ikiwemo silaha na risasi, msaada wa mwisho wa Marekani ulikuwa $800m.

    "Ulimwengu unapaswa kutambua kwamba tunapigana na Urusi, jeshi kubwa zaidi katika bara la Ulaya, na nchi yenye bajeti ya silaha mara nyingi zaidi ya Ukraine, hivyo tunahitaji silaha zaidi."

  5. 'Niliendesha gari kwa mara ya kwanza baada ya miaka 15'-Rais Samia

    Rais Samia Suluhu Hassan amezindua filamu yake mpya ya Royal Tour mjini New York katika ukumbi wa Guggenheim Museum, siku ya Jumatatu, April 18.

    Rais Samia amesema haikuwa kazi rahisi kwake kuifanya filamu hiyo wakati amezungukwa na walinzi wengi ambao walikuwa wakimwambia usifanye hiki na hiki.

    Ingawa lilikuwa jambo gumu kwake kulifanya ila angependa kurudia tena na tena kwa ajili ya taifa lake.

    Aidha rais alibainisha kuwa filamu hiyo ilimfanya aendeshe gari kwa mara ya kwanza baada ya miaka 15.

    Huku kwa upande wa wageni, wengi walikuwa na shauku ya kujua ni muda gani sahihi wa kutembelea Tanzania.

    Na sifa nyingi zilimuendea Rais kwa uthubutu wake wa kuigiza filamu.

    Hata hivyo muongozaji filamu hiyo alikiri ugumu wa kufanya kazi na rais na anashukuru kuwa alikuwa anamsikiliza.

  6. Mali yapokea vifaa zaidi vya kijeshi kutoka Urusi

    Mali imepokea shehena nyingine ya vifaa vya kijeshi kutoka Urusi baada ya Umoja wa Ulaya kusitisha mpango wake wa mafunzo ya kijeshi na taifa hilo la Sahel.

    Mkuu wa majeshi ya Mali, Meja Jenerali Oumar Diarra, alipokea helikopta mbili za kivita na rada za uchunguzi, ofisi ya rais wa Mali ilisema katika taarifa.

    Ofisi ya rais ilisambaza video inayoonyesha vifaa hivyo vikitolewa na ndege ya mizigo ya Urusi katika uwanja wa ndege wa mji mkuu Bamako.

    Bw Diarra alitaja uungaji mkono wa Urusi kwa Mali kama "dhihirisho la ushirikiano wenye manufaa makubwa".

    Mwezi uliopita, Mali ilipokea helikopta mbili za kivita na rada zilizotengenezwa na Urusi muda mfupi baada ya ripoti kuibuka kwamba waziri wake wa ulinzi na mkuu wa jeshi la anga walizuru Moscow ''kisiri''.

    Vyombo vya habari vya serikali vilitangaza sana mapokezi hayo na kupongeza uungaji mkono wa Urusi unaokua kwa Mali katika operesheni za kukabiliana na waasi.

    Mali imetetea uhusiano wake na Urusi baada ya mizozo ya kimataifa kuhusu uamuzi wa kupeleka mamluki kutoka kampuni ya kijeshi yenye utata ya Wagner mwezi Disemba.

    Hii ilisababisha kuondolewa kwa vikosi vya Ufaransa vya Oparesheni Barkhane na wanajeshi wa Ulaya chini ya Kikosi Kazi cha Takuba.

    Wapiganaji wa Wagner na jeshi la Mali wamehusishwa na madai ya ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu katika oparesheni za pamoja za kukabiliana na waasi katika miezi ya hivi karibuni, ripoti yaambayo Mali inakanusha.

  7. Ndege ya Urusi yazunguka 15,000km kuchukua wanadiplomasia waliofurushwa

    Ndege iliyotumwa kutoka Moscow kuwachukua wanadiplomasia wa Urusi waliofukuzwa Ugiriki na Uhispania imelazimika kubadili mkondo kwa kilomita 15,000 kutokana na marufuku ya ndege ya Umoja wa Ulaya, tovuti ya kufuatilia safari za ndege ya FlightRadar24 reports inaripoti.

    "Wakati Uhispania na Ugiriki zililitoa nafasi mara moja kwa ndege kuingia kwenye anga yao, ndege zilizunguka nchi zingine ambazo zinadumisha marufuku ya safari za ndege za Urusi," tovuti hiyo ilisema.

    Iliongeza kuwa umbali wa safari hiyo ulikuwa kilomita 15,163, "hii inakaribia na safari ndefu zaidi duniani kati ya Singapore na New York".

  8. Urusi inajaribu kuchukua udhibiti kamili wa mashariki - Jeshi la Ukraine

    Jeshi la Ukraine limesema kuwa vikosi vya Urusi vinafanya "vitendo vya uchokozi" ili kuchukua udhibiti kamili wa maeneo ya mashariki ya Donetsk na Luhansk, katika taarifa yake ya siku ya 55 ya vita.

    • Vikosi vya Urusi vinaendelea na harakati za silaha na vifaa vya kijeshi kwenda Ukraine kutoka mikoa ya kati na mashariki mwa Urusi.
    • Wanajeshi wa Urusi wanaendelea kuuzuia kwa kiasi mji wa Kharkiv kaskazini mashariki mwa Ukraine.
    • Lengo kuu la jeshi la Urusi ni kuvunja ulinzi wa jeshi la Ukraine katika eneo la Luhansk na Donetsk, na pia kuweka udhibiti kamili juu ya mji wa bandari wa kusini wa Mariupol.
    • Urusi inaendelea kutumia ardhi ya Belarus kufanya mashambulizi ya anga na kufanya uchunguzi wa anga nchini Ukraine.
    • Kikosi cha 810 cha Wanamaji wa Bahari Nyeusi kilipoteza wanajeshi 158, na wengine takriban 500 walijeruhiwa, na watu 70 hawajulikani waliko.
    • Wanajeshi wa Ukraine wameharibu vifaru 10, vitengo 18 vya silaha na vitengo nane vya vifaa vya magari katika saa 24 zilizopita.
    • Jeshi la anga la Ukraine lililenga shabaha saba - ndege moja, UAV nne na makombora mawili ya mbawa siku ya Jumatatu.
    • BBC haijaweza kuthibitisha madai haya kikamilifu.
  9. Wanajeshi walevi waua 15 mashariki mwa DR Congo

    Wanajeshi wawili wamewaua kwa kuwapiga risasi watu 15 katika mashambulio tofauti mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Wahasiriwa wote walikuwa raia.

    Haya yanajiri baada ya watu sita kujeruhiwa wakati wanajeshi waliporusha guruneti kwenye umati wa watu walipokuwa wakijaribu kuwakamata.

    Afisa mmoja katika jimbo la Kivu Kusini alisema mwanajeshi aliyekuwa mlevi kwenye boti la Ziwa Tanganyika aliwaua abiria wanane wakiwemo watoto kabla ya kukamatwa.

    Siku ya Jumapili mwanajeshi mwingine alimpiga risasi kanali mmoja, mlinzi wake na raia watano katika jimbo la Ituri.

    Muuaji huyo ambaye pia inasemekana alikuwa mlevi, alipigwa risasi na mwenzake alipokuwa akikimbia.

    Kwa zaidi ya miongo miwili watu kote mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wamevumilia mashambulizi ya mara kwa mara na makumi ya makundi yenye silaha.

    Rais Félix Tshisekedi amesema kukomesha ghasia hizo ni kipaumbele cha kwanza kwa serikali yake.

    Majimbo mawili yalizingirwa kwa karibu mwaka mmoja uliopita.

    Lakini ilikuwa na athari ndogo kwani waasi na wakati mwingine wanajeshi wa Congo wasio na nidhamu wanaendelea kusababisha uharibifu.

  10. Waingereza waliokamatwa na Urusi wakipigana Ukraine waomba msaada wa Uingereza

    Wanaume wawili wa Uingereza walioripotiwa kukamatwa na jeshi la Urusi wakati wakipigana nchini Ukraine wameonekana kwenye Televisheni ya serikali ya Urusi wakimuomba msaada Waziri Mkuu Boris Johnson.

    Shaun Pinner, 48, na Aiden Aslin, 28, walionyeshwa kwenye video mbili tofauti siku ya Jumatatu, wakiomba kubadilishana na mwanasiasa anayeiunga mkono Urusi iliyofanyika nchini Ukraine.

    Haijabainika iwapo maombi yao kwa waziri mkuu, yaliyoonyeshwa kwenye kituo cha Rossiya 24, yalifanywa kwa kulazimishwa.

    Ofisi ya Mambo ya Nje iliitaka Kremlin kuwatendea wafungwa utu. Chanzo kutoka idara hiyo kimelaani "unyonyaji wa wafungwa wa vita kwa madhumuni ya kisiasa".

    Katika sehemu hizo mbili, Bw Aslin na Pinner wanazungumza na waziri mkuu, wakiomba kubadilishana na mwanasiasa anayeunga mkono Kremlin Viktor Medvedchuk.

    Katika video yake, Bw Aslin anazungumza huku mtu asiyejulikana akiwa amesimama juu yake.

    Bw Medvedchuk pia ameonekana kwenye video, iliyotolewa na idara ya ujasusi ya Ukraine.

  11. Kampuni yalipa fidia kwa kumfanyia sherehe mfanyakazi wake

    Mwanaume mmoja wa Kentucky ametunukiwa dola 450,000 baada ya kampuni yake kumfanyia karamu ya kushtukiza ya siku ya kuzaliwa licha ya onyo alilolitoa kuwa ingeweza kumsababishia msongo wa mawazo na hofu.

    Mlalamikaji, Kevin Berling, anadai kuwa karamu ile ambayo hakuitaka ya siku ya kuzaliwa ya mwaka 2019 ilimsababishia matukio kadhaa ya kuwa na hofu.

    Madai ya kesi ya Bw Berling ilidai kuwa kampuni hiyo ilimbagua kwa sababu ya ulemavu wake. Kampuni hiyo imekanusha kufanya jambo lolote baya.

    Kwa mujibu wa kesi iliyowasilishwa katika Kaunti ya Kenton, Kentucky, Bw Berling - ambaye ana matatizo ya kuwa na wasiwasi - alimwomba meneja wake asisherehekee siku yake ya kuzaliwa kazini kama ilivyo kawaida kwa wafanyakazi wengine kwa sababu inaweza kumsababishia mashambulizi ya hofu na kurejesha kumbukumbu zisizofurahi za utotoni.

    Licha ya ombi la Bw Berling, kampuni hiyo, ambayo hufanya vipimo vya Covid-19, ilimfanyia karamu ya kushtukiza mnamo Agosti 2019, na kusababisha shambulio la hofu. Haraka alitoka kwenye sherehe na kumalizia chakula chake cha mchana kwenye gari lake.

    Kesi hiyo inabainisha kuwa Bw Berling "alishutumiwa na kukosolewa" katika mkutano siku iliyofuata, ambapo alishutumiwa "kwa kutowafurahisha wafanyakazi wenzake" na "kuwa binti mdogo".

    Mkutano huo wa mvutano ulisababisha shambulio la pili la hofu, baada ya hapo kampuni ikamrudisha nyumbani kwa muda uliosalia wa Agosti 8 na 9 Agosti.

  12. Mauaji na uharibifu nchini Ukraine katika picha

    Rais wa Ukraine Zelensky amesema kuwa Urusi imeanzisha mashambulizi ya kuliteka eneo la mashariki la Donbas.

    Siku ya Jumatatu, Urusi ilifyatua msururu wa roketi na mizinga katika maeneo kadhaa ya mashariki, huku raia wanane wakiuawa katika mji wa Kreminna huko Luhansk na katika eneo la Donetsk.

    Watu saba waliuawa na wengine 11 kujeruhiwa katika mashambulizi manne ya Urusi magharibi mwa Lviv, jiji ambalo liliepushwa kwa kiasi kikubwa na mashambulizi yaliyoonekana kwingineko nchini Ukraine.

    Picha zote ni kuanzia tarehe 18 Aprili.

  13. Vita vya Ukraine: Matukio ya hivi punde

    Ikiwa ndio mwanzo unajiunga nasi, hizi ndizo taarifa zinazojiri nchini Ukraine kwa muhtasari.

    • Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema "vita vya Donbas" vimeanza, baada ya Urusi kuanzisha mashambulizi yake katika eneo la mashariki.
    • Shambulio hilo la bomu limeiacha miji ya zamani ya watalii mashariki ikijiandaa kwa mashambulizi ya kijeshi.
    • Msemaji wa Pentagon John Kirby alisema Urusi imeanza "kujipanga" mashariki mwa Ukraine - kuweka mazingira ya mashambulizi makubwa.
    • Wakati huo huo, maafisa katika mji wa Lviv walisema Jumatatu kwamba shambulio la asubuhi liliua takriban raia saba na kujeruhi wengine 11.
    • Umoja wa Mataifa umeripoti kuwa zaidi ya raia milioni 4.9 wa Ukraine wameikimbia nchi hiyo tangu Urusi ilipovamia. Kwa mujibu wa doria ya mpaka wa Marekani, maelfu ya watu wamefika kwenye mpaka wa Marekani na Mexico.
    • Raia wengine 3,724 wa Ukraine walifika kwenye mpaka wa kusini mwezi Machi - kuruka mara kumi na mbili zaidi ya mwezi mmoja kabla.

    Unaweza pia kusoma

    • YA MSINGI:Mzozo wa Ukraine: Kwanini Urusi inaivamia Ukraine na Putin anataka nini?
    • UFAFANUZI:Mzozo wa Ukraine: Swift ni nini na kwa nini kuipiga marufuku Urusi ni muhimu sana?
    • UCHAMBUZI:Mzozo wa Ukraine: Putin humsikiliza nani?
    • KWENYE RAMANI:Uvamizi wa Ukraine: Shambulio la Urusi kwenye ramani
    • ZELENSKY:Volodymyr Zelensky: Mfahamu rais wa Ukraine aliyeacha umaarufu wake wa TV na kuingia kwenye siasa
    • PUTIN:Vladimir Putin: Rais wa Urusi aliyeagiza shambulio Ukraine
    • SILAHA:Mzozo wa Ukraine:Makombora ya stinger na silaha nyingine kali zinazotumiwa Ukraine
  14. Karibu kwa matangazo ya moja kwa moja leo Jumanne 19.04.2022.