Moja kwa moja, Israel yaanzisha mashambulizi mapya dhidi ya Iran na Lebanon

Wakati huo huo, UAE inasema mifumo yake ya ulinzi wa anga inajibu "tishio la kombora".

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Madereva wa malori wauawa na wanajihadi Mali

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Shirikisho la Kimataifa la Wafanyakazi wa Uchukuzi (ITF) limeitaka serikali ya Mali kuchukua hatua baada ya wimbi la mashambulizi mabaya ya msafara kuwalenga madereva wa malori ya usafirishaji mafuta.

    'Wafanyikazi wa usafiri ni muhimu ili jamii zihudumiwe - haistahili waachwe bila ulinzi', ITF ilisema katika taarifa kwa vyombo vya habari.

    Nchini Mali, kikundi chenye silaha chenye uhusiano na Al Qaeda kimewaua madereva kadhaa wa malori ya usafiri wa masafa marefu na vijana wawili waliokuwa wanafunzwa kazi ya udereva kusini magharibi mwa nchi hiyo, kulingana na ripoti iliyochapishwa Jumatatu Machi 9 na shirika la Human Rights Watch.

    Kwa mujibu wa HRW, mauaji hayo yalifanyika Januari 29, wakati wapiganaji kutoka Jama'at Nusrat al-Islam wa al-Muslimeen (JNIM) waliposhambulia msafara wa takriban malori 40 ya mafuta yaliyosindikizwa na jeshi kuelekea mji wa Kayes.

    Kuchapishwa kwa ripoti hii kuliibua hisia nyingi mtandaoni kwani inaonyesha jinsi hali imekuwa hatari kwa madereva wa malori.

    Miili ya waathiriwa iligunduliwa wiki mbili baadaye, huku wakiwa wamezibwa macho, mikono ikiwa imefungwa migongoni mwao na kukatwa koo, katika kile ambacho Human Rights Watch ilikielezea kuwa uhalifu wa kivita wa wazi.

    Mamlaka ya Mali bado haijatoa maoni yoyote kuhusu madai mahsusi katika ripoti ya Human Rights Watch. Serikali pia mara kwa mara inashutumu mashirika yasiyo ya kiserikali kwa upendeleo au kutegemea taarifa ambazo hazijathibitishwa.

    Na hivi majuzi zaidi, wanajeshi wa Mali na mamluki wa jeshi la Urusi barani Afrika waliripotiwa kuwaua raia saba karibu na mpaka wa Mauritania kwa madai ya kuwa na uhusiano na vikundi vya kijihadi.

    Waathiriwa hao waliripotiwa kusafiri kutoka Fassala kusini-mashariki mwa Mauritania kuelekea soko la kila wiki karibu na Tenenkou katika eneo la Mopti nchini Mali walipozuiwa na doria ya jeshi la Mali na wapiganaji wa Urusi.

    Abiria walijaribu kukimbia na sita "walipigwa risasi papo hapo, na wa saba akakatwa koo", ripoti hiyo ilisema.

    Wanajeshi wa Mali na mamluki wa Urusi mara nyingi wamekuwa wakishutumiwa kufanya ukatili dhidi ya raia, madai ambayo yamekanushwa mara kwa mara na utawala wa kijeshi, ikisisitiza kuwa operesheni zao zinalenga makundi ya kijihadi pekee.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Gharama ya vita vya Iran itakuwa mzigo kwa watumiaji, mkurugenzi wa kampuni ya usafirishaji aambia BBC

    .

    Ongezeko la gharama za usafirishaji zinazosababishwa na mzozo nchini Iran zitaishia kwa watumiaji, mkurugenzi wa kampuni ya pili kwa ukubwa duniani ya usafirishaji amesema.

    "Tuna mifumo ya kawaida ya ukandarasi inayoathirika na mabadiliko haya ya mafuta, iwe yanapanda au yanashuka, kwa wateja," Vincent Clerc, mkuu wa kampuni kubwa ya usafirishaji ya Denmark Maersk aliambia BBC katika mahojiano.

    "Kwa hivyo inamaanisha kwamba hatimaye, katika hali hii, ongezeko hili itakuwa gharama kwa wateja wetu na watumiaji."

    Kampuni hiyo ya Denmark inaongozwa ya usafirishaji wa makontena, ambalo lina jukumu muhimu katika kusafirisha bidhaa za watumiaji kama vile vinyago, nguo na vifaa vya elektroniki kote ulimwenguni.

    Soma zaidi:

  3. Polisi Canada wachunguza shambulizi dhidi ya ubalozi wa Marekani

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Washukiwa wasiojulikana wameshambulia ubalozi wa Marekani huko Toronto kwa risasikatika kile ambacho maafisa wamekielezea kama "tukio la usalama wa taifa", huku polisi wakijitahidi kubaini chanzo cha shambulio hilo.

    Mamlaka ilisema shambulizi hilo lilitokea mapema Jumanne asubuhi yapata saa 04:30 kwa saa za huko (08:30 GMT). Maafisa walipata maganda ya risasi kwenye eneo la tukio na jengo lilikuwa limeshambuliwa, alisema Frank Barredo, naibu mkuu wa Polisi wa Toronto.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilisema inafahamu kuhusu tukio hilo na inafuatilia kwa karibu hali hiyo kwa kushirikiana na vyombo vya sheria vya eneo hilo.

    Shambulizi hili linatokea huku polisi wa Norway wakichunguza mlipuko uliotokea nje ya ubalozi wa Marekani huko Oslo siku ya Jumapili.

    Pia unaweza kusoma:

  4. UN inasema kuwachukua kwa lazima watoto wa Ukraine hadi Urusi ni uhalifu dhidi ya binadamu

    .

    Chanzo cha picha, AP

    Umoja wa Mataifa umesema kufukuzwa na kuhamishwa kwa lazima kwa watoto wa Ukraine hadi nchini Urusi ni uhalifu dhidi ya binadamu na uhalifu wa kivita.

    Ripoti mpya ya Tume Huru ya Uchunguzi ya Kimataifa kuhusu Ukraine inasema mamlaka ya Urusi "katika ngazi ya juu zaidi" imewafukuza "maelfu" ya watoto kutoka maeneo iliyokalia ya Ukraine.

    "Ushiriki wa moja kwa moja" wa Vladimir Putin umekuwa "ukionekana tangu mwanzo," inaongeza.

    Ukraine inasema karibu watoto 20,000 wamepelekwa kinyume cha sheria nchini Urusi na Belarusi.

    Tume ya Umoja wa Mataifa hadi sasa imebaini visa 1,205 vya watoto waliochukuliwa kutoka maeneo ya Ukraine na Urusi mnamo mwaka 2022.

    Asilimia themanini ya watoto hawa bado hawajarudishwa, ripoti inasema, na wazazi na walezi wengi hadi leo hawajui mahali walipo watoto hao.

    Hii ni sawa na kutoweka kwa lazima na kucheleweshwa kurejeshwa nyumbani bila sababu, ambayo ni uhalifu dhidi ya binadamu na uhalifu wa kivita mtawalia, kulingana na Umoja wa Mataifa.

    Idadi kubwa ya watoto waliotajwa katika ripoti ya Umoja wa Mataifa waliishi katika kile kinachoitwa Jamhuri za Watu wa Donetsk na Luhansk - maeneo ya Ukraine ambayo Moscow inadai kuyadhibiti kinyume cha sheria.

    Soma zaidi:

  5. Israel yaanzisha mashambulizi mapya dhidi ya Iran na Lebanon

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Jeshi la Israeli limetoa taarifa mpya, likisema limeanzisha wimbi jipya la mashambulizi huko Beirut nchini Lebanon.

    Inasema inalenga miundombinu ambayo ni ya Hezbollah inayoungwa mkono na Iran kusini mwa mji mkuu wa Lebanon.

    Jeshi Kuu la Marekani lasema meli 16 za Iran zilizokuwa zikipeleka mabomu chini ya bahari zimeharibiwa

    Wakati huo huo, Kamandi Kuu ya Marekani (Centcom) inasema vikosi vya Marekani "vimeharibu" meli 16 za Iran zilizokuwa zikipeleka mabomu chini ya bahari leo ​​karibu na Mlango-Bahari wa Hormuz.

    Centcom pia ilishirikisha video inayoonekana kuonyesha meli hizo zikishambuliwa.

    Hii inafuatia maoni ya awali ya Rais wa Marekani Donald Trump, ambapo alisema jeshi lilishambulia meli 10 za Iran ambazo hazikuwa zikifanya kazi katika Mlango Bahari, baada ya kuahidi kukabiliana na meli hizo "haraka na na nguvu kubwa".

    Kupita kwa meli kupitia mlango bahari - mfereji wenye shughuli nyingi zaidi duniani wa usafirishaji wa mafuta - kumevurugwa vibaya wakati wa vita vya Marekani na Israeli dhidi ya Iran. Ujasusi wa Marekani waliamini kuwa Iran ilikuwa ikijiandaa kupeleka mabomu ya majini katika Mlango Bahari wa Hormuz, mshirika wa BBC wa Marekani CBS News iliripoti mapema leo.

    Soma zaidi:

  6. Hujambo. Karibu katika matangazo yetu mubashara ya tarehe 11/03/2026.