Wavamia hosteli na kuua 11 kwa risasi Afrika Kusini

Washambuliaji wakiwa na bunduki waliingia na kuanza kuwashambulia watu waliokuwa wakinywa pombe. Mtoto wa miaka 12 ni miongoni mwa waliouawa na ambaye hawakuwa miongoni mwa waliokuwa wanakunywa. Jumla ya watu 25 walishambuliwa.

Moja kwa moja

Na Yusuph Mazimu

  1. Mazungumzo ya amani yakiendelea, Urusi yaishambulia Ukraine kwa makombora

    a

    Urusi imefanya mashambulizi makubwa ya anga dhidi ya miundombinu ya Ukraine wakati mazungumzo kati ya Marekani na Ukraine yakiingia siku ya tatu huko Florida.

    Usiku wa kuamkia Jumamosi, Ukraine ilisema Urusi ilirusha ndege zisizo na rubani 653 na makombora 51, ambapo mengi yalidunguliwa, huku shambulio moja likilenga kituo cha reli cha Fastiv na kuharibu jengo kuu la stesheni.

    Rais Volodymyr Zelensky alisema mashambulizi hayo hayakuwa na maana kijeshi, huku Urusi ikidai inalenga viwanda vinavyohusiana na jeshi pamoja na miundombinu ya nishati na bandari. Wizara ya nishati ya Ukraine ilisema mashambulizi mapya yameathiri mikoa minane na kusababisha kukatika kwa umeme.

    Wakati huohuo, shirika la nyuklia la Umoja wa Mataifa lilisema kuwa Kiwanda cha Nyuklia cha Zaporizhzhia kilichodhibitiwa na Urusi kilipoteza nguvu za umeme za nje kwa muda, jambo ambalo limekuwa likijirudia tangu uvamizi wa Urusi kuanza.

    Huko Florida, mjumbe maalum wa Marekani Steve Witkoff na Rustem Umerov wa Ukraine walisema mazungumzo yao yamekuwa “ya kujenga” na wamekubaliana juu ya mfumo wa mipango ya kiusalama ambayo inaweza kuandamana na makubaliano ya amani. Walisema kumaliza vita kunategemea utayari wa Urusi kuchukua hatua za kupunguza mvutano na kusitisha mauaji.

    Mazungumzo hayo yameingia siku ya tatu, na timu ya Ukraine ikipokea taarifa kuhusu mkutano wa hivi karibuni kati ya Witkoff na Rais Vladimir Putin mjini Moscow.

  2. Wavamia hosteli na kuua 11 kwa risasi Afrika Kusini

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Watu 11 wameuawa kwenye shambulio la risasi katika hosteli moja nchini Afrika Kusini. Wengine 14 walijeruhiwa baada ya watu wenye silaha kuvamia eneo hilo lililoko katika mtaa wa Saulsville, magharibi mwa Pretoria, mapema Jumamosi. Mtoto wa miaka mitatu ni miongoni mwa waliouawa.

    Msemaji wa polisi, Brigedia Athlenda Mathe, alisema: “Watu wasiopungua watatu waliovalia kama wageni waliingia katika hosteli hii ambako kundi la watu lilikuwa likinywa pombe, na wakaanza kufyatua risasi hovyo.”

    Chanzo cha shambulio hicho bado hakijulikani na hakuna mtu yeyote aliyekamatwa mpaka sasa. Tukio hili linaongeza idadi ya mashambulio ya risasi yaliyotikisa taifa hilo lenye viwango vya juu vya uhalifu katika miaka ya karibuni.

    Inaripotiwa kuwa watu hao wenye bunduki waliingia majira ya saa 10:30 alfajiri kwa saa za Afrika Kusini na kuanza kuwashambulia watu waliokuwa wakinywa pombe. Mtoto wa miaka 12 na msichana wa miaka 16 ni miongoni mwa waliouawa.

    Mathe alisema, “Nathibitisha kwamba jumla ya watu 25 walipigwa risasi.”

    “Watu wasio na hatia pia wanajikuta wakipata madhara,” aliambia shirika la utangazaji la SABC.

    Afrika Kusini ni miongoni mwa mataifa yenye viwango vya juu zaidi vya mauaji dunian, vifo 45 kwa kila watu 100,000, kwa mujibu wa takwimu za 2023-2024 za Umoja wa Mataifa. Kulingana na takwimu za polisi, watu 63 waliuawa kila siku kati ya Aprili na Septemba.

  3. Marekani yasema mazungumzo mapya na Ukraine yamepiga hatua

    S

    Chanzo cha picha, EPA

    Marekani na Ukraine zimeitaka Urusi kuonyesha “nia ya dhati ya amani ya kudumu” baada ya mazungumzo ya wiki hii huko Moscow kushindwa kuleta mafanikio. Mjumbe wa Marekani Steve Witkoff na waziri wa usalama wa Ukraine Rustem Umerov wanaendelea na mazungumzo yakiingia siku ya tatu leo huko Florida, ambayo yalielezwa kuwa “ya kujenga”.

    Pande hizo zilikubaliana muundo wa mpango wa usalama utakaosimamia makubaliano ya amani na kujadili hatua za kuzuia uvamizi wa baadaye, huku mazungumzo yakitarajiwa kuendelea leo. Wakati wa mkutano huo, timu ya Ukraine iliarifiwa kuhusu mazungumzo ya Witkoff na Rais Vladimir Putin, ambayo Kremlin ilisema hayakutoa "makubaliano yoyote".

    Rais Volodymyr Zelensky amesema anataka taarifa kamili kuhusu kilichojadiliwa Moscow, ikizingatiwa kuwa mpango wa awali wa amani wa Marekani ulionekana kuipendelea Urusi kabla ya kufanyiwa marekebisho. Bado kuna masuala makubwa yanayozozaniwa, kama dhamana za usalama wa Ukraine baada ya vita na suala la mipaka.

    Urusi kwa sasa inadhibiti karibu robo ya eneo la Ukraine, hasa maeneo ya Donetsk na Luhansk. Putin ameonya wanajeshi wa Ukraine kujiondoa Donbas au sivyo Urusi “itayakomboa kwa nguvu”, madai ambayo Kyiv imekanusha, ikisema bado inadhibiti miji muhimu.

    Ukraine na washirika wake wa Ulaya wanaamini njia bora ya kuizuia Urusi baadaye ni kwa Ukraine kupewa uanachama wa NATO au dhamana imara za usalama. Hata hivyo, Urusi inapinga vikali na Trump naye ameonyesha mara kadhaa kutounga mkono Ukraine kujiunga na NATO, suala ambalo lilijadiliwa pia Moscow.

  4. Mapigano mapya yazuka kati ya Pakistan na Afghanistan

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mapigano mapya yaliyosabisha vifo yameripotiwa mpakani karibu na mji wa Spin Boldak, huku Pakistan na Taliban kila upande ukilaumu mwingine kuvunja makubaliano ya usitishaji mapigano.

    Wakazi wa Spin Boldak walikimbia usiku kucha. Taarifa zinasema Hospitali ya Kandahar imepokea miili ya watu wanne, huku Pakistan ikiripoti majeruhi watatu. Hali ya mvutano imekuwa ikijirudia kwa miezi kadhaa.

    Taliban imewahi kuihusisha Pakistan na mashambulizi ya anga ndani ya Afghanistan, madai ambayo Pakistan imekuwa ikikanusha. Kila upande umethibitisha kushambuliana kwa risasi katika mapigano ya karibu saa nne.

    Msemaji wa Waziri Mkuu wa Pakistan alisema Taliban ilianza mashambulizi “bila sababu”, na kwamba jeshi la nchi hiyo lilijibu mapigo “vikali”. Taliban nayo ilidai Pakistan “imeanzisha mashambulizi tena”, hivyo wakaamua kujitetea.

    Video zinaonyesha raia wengi wakikimbia kwa miguu na kwa magari kutokana na hofu ya mapigano kuongezeka. Mapigano haya yametokea chini ya miezi miwili tangu Qatar na Uturuki kusaidia kufikia usitishaji mapigano uliomaliza vita vikali zaidi kati ya pande hizo tangu 2021.

    Hata hivyo, uhasama bado uko juu. Pakistan imekuwa ikiituhumu Taliban kuwahifadhi wapiganaji wanaoishambulia, madai ambayo Taliban inakanusha na kusema Pakistan inalaumu watu wengine kwa “kushindwa kwake katika eneo la usalama”.

    Wiki iliyopita, duru ya nne ya mazungumzo ilifanyika Saudi Arabia, lakini hakuna makubaliano mapya yaliyofikiwa. Hata hivyo, vyanzo vinaeleza kuwa pande zote mbili zilikubaliana kuendelea kuheshimu usitishaji mapigano.

  5. Kenya na Marekani zasaini makubaliano ya afya licha ya hofu kuhusu usalama wa taarifa

    a

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kenya imesaini makubaliano ya kihistoria ya miaka mitano na Marekani kuhusu afya, ikiwa ya kwanza kufanyika tangu serikali ya Donald Trump kubadili mfumo wa misaada ya kigeni.

    Mkataba huo wa thamani ya $2.5bn unalenga kukabiliana na magonjwa ya kuambukiza nchini Kenya, huku makubaliano kama hayo yakitarajiwa pia kwa mataifa mengine ya Afrika yanayoendana na sera mpya za Marekani.

    Hata hivyo, mpango huo umeibua hofu kwamba Marekani inaweza kupata taarifa nyeti za kiafya za Wakenya, lakini Waziri wa Afya Aden Duale amesema kuwa taarifa itakayotolewa itakuwa ya jumla tu bila taarifa za mtu mmoja mmoja.

    Tangu kuingia madarakani, Trump alivunja USAID na kusitisha misaada mingi, hatua iliyoathiri upatikanaji wa dawa katika nchi zinazoendelea. Sasa, chini ya “America First Global Health Strategy,” misaada imekuwa ikitolewa kupitia makubaliano ya moja kwa moja baina ya serikali.

    Kupitia makubaliano haya, Marekani itachangia $1.7bn huku Kenya ikitoa $850m, ikilenga HIV/Aids, malaria, kifua kikuu, huduma ya uzazi, polio na maandalizi dhidi ya milipuko ya magonjwa. Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio alisifu makubaliano haya na kuitaja Kenya kama mshirika wa muda mrefu, akitoa pongezi kwa uongozi wake katika jukumu la kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini Haiti.

    Rais William Ruto amesema fedha hizo zitatumika kuboresha vifaa vya hospitali na kuongeza watumishi katika sekta ya afya, akiahidi uwazi na uwajibikaji.

  6. Kombe la Dunia 2026: Droo yazipanga makundi magumu timu za Afrika

    a

    Chanzo cha picha, Feargal

    Droo ya Kombe la Dunia 2026 imepangwa rasmi, na mataifa ya Afrika sasa yanajipanga kwa michuano mikubwa zaidi duniani itakayofanyika Marekani, Canada na Mexico, Julai 2026.

    Afrika itawakilishwa na timu kadhaa zenye historia na ubora, ambazo zote zimepangwa kwenye makundi yanayohitaji umakini na maandalizi makubwa. Mpaka sasa timu 9 za Afrika zimefuzu, DRC inasubiri mchuzo wa mwezi Machi, 2026 kuona kama na yeye itapata nafasi.

    Kundi A: Afrika Kusini imeangukia kundi moja na wenyeji Mexico, Korea Kusini pamoja na mshindi wa mchujo wa UEFA D. Ingawa kundi ni gumu, Bafana Bafana wameonyesha maendeleo makubwa miaka ya karibuni.

    Kundi C: Morocco, ambao waliandika historia Qatar 2022 kwa kufika nusu fainali, wako pamoja na Brazil, Haiti na Scotland. Wawakilishi wa Afrika Kaskazini wanaingia kama moja ya timu zinazopewa nafasi nzuri kutokana na kiwango chao cha juu.

    Kundi E: Ivory Coast watavaana na Ujerumani, Curacao na Ecuador. Baada ya ubora waliouonyesha Afcon, Tembo wana nafasi ya kuonyesha makucha dhidi ya timu kubwa.

    Kundi G: Misri watapambana na Ubelgiji, Iran na New Zealand. Pharaohs wakiendelea kujengwa upya, kundi hili linahitaji nidhamu na uimara mkubwa ili kutinga hatua ya mtoano.

    Kundi I: Senegal, mabingwa wa Afrika 2022, wamewekwa na Ufaransa, Norway na mshindi wa Fifa play-off 2. Hili ni kundi lenye nguvu, lakini Senegal imekuwa ikifanya vizuri kimataifa na ina wachezaji wanaocheza ligi kubwa duniani.

    Kundi L: Ghana wapo na England, Croatia na Panama. Black Stars watakutana na vigogo wawili wa Ulaya lakini mara nyingi wamekuwa timu ya kusababisha maajabu kwenye Kombe la Dunia.

  7. Trump asifu makubaliano ya amani ya kihistoria kati ya DR Congo na Rwanda

    s

    Chanzo cha picha, Screengrab

    Rais wa Marekani Donald Trump amepongeza makubaliano ya amani kati ya DR Congo na Rwanda kama “ya kihistoria”, wakati viongozi wa mataifa hayo mawili wakisaini mkataba wa kumaliza mzozo wa muda mrefu katika hafla iliyoandaliwa Washington. Hata hivyo, wachambuzi wanasema hii ni kuidhinisha tu makubaliano ya Juni ambayo hayajafaulu kusitisha mapigano.

    Hafla hiyo ilifanyika wakati mapigano mapya yakiripotiwa mashariki mwa DR Congo, ambapo jeshi la serikali lilishutumiana na waasi wa M23 wanaodaiwa kuungwa mkono na Rwanda, kila upande ukimtuhumu mwenzake kuvuruga mchakato wa amani.

    Katika sherehe ya kusaini, Rais Félix Tshisekedi na Paul Kagame hawakupeana mikono na walionekana kukwepana, lakini hilo halikumzuia Trump kusisitiza kwamba makubaliano hayo ni “muhimu kwa Afrika na dunia”.. Alisema ana imani viongozi hao wataheshimu mkataba na kuleta mustakabali mpya kwa watu wao.

    Viongozi kutoka Kenya, Angola, Burundi, Togo, pamoja na makamu wa rais wa Uganda, walihudhuria tukio hilo. Kagame alimpongeza Trump kama kiongozi “mwenye usawa” na mwenye mtazamo wa kiutendaji, akisema njia ya mbele haijawahi kuwa wazi kiasi hicho. Tshisekedi naye alitoa “shukrani za dhati” huku akisisitiza umuhimu wa Rwanda kuheshimu makubaliano hayo.

    Wakati huo huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda Olivier Nduhungirehe alisema hakuna sehemu ya makubaliano inayolazimisha Rwanda kuondoa wanajeshi nchini DR Congo kwa kuwa “hakuna wanajeshi wa Rwanda” waliopo humo. Hata hivyo, wataalamu wa Umoja wa Mataifa wanasema jeshi la Rwanda linadhibiti kwa kiasi kikubwa oparesheni za M23.

    Waziri huyo pia alitilia shaka dhamira ya serikali ya DR Congo, akidai Kinshasa imeendelea kufanya mashambulizi ya angani licha ya mkataba wa Juni. DR Congo nayo imekuwa ikiishutumu Rwanda kwa ukiukaji kama huo, huku ripoti za UN zikionyesha vikosi vya Rwanda na M23 vikiendelea kuwepo katika ardhi ya DRC.