Idadi ya waliofariki Kenya kwa mafuruko yafikia 28 huku tahadhari ya hatari za kiafya ikitolewa

Chanzo cha picha, EPA
Idadi ya waliofariki dunia imeonezeka hadi 28 kutokana na mvua kubwa inayoendelea kunyesha kote nchini huku wizara ya afya Kenya ikitoa tahadhari kuhusu hatari zinazoweza kutokea kiafya.
Timu za uokozi bado zinatafuta manusura, polisi imesema.
Mkuu wa polisi wa Nairobi George Seda alisema miili mitano zaidi ilipatikana Jumamosi jioni huku kukiwa na hofu kwamba idadi ya vifo inaweza kuongezeka wakati shughuli za utafutaji zikiendelea.
"Timu ziko huko tena kuendelea kutafuta manusura wanaoweza kupatikana lakini tunatarajia kupata miili zaidi," alisema.
Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Afya nchini Kenya Mary Muthoni amesema kwamba mvua kubwa na mafuriko vinaweza kusababisha uchafuzi wa vyanzo vya maji, kuongezeka kwa uzalishaji wa vijidudu vya magonjwa kama vile mbu na kuvuruga mifumo ya usafi.
Hali hizi, aliongeza, zinaweza kuchangia milipuko ya magonjwa ya kuambukiza na mengineo kama kipindupindu, homa ya matumbo, na kuhara ambayo yanaweza kutokea kutokana na unywaji wa maji au chakula kilichochafuliwa.
Maafisa wa afya walitahadharisha zaidi kwamba hali ya hewa ya baridi na unyevunyevu inaweza kusababisha kuongezeka kwa maambukizi ya njia ya upumuaji, hasa miongoni mwa makundi yaliyo hatarini kama vile watoto, wazee na wenye kinga dhaifu.
Majeraha yanayohusiana na mafuriko pia yaliorodheshwa miongoni mwa hatari zinazowezekana wakati wa msimu wa mvua.
Wizara pia imetaka raia kuwa na tahadhari juu ya kuzama maji pamoja na kuumwa na nyoka kipindi hiki cha mafuriko.
Soma zaidi:



