Mahakama
nchini Nigeria imemhukumu aliyekuwa Waziri wa Nishati, Saleh Mamman,
kifungo cha miaka 75 jela baada ya kupatikana na hatia ya kutakatisha fedha
kiasi cha naira bilioni 33.8 sawa na dola milioni 24.7 za Marekani.
Uamuzi huo
ulitolewa Jumatano katika mji mkuu wa Abuja baada ya mahakama kumtia
hatiani mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 68 bila yeye kuwepo mahakamani.
Mapema mwezi
huu, Saleh Mamman alipatikana na hatia kwa makosa 12 yanayohusiana na
udanganyifu na utakatishaji fedha katika kesi iliyowasilishwa na shirika la
kupambana na ufisadi nchini Nigeria, la Economic and Financial Crimes
Commission (EFCC).
Mahakama
iliamuru vifungo hivyo vya gerezani kutumikia kwa mfululizo. Pia ilimtaka
Mamman kurejesha naira bilioni 22 zinazohusishwa na miradi ya umeme ya Mambilla
na Zungeru, ambayo alikuwa akiisimamia alipokuwa madarakani.
Wiki chache
kabla ya hukumu hiyo kutolewa, Mamman alikuwa amechukua fomu za kuwania uteuzi
wa uchaguzi wa ugavana katika jimbo la Taraba kupitia chama tawala cha All
Progressives Congress kabla ya uchaguzi wa mwaka 2027.
Hajulikani alipo
kwa sasa na hajatoa tamko lolote hadharani kuhusu hukumu hiyo.
Mamman
aliwahi kuhudumu kama Waziri wa Nishati chini ya rais wa zamani wa Nigeria,
Muhammadu Buhari, ambaye serikali yake iliingia madarakani kwa ahadi ya
kupambana na ufisadi.
Hukumu hiyo
imewashangaza Raia wengi wa Nigeria, kwani kutiwa hatiani kwa maafisa wakuu wa
serikali kwa makosa ya ufisadi bado ni jambo lisilo la kawaida nchini humo.
Kesi hiyo ni
sehemu ya kampeni pana ya EFCC dhidi ya maafisa wa zamani wa serikali
wanaotuhumiwa kwa ufisadi.
Uchunguzi
mwingine mkubwa umehusisha aliyekuwa Waziri wa Sheria, Abubakar Malami, pamoja
na aliyekuwa Waziri wa Masuala ya Kibinadamu, Sadiya Umar Farouq, ambaye hivi
karibuni alitangazwa kusakwa na shirika hilo.
Hukumu hiyo
pia imefufua hasira za wananchi kuhusu mgogoro wa muda mrefu wa umeme nchini
Nigeria — hasa ikizingatiwa kuwa Mamman aliwahi kuahidi kuwa wizara yake
ingeboresha usambazaji wa umeme kwa wananchi.
Licha ya
kuwa mmoja ya wazalishaji wakubwa wa nishati barani Afrika, Nigeria bado
inakabiliwa na uhaba mkubwa wa umeme, huku kukatika kwa umeme mara kwa mara
kukiathiri biashara kote nchini.
Familia
nyingi pamoja na kampuni hutegemea jenereta zinazotumia mafuta ili kupata
umeme, huku kupanda kwa bei ya mafuta kukiwaacha mamilioni ya watu wakihangaika
kumudu gharama za vyanzo mbadala vya nishati.