Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Seoul yataka wanajeshi wa Korea Kaskazini waondoke Urusi mara moja

Korea Kusini imemwita balozi wa Urusi, ikitaka "kuondoka mara moja" kwa wanajeshi wa Korea Kaskazini ambayo inasema wanapewa mafunzo ya kupigana nchini Ukraine.

Muhtasari

  • Mpango wa kumaliza mzozo 'mara moja, kwa wote' unajadiliwa - mjumbe wa Marekani
  • Mashambulizi ya Israel: Tunachokijua kufikia sasa
  • Kenya yathibitisha kuwa raia wanne wa Uturuki walirejeshwa nyumbani
  • Hamas inakusudia kuweka utambulisho wa kiongozi wake mpya kuwa siri
  • Mjumbe wa Marekani Mashariki ya Kati awasili Beirut kwa mazungumzo ya kusitisha mapigano
  • Seoul yataka wanajeshi wa Korea Kaskazini waondoke Urusi mara moja
  • Rais wa Zambia awatimua majaji wakuu waliotoa uamuzi uliomnufaisha mpinzani wake
  • Hakuna mahali salama mjini Gaza-Daktari
  • Kesi tano mpya zafunguliwa dhidi ya Sean 'Diddy'
  • Mfumo wa Marekani wa kuzuia makombora sasa unapatikana Israel
  • ‘Si Mfalme wangu’, seneta wa Australia amfokea Mfalme Charles
  • Shambulizi latokea dakika chache kabla ya ndege kuwasili
  • Trump asema hana matatizo ya akili au uelewa na kuitisha mtihani kwa wagombea
  • Marekani inachunguza kuvuja kwa mpango wa Israel kushambulia Iran
  • Misri yatokomeza ugonjwa wa malaria - Shirika la Afya Duniani
  • Rais wa Brazil afuta safari ya Urusi baada ya kujeruhiwa kichwa
  • 'Nitagombea urais Putin atakapoondoka'- Mjane wa Navalny
  • Milipuko mipya imesikika Lebanon huku Israel ikiapa kushambulia benki za Hezbollah

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Mpango wa kumaliza mzozo 'mara moja, kwa wote' unajadiliwa - mjumbe wa Marekani

    Marekani imekuwa ikiimarisha juhudi za kidiplomasia kufufua mazungumzo ya kusitisha mapigano katika Gaza na Lebanon.

    Mjumbe maalumu wa rais wa Marekani nchini Lebanon, Amos Hochstein, anasema pande zote zinafanya kazi katika kutengeneza kanuni itakayomaliza mzozo wa Israel na Hezbollah "mara moja na kwa wote".

    Hochstein amesema walikuwa wakijaribu kuweka mifumo ili kuwezesha pande zote kuingia katika enzi mpya ya ustawi.

    "Marekani inataka kumaliza mzozo huu haraka iwezekanavyo," mjumbe anaongeza.

    Alikuwa akizungumza katika mji mkuu wa Lebanon Beirut, ambako amekuwa akikutana na kiongozi mkongwe wa Shia Nabih Berri, ambaye ana jukumu la kufanya mazungumzo kwa niaba ya Hezbollah.

    Unaweza kusoma;

  2. Mashambulizi ya Israel: Tunachokijua kufikia sasa

    Baada ya wimbi la mashambulizi ya Israel kuzikumba benki zenye uhusiano na Hezbollah kote nchini Lebanon jana usiku, vyombo vya habari vya serikali ya Lebanon vimeripoti mashambulizi zaidi kusini mwa Lebanon katika saa chache zilizopita.

    Wizara ya afya ya Lebanon imesema kuwa watu kadhaa wameuawa katika mashambulizi kote nchini humo na Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) linasema kuwa linaendesha mashambulizi "kidogo, ya ndani, yaliyolenga" kusini mwa Lebanon.

    Nchini Israeli, IDF inasema "takribani makombora 60" yamevuka hadi nchini kutoka Lebanon hadi sasa. Kwingineko, huko Gaza, IDF inasema "makumi ya wakazi" wameondoka kwenye kambi ya wakimbizi ya Jabalia, kaskazini, kupitia njia zilizopangwa.

    Kama tulivyoripoti hapo awali, vyombo vya habari vya ndani vimeripoti kuwa watu saba wameuawa kwenye kambi hiyo kufuatia operesheni ya Israeli.

    Wakati huo huo, Marekani imeongeza juhudi za kidiplomasia kufufua mazungumzo ya kusitisha mapigano Gaza na Lebanon, ambapo mjumbe wa Mashariki ya Kati wa Marekani tayari yuko Beirut, na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken kuelekea eneo hilo baadaye leo.

    Afisa wa Hamas ameiambia BBC kwamba vuguvugu hilo huenda likaweka utambulisho wa kiongozi wake mpya, ambao unakusudia kumchagua Machi mwaka ujao,ukawa wa siri kwa sababu za kiusalama.

  3. Kenya yathibitisha kuwa raia wanne wa Uturuki walirejeshwa nyumbani

    Kenya imethibitisha kuwa raia wanne wa Uturuki walirudishwa nchini mwao siku ya Ijumaa, tarehe 18 mwezi Oktoba mwaka 2024, kwa ombi la Serikali ya Uturuki.

    Kenya ilikubali ombi hilo kutokana na mahusiano imara ya kihistoria na kimkakati baina ya nchi hizo mbili, imeeleza taarifa ya Wizara ya Mambo ya nje ya Kenya.

    Raia hao wanne walikuwa wakiishi kwa hadhi ya ukimbizi nchini Kenya.

    Wizara ya masuala ya kigeni imehakikishiwa na mamlaka za Uturuki kuwa watu hao wanne watazingatiwa utu wao kwa mujibu wa sheria za kitaifa na kimataifa.

    Kenya inazingatia faragha na usiri wa raia hao na haitazungumza na vyombo vya habari kuhusu suala hilo mpaka pale uchunguzi wa pande hizo mbili kuhusu jambo hilo utakapokamilika.Ilisema taarifa yake.

  4. Hamas inakusudia kuweka utambulisho wa kiongozi wake mpya kuwa siri

    Afisa wa Hamas ameiambia BBC kwamba vuguvugu hilo huenda likaficha utambulisho wa kiongozi wake mpya kwa sababu za kiusalama (vuguvugu hilo lilifanya vivyo hivyo mwaka wa 2003 kufuatia kuuawa kwa mkuu wa Hamas wakati huo, Sheikh Ahmed Yassin, na Israel mwaka 2003, na mrithi wake, Dk Abdel Aziz al-Rantissi).

    Hamas inanuia kumchagua kiongozi mpya mwezi Machi mwaka ujao lakini hadi wakati huo litaendeshwa na kamati ya watu watano.

    Kamati hiyo itaundwa na Khalil al-Hayya, Khaled Meshaal, Zaher Jabarin, Muhammad Darwish, mkuu wa Baraza la Shura, na mtu wa tano ambaye utambulisho wake bado haujawekwa wazi.

    Afisa huyo alidokeza kwamba Khalil al-Hayya amejitwika jukumu la masuala mengi ya kisiasa na nje ya nchi, pamoja na uangalizi wake wa moja kwa moja wa masuala yanayohusiana na Gaza.

    Anafanya kazi kwa ufanisi kama mkuu wa mpito.

    Afisa huyo aliongeza kuwa Hamas walishangazwa na jinsi Yahya Sinwar alivyouawa wiki iliyopita kwani uelewa wao ulikuwa kwamba alikuwa katika eneo salama zaidi.

    Akizungumzia suala la mateka, afisa huyo alisisitiza kwamba vuguvugu hilo lina uwezo na wafanyakazi kuhakikisha usalama wao, ingawa alijizuia kutoa maelezo maalum.

    Pia alibainisha kuwa kumekuwa na mazungumzo madogo tangu Juni mwaka jana.

    Afisa huyo alifichua kwamba waziri wa mambo ya nje wa Iran alikutana na Khalil al-Hayya siku ya Ijumaa katika mji mkuu wa Uturuki Ankara na kutoa salamu zake za rambirambi kwa kuuawa shahidi Sinwar, na kusema kuwa Iran inatarajia mashambulizi ya Israel dhidi ya Iran yanaweza kutokea wiki moja au chini ya hapo kabla ya uchaguzi wa Marekani.

    Unaweza kusoma;

  5. Mjumbe wa Marekani Mashariki ya Kati awasili Beirut kwa mazungumzo ya kusitisha mapigano

    Mjumbe wa Rais wa Marekani Joe Biden katika Mashariki ya Kati, Amos Hochstein amewasili Beirut katika jaribio la kutafuta mwafaka wa kumaliza vita kati ya Hezbollah na Israel.

    Hii ni ziara ya kwanza ya Hochstein nchini Lebanon tangu Israel ilipoongeza kampeni yake ya kijeshi dhidi ya Hezbollah wiki nne zilizopita.

    Katika safari zake za awali Hochstein amejaribu, na kushindwa, kuzuia vita ambavyo vimesababisha madhara makubwa kwa watu na miundombinu nchini Lebanon.

    Alipofika Beirut, Hochstein alionya kuwa haikuwa kwa manufaa ya Lebanon kuwa na mustakabali wake unaohusishwa na migogoro ya kikanda, akimaanisha uhusiano wa karibu wa Hezbollah na Iran na uamuzi wake wa kuunga mkono Hamas katika mapambano yake na Israel.

    Israel kwa muda mrefu imekuwa ikilalamika kwamba njia hii ilishindwa kuzuia Hezbollah kujenga uwepo wa kijeshi wa kutisha kusini mwa Lebanon na kurusha roketi kaskazini mwa Israeli, sababu inasema ilianza kampeni hii.

    Lakini pande hizo mbili bado ziko mbali sana; haijabainika bado kama Israel au Hezbollah wako tayari kuacha mapigano.

    Unaweza kusoma;

  6. Seoul yataka wanajeshi wa Korea Kaskazini waondoke Urusi mara moja

    Korea Kusini imemwita balozi wa Urusi, ikitaka "kuondoka mara moja" kwa wanajeshi wa Korea Kaskazini ambayo inasema wanapewa mafunzo ya kupigana nchini Ukraine.

    TakribanI wanajeshi 1,500 wa Korea Kaskazini, wakiwemo wale wa kikosi maalum tayari wamewasili nchini Urusi, kwa mujibu wa shirika la kijasusi la Seoul.

    Katika mkutano na balozi Georgiy Zinoviev, makamu wa waziri wa mambo ya nje wa Korea Kusini Kim Hong-kyun alishutumu hatua hiyo na kuonya kwamba Seoul "itajibu kwa hatua zote zinazowezekana".

    Bw Zinoviev alisema atawasilisha jambo hilo, lakini akasisitiza kuwa ushirikiano kati ya Moscow na Pyongyang "uko ndani ya mfumo wa sheria za kimataifa".

    Haijulikani alikuwa akimaanisha ushirikiano gani. Balozi huyo hakuthibitisha madai kuwa Korea Kaskazini imetuma wanajeshi kupigana na jeshi la Urusi.

    Pyongyang pia haijazungumzia madai hayo. Korea Kusini kwa muda mrefu imekuwa ikiishutumu Kaskazini kwa kusambaza silaha kwa Urusi kwa ajili ya matumizi katika vita dhidi ya Ukraine, lakini inasema hali ya sasa imevuka uhamishaji wa vifaa vya kijeshi.

    Baadhi ya ripoti za vyombo vya habari vya Korea Kusini vimesema kuwa wanajeshi 12,000 wa Korea Kaskazini wanatarajiwa kutumwa. "[Hii] sio tu inatishia sana Korea Kusini lakini jumuiya ya kimataifa," Kim alisema Jumatatu.

    Moscow na Pyongyang zimeongeza ushirikiano baada ya viongozi wao Vladimir Putin na Kim Jong Un kutia saini mkataba wa usalama mwezi Juni, wakiahidi kuwa nchi zao zitasaidiana iwapo kutatokea "uchokozi" dhidi ya nchi yoyote ile.

    Unaweza kusoma;

  7. Rais wa Zambia awatimua majaji wakuu waliotoa uamuzi uliomnufaisha mpinzani wake

    Rais wa Zambia Hakainde Hichilema amewafuta kazi majaji watatu wakuu aliowasimamisha kazi hapo awali kwa madai ya utovu wa nidhamu wa kimahakama, na kuibua shutuma zaidi za mahakama kuingiliwa kisiasa.

    Majaji watatu wa Mahakama ya Kikatiba waliongoza ombi la rais mwaka 2016 ambapo walitupilia mbali pingamizi la Hichilema dhidi ya ushindi wa Rais wa zamani Edgar Lungu katika uchaguzi.

    Pia walishiriki katika uamuzi wenye utata uliomruhusu Lungu kugombea katika uchaguzi wa 2021, licha ya kuwa aliwahi kuwa rais wa Zambia mara mbili.

    Kufukuzwa kwao kumekuja baada ya kushindwa katika ombi la mahakama la kutaka kuhakiki uamuzi wa jopo la mahakama uliopendekeza kusimamishwa kwao kazi.

    Siku ya Jumapili jioni, taarifa iliyotolewa na ofisi ya rais ilisema "wameondolewa mara moja" kufuatia pendekezo la Tume ya Malalamiko ya Mahakama (JCC).

    "Kuondolewa kwa majaji ni kutekeleza mamlaka aliyopewa Rais chini ya [katiba ya Zambia]," ilisema.

    JCC ilikuwa imewachunguza kuhusu madai ya utovu wa nidhamu uliokithiri kufuatia malalamiko ya Moses Kalonde, ambaye ni raia wa kawaida.

    Mwaka jana, JCC ilikataa malalamiko ya wakili Joseph Busenga, ambaye aliwasilisha ombi la kuondolewa kwa majaji hao watatu, kwa madai kwamba walishughulikia vibaya ombi la uchaguzi wa 2016.

    Kumekuwa na maoni tofauti kuhusu kutimuliwa kwa majaji hao.

    Mvutano wa kisiasa umekuwa ukiongezeka nchini Zambia kabla ya uchaguzi wa mwaka 2026, wakati Hichilema na Lungu wanatarajiwa kuchuana kwa mara ya nne.

  8. Hakuna mahali salama mjini Gaza-Daktari

    Daktari anayefanya kazi huko Gaza amesema yeye na wenzake wanafanya kazi katika "eneo la vita", akielezea jinsi risasi iliyopotea ilivyoingia katika hospitali yake katika siku za hivi karibuni.

    Dkt Clare Frost, daktari mkuu kutoka Cardigan, Ceredigion, alisema ni "mazingira yenye changamoto na uhasama kuwa mfanyakazi wa afya".

    Dk Frost, 38, ambaye anaendesha hospitali katikati mwa Gaza, pia alielezea hali ya kibinadamu katika eneo hilo, akisema "idadi ya watoto wenye utapiamlo inaongezeka" kila wiki.

    Umoja wa Mataifa umeonya kwamba "hatari ya njaa inaendelea katika Ukanda wote wa Gaza".

    Dk.Frost, ambaye amekuwa akifanya kazi Gaza tangu Septemba, alisema kituo chake cha al-Zawaida, katikati mwa Gaza, kinawahudumia wagonjwa kati ya 300 na 400 kwa siku.

    "Tunashughulika na watu ambao wanahusika katika matukio ya vifo vya watu wengi, kutokana na mashambulizi ya anga, tunaona watu wakiwa na majeraha ya kukatwa na kiwewe, majeraha ya mlipuko, kuvunjika kwa viungo vingi," aliiambia BBC Radio Wales Breakfast.

    "Maambukizi ya maradhi ya ngozi, magonjwa ya njia ya upumuaji, cha kusikitisha ni kwamba haya ni mambo rahisi kutibu lakini kwa sasa hatuna dawa ya kutibu haya," alisema.

    Dk Frost, ambaye anaendesha hospitali kwa shirika la misaada la UK-Med, alisema hapo awali alikuwa akifanya kazi katika mazingira magumu ya kibinadamu, lakini "sijawahi kuwa na ukosefu wa vitu vya msingi vinavyohitajika kuwa daktari".

    Alisema glavu na nguo za kuvaa ni "haba kwa muda mrefu", na pia kuna "ukosefu mkubwa wa dawa".

    Unaweza kusoma;

  9. Kesi tano mpya zafunguliwa dhidi ya Sean 'Diddy'

    Mashtaka matano mapya yamefunguliwa dhidi ya Sean "Diddy" Combs katika mahakama ya shirikisho huko New York.

    Wanaume wawili na wanawake watatu wanamshutumu nguli huyo wa hip-hop kwa kuwanyanyasa kingono kwenye karamu mbalimbali huko LA, New York na Las Vegas.

    Mlalamikaji mdogo alikuwa 13 wakati wa tukio la madai.

    Bwana Combs bado yuko kizuizini katika jela ya Brooklyn. Kando na hayo anakabiliwa na mashtaka ya biashara ya ngono na ulaghai, ambayo anakanusha.

    BBC imewasiliana na timu yake ya wanasheria ili kupata maoni yao kuhusu kesi hizo mpya.

    Mawakili wake hivi karibuni walipuuzilia mbali msururu wa kesi hizo wakisisitiza kwamba "Bw Combs hajawahi kumnyanyasa mtu yeyote kingono, mtu mzima au mdogo, mwanaume au mwanamke." Kesi zote tano mpya za madai kwamba Bw Combs, au kwa wakala kupitia washirika wake, alikunywa vileo katika matukio ambayo yaliwafanya walalamikaji kupata kizunguzungu, kichefuchefu na kutojitambua.

    Katika kesi kadhaa, walalamikaji wanadai kuwa Bw Combs aliwabaka, kuwalazimisha ngono ya mdomo, au kuwapapasa .

    Bw Combs kwa sasa anasubiri kesi yake Mei mwaka ujao kwa mashtaka ya biashara ya ngono na ulaghai. Anakabiliwa na kifungo cha maisha jela ikiwa atapatikana na hatia.

    Msanii huyo wa muziki wa hip-hop amekana mashtaka yote na amenyimwa dhamana mara kadhaa.

    Shitaka hilo pamoja na mashitaka kadhaa, yanahusisha makampuni yake mbalimbali ya biashara, kwa madai yalishiriki katika kuwezesha na kufadhili vitendo vyake vya unyanyasaji ndani na nje ya tasnia ya muziki.

    Kesi hizo zinamshutumu zaidi Bw Combs kwa kutumia nguvu na ushawishi wake katika burudani kutumia hila, kuwatisha, na kuwanyamazisha wale walio karibu naye.

    Unaweza kusoma;

  10. Mfumo wa Marekani wa kuzuia makombora sasa unapatikana Israel

    Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin amesema mfumo wa kuzuia makombora ambao Marekani ilituma Israel sasa unapatikana nchini humo.

    Austin hangeweza kusema ikiwa mfumo huo unafanya kazi, lakini, akizungumza wakati wa ziara yake nchini Ukraine, alisema: "Tuna uwezo wa kuuwezesha kufanya kazi haraka sana na tuko ndani ya matarajio yetu."

    Maafisa wanasema mfumo wa ulinzi wa Terminal High Altitude Area, unaojulikana kama THAAD, utaimarisha ulinzi wa anga wa Israel.

    Inajumuisha kutumwa kwa wanajeshi wapatao 100 wa Marekani.

  11. ‘Si Mfalme wangu’, seneta wa Australia amfokea Mfalme Charles

    Mfalme Charles amefokewa na seneta huru aliyemwambia "wewe si Mfalme wangu" mara tu alipomaliza kuhutubia katika Bunge la Australia siku ya pili ya ziara yake rasmi nchini humo.

    Lidia Thorpe alikatiza hafla hiyo kwa kupiga kelele kwa takriban dakika moja kabla ya kusindikizwa na usalama akitolewa nje.

    Mfalme alikuwa ametoka tu mbele kuzungumza na akawa anakwenda kuungana tena na Malkia Camilla aliyekuwa ameketi kwenye jukwaa wakati Thorpe alipoanza kupiga kelele.

    Baada ya kutoa madai ya mauaji ya kimbari dhidi ya "watu wetu", alisikika akipiga kelele: "Hii si ardhi yako, wewe si Mfalme wangu."

    Sherehe ilihitimishwa bila kurejelea tukio hilo, na wanandoa wa kifalme waliendelea kukutana na mamia ya watu ambao walikuwa wamesubiri nje kuwasalimu.

    Australia ni nchi ya Jumuiya ya Madola ambapo Mfalme huudumu kama mkuu wa nchi.

    Baadaye, Thorpe aliiambia BBC kuwa alitaka kutuma "ujumbe wazi"

    Alisema Mfalme alihitaji kuagiza Bunge kujadili makubaliano ya amani na watu wa kwanza.

    "Tunaweza kuongoza hilo, tunaweza kufanya hivyo, tunaweza kuwa nchi bora zaidi - lakini hatuwezi kumsujudia mkoloni, ambaye mababu zake aliowazungumzia humo wanahusika na mauaji ya halaiki."

  12. Mashambulizi yatokea karibu na uwanja wa ndege wa Beirut dakika chache kabla ya ndege kuwasili

    Israel imefanya mashambulizi zaidi ya anga huko Beirut na Lebanon usiku kucha, yakilenga matawi ya benki ya AQAH.

    Shirika la habari la serikali ya Lebanon NNA liliripoti shambulizi kwenye tawi la benki hiyo karibu na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Rafic Hariri mjini Beirut.

    Hadi shambulizi lilipotokea mwendo wa saa 23:45 kwa saa za eneo, uwanja wa ndege ulikuwa ukifanya kazi kama kawaida.

    Ndege kutoka Dubai, iliyopaswa kutua saa 23:59, ilichelewa kuwasili kwa dakika 17.

    Soma zaidi:

  13. Trump asema hana matatizo ya akili au uelewa na kuitisha mtihani kwa wagombea

    Trump amesema anafikiria wagombea wote wa urais wanapaswa kupewa mtihani wa uelewa, huku akisisitiza kwamba yuko sawa kiafya ya akili na muafaka kuingia madarakani.

    Akimzungumzia Kamala Harris huko Pennsylvania, alisema: "Sina tatizo la uelewa – lakini yeye anaweza kuwa na tatizo hilo."

    Trump mwenye umri wa miaka 78 aliambia ukumbi wa jiji la Lancaster: "Kwa kweli natoa wito wa mtihani wa uelewa kwa watu wote wanaotaka kugombea urais. Sio kulingana na umri. Sina miaka 80, na siko karibu miaka ya 80.

    "Upande wa Biden, ana miaka 81 au 82, na unajua, hiyo inaeleweka".

    Trump aliendelea: "Tumekuwa na baadhi ya viongozi bora katika historia ya dunia ambao wako katika miaka ya 80. Nimefanya mtihani mara mbili na niliwashinda wote wawili. Daktari wakati mmoja alisema, 'Sijawahi kuona mtu bora kama wewe."

    Trump anasema aliambiwa mtihani wa lazima wa afya ya akili utakuwa kinyume na katiba.

    Kampeni ya Harris imerudia kutilia shaka afya ya kiakili ya Trump na kumkosoa kwa kukataa kutoa rekodi zake za matibabu.

    Soma zaidi:

  14. Marekani inachunguza kuvuja kwa mpango wa Israel kushambulia Iran

    Marekani inachunguza uvujaji wa nyaraka za siri zinazoelezea tathmini ya Marekani kuhusu mipango ya Israel kushambulia Iran, Spika wa Baraza la Wawakilishi Mike Johnson amethibitisha.

    Nyaraka hizo ziliripotiwa kuchapishwa mtandaoni wiki iliyopita na zinasemekana kuelezea picha za satelaiti zinazoonyesha Israel ikihamisha zana za kijeshi kwa ajili ya kujiandaa kukabiliana na shambulio la kombora la Iran tarehe 1 Oktoba.

    Nyaraka hizo, ambazo ni siri kuu, zinaweza kusambazwa ndani ya muungano wa mashirika ya kijasusi wa ‘Five Eyes’ wa Marekani, Uingereza, Kanada, New Zealand na Australia, CBS, mshirika wa BBC wa Marekani, aliripoti.

    Kwa wiki kadhaa Israel imekuwa ikiamua jinsi na wakati wa kujibu shambulio la hivi punde la kombora la Iran. Waziri wa ulinzi wa Israel ameonya kuwa litakuwa "Kali, sahihi na la kushangaza".

    Nyaraka hizo mbili zinaripotiwa kuhusishwa na Shirika la Kitaifa la Ujasusi la Geospatial la Marekani na Shirika la Usalama wa Taifa (NSA), na zilichapishwa kwenye akaunti ya Telegram inayofungamana na Iran siku ya Ijumaa.

    Johnson, mwanachama wa ngazi ya juu zaidi wa Congress, aliiambia CNN Jumapili kwamba "uvujaji huo unatia wasi wasi sana".

    "Kuna madai mazito yanayotolewa, uchunguzi unaendelea, na nitapata maelezo mafupi juu ya hilo baada ya saa chache," mjumbe huyo wa Republican wa Louisiana alisema.

    Pentagon ilithibitisha katika taarifa yake kwamba inafahamu ripoti kuhusu hati hizo, lakini haikutoa maoni zaidi.

    Mashirika ya Marekani yanayohusika, pamoja na serikali ya Israel, hazijatoa maoni yao hadharani kuhusu uvujaji huo.

    CNN na Axios kwanza ziliripoti uvujaji huo, ambao unathibitisha kwa mara nyingine tena kwamba Marekani huichunguza mshirika wake wa karibu Israel.

    Hati moja inarejelea uwezo wa nyuklia wa Israeli - ambayo Marekani na Israel kamwe hawajakiri rasmi – na kufutilia mbali matumizi ya chaguo kama hilo katika shambulio lolote lililopangwa .

    Afisa mmoja wa zamani wa ujasusi wa Marekani aliiambia BBC kuwa kutolewa bila kibali kwa hati hizo pengine ni jaribio la kufichua ukubwa wa ulipizaji kisasi uliopangwa, kwa lengo la kuuvuruga.

    Marekani inachunguza iwapo taarifa hizo zilifichuliwa kimakusudi na ajenti wa Marekani, au iwapo ziliibwa, pengine kwa njia ya udukuzi, maafisa waliambia Associated Press (AP).

    Nyaraka hizo mbili zinaonekana kutegemea taarifa za satelaiti zilizopatikana kuanzia tarehe 15-16 Oktoba.

    Soma zaidi:

  15. Misri yatokomeza ugonjwa wa malaria - Shirika la Afya Duniani

    Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) limethibitisha kwamba Misri haina malaria - jambo ambalo shirika la afya ya umma la Umoja wa Mataifa lilisema ni "la kihistoria".

    "Malaria ni ya zamani kama ustaarabu wa Misri yenyewe, lakini ugonjwa ambao uliwasumbua mafarao sasa ni historia," mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus alisema.

    Mamlaka ya Misri ilizindua juhudi zao za kwanza kukomesha ugonjwa hatari wa kuambukiza unaoenezwa na mbu karibu miaka 100.

    Uidhinishaji hutolewa wakati nchi inapothibitisha kuwa mkondo wa usambazaji umekatizwa kwa angalau miaka mitatu mfululizo iliyopita.

    Malaria huua watu wasiopungua 600,000 kila mwaka, karibu wote ni kutoka barani Afrika.

    Soma zaidi:

  16. Rais wa Brazil afuta safari ya Urusi baada ya kujeruhiwa kichwa

    Rais wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva amekatisha safari yake kuelekea Urusi baada ya kuumia kichwa katika ajali iliyotokea nyumbani siku ya Jumamosi.

    Lula mwenye umri wa miaka 78 alipangiwa kusafiri siku ya Jumapili alasiri kwa mkutano wa Brics - kundi la nchi zinazoendelea zikiwemo Brazil, Urusi, India, China na Afrika Kusini.

    Hospitali kuu katika mji mkuu Brasília ilisema ilimshauri rais kuepuka safari za ndege za masafa marefu kwa muda.

    Sasa atashiriki katika mikutano kwa njia ya video.

    Katika taarifa, Hospitali ya Sírio-Libanês huko Brasília ilisema rais alishauriwa dhidi ya kusafiri umbali mrefu, lakini anaweza kuendelea na shughuli zingine kama kawaida.

    Iliongeza kuwa Lula alipata jeraha sehemu ya nyuma ya kichwa na anafuatiliwa na madaktari.

    Ofisi ya rais ilisema atashiriki katika mkutano huo kutoka Brasília na ataendelea na kazi yake nyingine.

    Ofisi yake haikufichua maelezo yoyote kuhusu jeraha lake.

    Pia unaweza kusoma:

  17. 'Nitagombea urais Putin atakapoondoka'- Mjane wa Navalny

    Yulia Navalnaya anakusudia kuwa rais wa Urusi, amezungumza na BBC.

    Anaangalia moja kwa moja machoni. Hakuna kusitasita wala kuyumba.

    Hili, kama maamuzi mengi aliyofanya na mumewe, kiongozi wa upinzani Alexei Navalny, halina utata.

    Navalnaya anajua atakuwa katika hatari ya kukamatwa iwapo atarejea nyumbani wakati Rais Putin angali madarakani.

    Utawala wake umemshutumu kwa kushiriki katika itikadi kali.

    Hili si tishio tu la bure. Na nchini Urusi, inaweza kusababisha kifo.

    Mumewe, mkosoaji mkubwa wa Rais Putin, alihukumiwa kifungo cha miaka 19 kwa itikadi kali, mashtaka ambayo yalionekana kuchochewa kisiasa.

    Alifariki dunia mnamo Februari katika gereza la adhabu ya kikatili huko Arctic Circle.

    Rais wa Marekani Joe Biden alisema "hakuna shaka" Putin ndiye wa kulaumiwa.

    Hata hivyo, Urusi inakanusha kumuua Navalny.

    Yulia Navalnaya, akiwa ameketi kwa mahojiano na BBC katika maktaba ya kisheria ya London, anaonekana na kusikika kila inchi kama mrithi wa Navalny, wakili huyo aligeuka mwanasiasa ambaye ana ndoto ya Urusi tofauti.

    Anapozindua kumbukumbu ambayo mumewe alikuwa akiandika kabla ya kifo chake, Yulia Navalnaya alirejelea mipango yake ya kuendeleza vita vyake vya demokrasia.

    Wakati ufaao, "Nitashiriki katika uchaguzi ... kama mgombea," aliiambia BBC.

    “Mpinzani wangu wa kisiasa ni Vladimir Putin. Na nitafanya kila kitu utawala wake uanguke haraka iwezekanavyo”.

    Soma zaidi:

  18. Milipuko mipya imesikika Lebanon huku Israel ikiapa kushambulia benki za Hezbollah

    Israel imefanya mashambulizi zaidi ya anga huko Beirut na kusini mwa Lebanon, ikiwa ni pamoja na matawi ya benki ambayo inasema inaunga mkono Hezbollah.

    Milipuko ilisikika katika wilaya ya Dahieh ya Beirut kusini, eneo linalodhibitiwa na Hezbollah, pamoja na Bonde la Bekaa na kusini mwa Lebanon. Bado haijulikani ikiwa kuna majeruhi wowote.

    Jeshi la Israel awali lilionya watu wanaoishi katika maeneo 25 nchini Lebanon - ikiwa ni pamoja na 14 katika mji mkuu Beirut - kwamba ilipanga kufanya mashambulizi usiku kucha.

    Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) pia lilisema litalenga benki na miundombinu mingine ya kifedha inayosaidia Hezbollah.

    Katika taarifa iliyotolewa Jumapili jioni, msemaji wa IDF Adm Daniel Hagari alionya kwamba "mtu yeyote aliye karibu na maeneo yanayotumiwa kufadhili shughuli za ugaidi za Hezbollah lazima aondoke kwenye maeneo haya mara moja".

    "Tutashambulia maeneo lengwa kadhaa katika saa zijazo na maeneo mengine lengwa zaidi usiku kucha," alisema.

    "Katika siku zijazo, tutafichua jinsi Iran inavyofadhili shughuli za kigaidi za Hezbollah kwa kutumia taasisi za kiraia, vyama na mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo yanatumika kama vyanzo vya pesa za ugaidi," msemaji huyo wa Israel aliongeza.

    Shirika la habari la serikali ya Lebanon NNA liliripoti mashambulizi kwenye matawi ya benki ya Al-Qard Al-Hassan association, ikiwa ni pamoja na Mashariki ya Bekaa Valley.

    Soma zaidi:

  19. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 21/10/2024