Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Maalim Seif: Zitto ahoji polisi kuzuia kongamano la kiongozi wa upinzani Zanzibar
Kiongozi wa chama cha upinzani Tanzania cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe amelaani kitendo cha jeshi la polisi visiwani Zanzibar kuzuia kongamano la kuadhimisha miaka tisa ya maridhiano ya Wazanzibari licha ya kamanda wa polisi visiwani humo kukanusha madai waliuvunja mkutano huo.
Akizungumza na BBC Zitto alisema: ''Kongamano lilikua linaendelea akaja mkuu wa polisi wa kituo cha Malindi na kutoa amri mbili, amri ya kwanza ni ya kulisimamisha Kongamano na amri ya pili ni ya Maalim Seif kutakiwa kituo cha polisi baada ya hapo viongozi wetu wasaidizi wa Maalim walitoka nae kwaajili ya kwenda kuitikia wito na baadae ikabidi mkutano usimamishwe kwasababu polisi waliomba mkutano usimamishe ''
Mbunge huyo wa Kigoma Mjini amesema kuvunjwa kwa kongamano hilo na polisi kumtaka Maalim Seif kuondoka ukumbini ni kinyume na sheria na taratibu.
Kwa mujibu wa naibu katibu wa kamati ya habari Zanzibar wa ACT-Wazalendo, Seif Hamad amesema mara baada ya kuvunjika kwa kongamano hilo Maalim Seif aliombwa kuondoka, kusindikizwa na polisi.
Taarifa za awali zilielezea kuwa mwanasiasa huyo mkongwe na mkosoaji mkubwa wa uongozi wa Mohammed Shein wa na Chama Cha Mapinduzi CCM, visiwani humo alikwenda polisi kuitikia wito
Lakini Bw. Zitto aliongeza kuwa baada ya mashauriano ya kisheria na kutokana na hadhi ya Maalim Seif wakaonelea ni vyema Seif arejee nyumbani na kama kuna wito wa polisi ''basi wito huo uje rasmi'' kwa mujibu wa taratibu za sheria.