Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kenya yaizamisha Tanzania 3-2 AFCON 2019
Ubishi umekwisha, Kenya ni mbabe wa Tanzania.
Baada ya presha kupanda na kushuka kwa muda mrefu nje ya uwanja, dakika 90 za ndani ya uwanja zimetoa majibu.
Kenya imewafunga Tanzania goli 3-2.
Haukuwa ushindi mwepesi kwa Kenya hata hivyo.
Tanzania ilitangulia kuchukua uongozi katika dakika ya sita ya mchezo kupitia mshambuliaji Simon Msuva aliyemalizia shambulio kali lililoanzia kwa nahodha Mbwana Samatta.
Michael Olunga akaisawazishia Kenya katika dakika 39 kwa bao safi la tiki taka, lakini dakika mbili baadaye, nahodha wa Tanzania akairudishia timu yake uongozi katika dakika ya 41 baada ya kuipangua safu ya ulinzi ya Kenya.
Kipindi cha kwanza kikaisha kwa Tanzania kuwa kifua mbele kwa goli 2-1.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi, huku safu ya kiungo ya Kenya ikiongozwa na nahodha Victor Wanyama ikiutawala mchezo huo.
Kenya pia ilionekana dhahri kuwashinda Tanzania katika kucheza mipira ya juu.
Johanna Omollo aliirudisha Kenya mchezoni katika dakika ya 62 kwa kupiga kichwa kikali katika eneo la hatari la Tanzania bila kubughudhiwa na walinzi wa Tanzania.
Baada ya hapo Kenya waendelea kulisakama lango la Tanzania, na ilikuwa ni Michael Olunga tena ambaye aliizamisha Tanzania kwa kufunga goli lake la pili na la tatu kwa Kenya katika dakika ya 80.
Olunga ndiye aliyeibuka mchezaji bora wa mechi hiyo.
Dakika 10 za mwisho Tanzania walijitahidi kupenya safu ya ulinzi ya Kenya bila mafanikio yoyote.
Ushindi huu ni wa kwanza kwa Kenya katika mashindano ya mwaka huu na wa pili katika mashindano yote sita ya Afcon waliyoshiriki.
Takwimu za mchezo zinaonesha kuwa timu hizo zilikuwa sawa kwenye umiliki wa mpira, yaani wote walimiliki kwa asilimia 50.
Kenya ilipiga mashuti 14, kati ya hayo 12 yakilenga goli.
Tanzania lipiga mashuti 12, tisa yakilenga goli.
Ushindi wao wa kwanza ulikuwa mwaka 2004 walipoilaza Burkina Faso kwa magoli 3-0. Magoli yaliyofungwa na Emanuel Ake, Dennis Oliech na John Baraza.
Tayari matokeo ya mchezo huo yamepokewa kwa hisia mbalimbali kutoka kwa mashabiki.
Kiongozi wa upinzani Kenya Raila Odinga ambaye alijitutumua kabla ya mchezo kuw hakuna cha kuwasimamisha Kenya amepokea kwa mikono miwili ushindi huo.
Mashabiki wa Tanzania wamekuwa wakijipa moyo, na kusifu timu yao kwa kiwango walichoonesha usiku wa leo.
Tanzania ilipoteza mchezo wa kwanza dhidi ya Senegal kwa goli 2-0.
Kenya ilipoteza mchezo wa kwanza pia kwa goli 2-0 dhidi ya Algeria.
Tanzania itamalizia mchezo wake wa mwisho dhidi ya Algeria ambao wameshafuzu kwenda hatua ya mtoano siku ya Jumatatu.
Je Tanzanzania itashinda aka kuambulia walau alama moja?
Kenya wao watashuka dimbani dhidi ya Senegal ambao wamejeruhiwa na Algeria kwa kufungwa moja bila.
Endapo Kenya itashinda, itafuzu moja kwa moja.
Wanaweza pia kufuzu endapo watatoka sare.