Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kasuku aina ya kakapo wapo kwenye hatihati ya kupotea na upasuaji huo ni jitihada za kuwaokoa
Madaktari wa Wanyama nchini New Zealand wamemfanyia upasuaji kasuku mmoja kutoka jamii ya kakapo ambayo ipo hatarini kutoweka.
Madaktari hao wa upasuaji, walitumia mbinu za upasuaji zinazotomika kwa binadamu na wanyama wengine jamii ya mamalia kumfanyia upasuaji kifaranga hicho cha kasuku chenye siku 56.
Kifaranga hicho kilikuwa na tundu kwenye fuvu.
Kakapos - ndiyo kasuku wanene zaidi duniani - hawapai na hutoka usiku tu. Hata hivyo aina hiyo ya kasuku ipo hatarini kutoweka kutokana na kuwindwa na majangili na wanyama wengine wa mwituni.
Kwa sasa kuna kasuku jamii ya kakapos 144 tu duniani, na wana asili ya visiwa vya New Zealand.
Kifaranga hicho kilicopewa jina la Espy 1B, kilitotolewa katika kisiwa cha Codfish kusini mwa New Zealand na kipo chini ya uangalizi wa Idara ya Uhifadhi ya kisiwa hicho, na wafanyakazi wa kitengo hicho ndio waligundua uvimbe kichwani mwake.
Kifaranga hicho kilisafirishwa bure na shirika la ndege la nchi hiyo mpaka kwenye hospitali ya wanyama ya Wildbase ya Chuo Kikuu cha Massey ambapo upasuaji huo ulifanyika.
Katika taarifa iliyotolewa na mkurugenzi wa hospitali hiyo, Profesa Brett Gartrell, amesema kulikuwa na ngozi nyembamba sana iliyotenganisha ubongo wa kifaranga hicgo na dunia.
"Shimo hilo liliruhusu sehemu ya ubongo kutokeza na kusabaisha uvimbe."
Profesa huyo pia amesema upasuaji huo hatari wa ubongo ilibidi ufanyike ili kunusuru maisha ya ndege huyo, lakini pia alikiri kuwa: "kitu kama hicho hakijawahi kufanyika kwenye historia ya matibabu ya ndege."
Kwa ujumla hospitali ya Wildbase inasema upasuaji huo uliofanyika wiki iliyopita umefanikiwa na kifaranga hicho kinaendelea vizuri.
Kasuku wa jamii ya kakapos walikuwa ni moja ya jamii kubwa ya ndege nchini New Zealand, lakini sasa Shirika la Kimataifa la Uhifadhi wa Maliasaili (IUCN) limeiweka jamii hiyo ya kasuku kama wanyama ambao wamo hatarini kuangamia.
Hivi karibuni, jamii hiyo ya kasuku iliweza kupata msimu bora zaidi wa kuzaliana katika miaka ya hivi karibuni.