Mabasi mapya ya utalii yaanza kutumiwa Rwanda

Chanzo cha picha, HISANI/JIJI LA KIGALI
Mabasi hayo yanatarajiwa kurahisisha usafiri wa watalii wanaoizuru Rwanda yameanza kutumiwa wiki hii jijini Kigali
Wazo la kuanzisha usafiri huo lilianzishwa na mjasiliamali wa Kinyarwanda Augustin Munyandamutsa.
Munyandamutsa, aliliambia gazeti la Sunday Times nchini humo kuwa mchakato wa kuleta mabasi hayo ya utalii utamalizika mwishoni mwa mwezi Agosti mwaka huu.
Walioshuhudia mabasi hayo wanaulinganisha muundo wake na ule wa mabasi ya utalii wa jiji la London,(London buses).

Chanzo cha picha, HISANI/JIJI LA KIGALI
Basi moja lina thamani ya franga za Rwanda milioni 160, kila basi likiwa na uwezo wa kuwasafirisha watalii 200 kila siku, kuwapeleka katika maeneo ya utalii yakiwemo yale yanayoelezea historia ya jiji la kigali.
Ripoti mpya imeonyesha kuwa utalii wa ndani ndio unaoongoza kwa katika sekta ya utalii nchini Rwanda.

Chanzo cha picha, HISANI/JIJI LA KIGALI
Raia wa kigeni hulipa dola $50 kwa mizunguko mitatu huku raia na wakazi pamoja na raia wa mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wakilipa franga za Rwanda 25, 000 kwa mizunguko hiyo.
- https://www.bbc.com/swahili/medianuai/2016/05/160510_tanzania_new_buses

Katika miaka ya hivi karibuni baadhi ya nchi za Afrika mashariki zimekuwa zikiimarisha sekta ya usafiri wake ili kukabiliana na msongamano mkubwa wa magari, unaokwamisha shuguli nyingi kwenye miji.
Nchini Tanzania huduma ya mabasi ya uchukuzi yanayoenda kwa kasi BRT ilianzishwa mwaka 2016 katika jiji la kibiashara la Dar es Salaam Tanzania, na kupunguza adha ya foleni za magari jijini humo.

Chanzo cha picha, HISANI/KENHA
Nchini Kenya serikali ilianzisha mpango wa kutenga mkondo mmoja kwenye barabara kuu ya Thika wa kutumiwa na mabasi ya kubeba abiria jijini Nairobi mwezi Mei mwaka jana, kwa lengo la kupunguza msongamano mkubwa wa magari jijini humo.
Hata hivyo mpango huo ambao ulipingwa na watumiaji wa barabara za jiji haujaanza kutekelezwa kama ilivyotarajiwa.













