Mahakama: 'Kuendesha gari baada ya kunywa pombe sio makosa Kenya'

Mahakama moja ya kiambu nchini Kenya imetoa uamuzi wa kipekee ikisema kuendesha gari baada ya kunywa pombe sio makosa iwapo dereva huyo amelidhbiti vya kutosha gari analoendesha.

Kulingana na mtandao wa runinga ya Citizen nchini Kenya ,hakimu mkaazi wa Kiambu Bryan Khaemba alitoa uamuzi huo katika kesi ambapo dereva Michael Ngobe Mugo ameshtakiwa kwa makosa ya kuendesha gari chini ya shinikizo la pombe.

Mahakama hiyo iliamuru kwamba kwa dereva ambaye anaendesha gari kuwa mlevi na kupatikan na makosa , ni sharti mwendesha mashtaka kuwa na ushahidi wa kutosha kwamba dereva huyo alishindwa kulidhibiti gari hilo.

Bwana Mugo alishtakiwa kwamba mnamo tarehe 23 mwezi Mei 2018 akiwa anaendesha gari katika barabara ya Banana-Ruaka mjini Kiambu , aliendesha gari hilo akiwa mlevi hivyobasi hakuwa na udhibiti mzuri wa gari lake.

Kulingana na mtandao huo afisa mmoja wa trafiki ambaye alitoa ushahidi katika kesi hiyo alisema kuwa mshtakiwa huyo aliwashinda nguvu yeye na wenzake wawili hivyobasi wakashindwa kumkamata.

''Hilo haliwezekani kwa mtu ambaye anadaiwa kuwa mlevu chakari '', ulisema uamuzi huo.

Huku akifutilia mbali kesi hiyo mahakama hiyo ilisema kuwa mshtakiwa hakuathiriwa na pombe hiyo , sababu iliowafanya maafisa hao kushindwa kumkamata.

''Naamuru kwamba upande wa mashtaka ulishindwa kuwakilisha kesi yenye ushahidi mzuri dhidi ya mshukiwa kwa kushinda kutoa ushahidi kwamba alishindwa kulidhibiti gari alilokuwa akiendesha'', alisema hakimu mkuu mkazi Khaemba.

Mahakama iliongezea kwamba kuendesha gari chini ya shinikizo la pombe sio makosa.