Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Mwanafunzi ashtakiwa wizi kwa kuponda pesa alizotumiwa kimakosa Afrika Kusini
Mwanafunzi wa kike wa Afrika Kusini ambaye alitumia zaidi ya dola $63,000 kati ya dola milioni moja na laki moja ($1.1m) alizopokea kimakosa amefikishwa mahakamani kwa mashtaka ya wizi .
Mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 28, anayesoma masomo ya uhasibu katika Chuo Kikuu cha Walter Sisulu, alikamatwa na polisi wa kitengo kinachokabiliana na uhalifu mkubwa baada ya kumtaka ajisalimishe kwapolisi, amesema Anelisa Feni, msemaji wa kitengo hicho maalumu katika mahojiano na waandishi wa habari.
Mwaka jana Sibongile Mani alikuwa anafaa kupokea kiwango dola $110 kwa mwezi kama pesa ya chakula kutoka hazina ya kitaifa za msaada wa karo ya wanafunzi (NSFAS ), unaowasaidia wanafunzi wanaotoka katika jamii zisizojiweza kiuchumi.
Hata hivyo, mwezi Juni alitumiwa dola milioni moja na laki moja $1.1m, na alipogundua hilo alianza kuzitumia kiholela .
Alitumia dola $63,000 kujisherehesha na kununua nguo za bei ya juu.
Mara baada ya Hazina ya Kitaifa za Msaada wa Karo ya Wanafunzi kubaini makosa yake miezi mitatu baadae, iliweza kupata ujumbe wa taarifa za pesa kutoka kwenye akaunti ya benki ya Sibongile Mani.
Bi Mani hakuambiwa akiri mashtaka alipofikishwa kortini Jumanne, badala yake mahakama ikaamua kumuonya na kumuagiza arejee mahakamani tena tarehe 2 Julai.
Watu mtandaoni walikuwa na maoni tofauti huku baadhi kwenye Twitter wakimkosoa na wengine wakimuhurumia.
Awali Chuo Kikuu cha Walter Sesulu kilisema kuwa makosa hayo yakijulikana baada ya risiti ya akaunti ya mwanafunzi huyo kuonyesha kuwa na mamilioni ya pesa baada ya kuwekwa katika mtandao wa kijamii.
Msemaji wa Chuo hicho Yonela Tukwayo, alisema kuwa pesa hizo ziliwekwa kwenye akaunti hiyo kimakosa na kampuni ambayo inasimamia fedha za hazina ya kitaifa za msaada wa karo ya wanafunzi (NSFAS) ambayo inajulikana kama Intellicard na kwamba ni sharti mwanafunzi huyo arejeshe fedha hizo.
Ripoti ya shirika la habari la EWN ilionesha picha za kwenye mitandao ya kijamii, zikionyesha mwanafunzi huyo Bi Mani akijisifu na kujionyesha kwenye sherehe moja huku akijiburudisha na vitu vizuri vizuri, kama vile simu mpya ya mkononi.