Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Munyakazi kushtakiwa katika mahakama ya Rwanda
Rwanda imesema mtuhumiwa wa mauaji ya kimbari Leopold Munyakazi aliyekabidhiwa nchi hiyo na Marekani, atashitakiwa katika mahakama za kawaida na siyo mahakama maalumu kama inavyotokea kwa watuhumiwa wengine wa mauaji ya kimbari, wanaokabidhiwa Rwanda kutoka mataifa ya kigeni.
Bwana Munyakazi mwenye umri wa miaka 65, anakabiliwa na mashitaka kadhaa yakiwemo kupanga na kutekeleza mauaji,kuuwa kwa kukusudia,kuwachochea wanamugambo wa kihutu kuwauwa watutsi na makosa mengine yenye uhusiano na mauaji ya kimbari.
Yote hayo kwa mujibu wa ofisi ya mashtaka, aliyatekeleza katika kijiji chake cha Kayenzi mkoa wa kusini
Bwana Munyakazi aliwahi kushitakiwa kwa makosa hayo nchini Rwanda kabla ya kuachiwa huru kwa dhamana mwaka 1999.
Wakati upelelezi ulipokuwa unaendelea dhidi yake alitoroka Rwanda na kukimbilia Marekani mwaka 2004.
Akiwa Marekani alipata uraia na kuwa mhadhiri katika chuo kikuu nchini humo. Marekani imemtimua kwa makosa ya kudanganya mamlaka zake za uhamiaji.