Tunachojua kuhusu milipuko ya vifaa vya mawasiliano vya Hezbollah

Maelfu ya watu wamejeruhiwa nchini Lebanon, baada ya vifaa vya mawasiliano vinavyotumiwa na kundi lenye silaha la Hezbollah kuwasiliana kwa kiasi kikubwa kulipuka karibu wakati huo huo nchini kote siku ya Jumanne.
Takriban watu tisa waliuawa na wengine 2,800 kujeruhiwa, wengi wao vibaya sana.
Haijulikani ni jinsi gani shambulio hilo - ambalo linaonekana kuwa la kisasa sana - lilitokea, ingawa Hezbollah imewalaumu wapinzani wake Israel. Maafisa wa Israel hadi sasa wamekataa kutoa maoni yao.
Haya ndio tunayoyajua hadi sasa.
Ilifanyika lini na wapi?
Milipuko hiyo ilianza katika mji mkuu wa Lebanon Beirut na maeneo mengine kadhaa ya nchi mnamo 15:45 saa za ndani (13:45 BST) siku ya Jumanne.
Mashahidi waliripoti kuona moshi ukitoka kwenye mifuko ya watu, kabla ya kuona milipuko midogo iliyosikika kama fataki na milio ya risasi.
Katika video moja, picha za CCTV zilionekana kuonesha mlipuko kwenye mfuko wa suruali ya mwanaume alipokuwa amesimama kwenye eneo la duka.
Milipuko iliendelea kwa takribani saa moja baada ya milipuko ya awali, shirika la habari la Reuters liliripoti.
Muda mfupi baadaye, watu wengi walianza kuwasili katika hospitali kote Lebanon, na mashahidi wakiripoti matukio ya machafuko makubwa.
Vifaa vya mawasiliano vililipukaje?
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Wachambuzi wamekuwa wakieleza kushtushwa na ukubwa wa shambulio la Jumanne, wakisema Hezbollah inajivunia hatua zake za usalama.
Baadhi walisema udukuzi ulisababisha betri za vifaa kupata joto kupita kiasi, na kusababisha vifaa kulipuka. Kitendo kama hicho hakitawahi kutokea.
Lakini wataalamu wengi wanasema hilo haliwezekani, kwa kuwa picha za milipuko hiyo haziendani na joto la hali ya juu la betri.
Wachambuzi wengine wanasema badala yake kwamba aina fulani ya shambulio la mnyororo wa usambazaji, ambalo lilihusisha kuchezewa kwa vifaa hivyo wakati wa utengenezaji wake au katika usafirishaji, lilikuwa na uwezekano zaidi.
Mashambulizi ya msururu ni wasiwasi unaoongezeka katika ulimwengu wa usalama wa mtandao huku matukio mengi ya hadhi ya juu hivi karibuni yakisababishwa na wadukuzi kupata bidhaa wakati zinatengenezwa.
Mtaalamu wa zamani wa silaha za Jeshi la Uingereza, ambaye hakutaka jina lake litajwe, aliiambia BBC kuwa vifaa hivyo vingeweza kuwa vimefungwa kati ya gramu 10 hadi 20 kila moja ya vilipuzi vya kiwango cha juu cha kijeshi, vilivyofichwa ndani ya kifaa bandia cha kielektroniki.
Hii, alisema mtaalam, ingekuwa na silaha na ishara, kitu kinachoitwa ujumbe wa maandishi wa alphanumeric.

Chanzo cha picha, Getty Images
Ni nini kinachofahamika kuhusu waathiriwa?
Chanzo karibu na Hezbollah kiliiambia AFP kwamba wawili kati ya waliouawa walikuwa wana wa wabunge wawili wa Hezbollah. Pia walisema binti wa mwanachama wa Hezbollah aliuawa.
Miongoni mwa waliojeruhiwa ni balozi wa Iran nchini Lebanon, Mojtaba Amani. Ripoti katika vyombo vya habari vya Iran zilisema majeraha yake yalikuwa madogo.
Mkuu wa Hezbollah Hassan Nasrallah hakujeruhiwa katika milipuko hiyo, shirika la habari la Reuters liliripoti likinukuu chanzo.
Waziri wa Afya ya Umma wa Lebanon Firass Abiad alisema uharibifu wa mikono na uso ndio unaochangia majeruhi wengi.
Akizungumza na kipindi cha Newshour cha BBC, alisema: “Majeraha mengi yanaonekana usoni na hasa machoni na pia baadhi ya viungo, iwe mikononi au vidoleni."
Aliongeza: "Idadi kubwa ya watu wanaofika kwenye vyumba vya dharura wamevaa kiraia, kwa hivyo ni ngumu sana kutambua ikiwa ni wa chombo fulani kama Hezbollah au wengine ...
"Lakini tunaona miongoni mwao watu ambao ni wazee au watu ambao ni wadogo sana, kama mtoto ambaye alikufa kwa bahati mbaya ... na kuna baadhi yao ambao ni wahudumu wa afya," Waziri alisema.
Nje ya Lebanon, watu 14 walijeruhiwa katika milipuko kama hiyo katika nchi jirani ya Syria, kulingana na taasisi ya wanaharakati yenye makao yake nchini Uingereza ya Syrian Observatory for Human Rights.
Ni nani aliyehusika?
Hadi sasa, hakuna aliyedai kuhusika, ingawa waziri mkuu wa Lebanon na Hezbollah wameilaumu Israel.
Waziri Mkuu Najib Mikati alisema milipuko hiyo inawakilisha "ukiukwaji mkubwa wa mamlaka ya Lebanon na uhalifu kwa viwango vyote".
Katika taarifa yake inayoishutumu Israel kwa kuhusika na mashambulizi hayo, Hezbollah ilisema inaishikilia nchi hiyo "kikamilifu kuwajibika kwa uvamizi huu wa uhalifu ambao pia ulilenga raia".
"Adui huyu msaliti na mhalifu hakika atapata adhabu yake ya haki kwa uchokozi huu wa dhambi, iwe anatarajia au la," iliongeza.
Maafisa wa Israel hawajazungumzia madai hayo, lakini wachambuzi wengi wanakubali kwamba inaonekana kuna uwezekano kuwa ndio waliohusika na shambulio hilo.
Prof Simon Mabon, Mkuu wa idara ya Uhusiano wa Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Lancaster, aliiambia BBC: "Tunafahamu kuwa Israel ina historia ya kutumia teknolojia kufuatilia lengo lake", lakini aliita ukubwa wa shambulio hili "haujawahi kutokea".
Lina Khatib, kutoka Chatham House yenye makao yake nchini Uingereza, alisema shambulio hilo linaonesha kuwa Israel "imejipenyeza" kwenye "mtandao wa mawasiliano" wa Hezbollah.

Chanzo cha picha, EPA
Kwa nini Hezbollah inatumia vifaa hivi vya mawasiliano?
Hezbollah imeegemea aina hii ya vifaa vidogo vya mawasiliano sana kama njia ya teknolojia ya chini ya mawasiliano ili kujaribu kukwepa kufuatiliwa na Israel.
Page ni kifaa cha mawasiliano ya simu kisichotumia waya ambacho hupokea na kuonesha jumbe za alphanumeric au sauti.
Simu za mkononi zimeachwa kwa muda mrefu kama hatari sana, kama mauaji ya Israeli dhidi ya mtengenezaji wa bomu wa Hamas Yahya Ayyash yalidhihirisha muda mrefu uliopita kama 1996, wakati simu yake ilipolipuka mkononi mwake.
Lakini mhudumu mmoja wa Hezbollah aliliambia shirika la habari la AP kwamba watengenezaji wa vifaa hivyo vilikuwa chapa mpya ambayo kundi hilo lilikuwa halijaitumia hapo awali.
Emily Harding, mchambuzi wa zamani wa CIA, alisema uvunjaji wa usalama ulikuwa wa aibu kubwa kwa Hezbollah.
"Ukiukaji wa kiwango hiki sio tu kuwa na madhara ya kimwili, lakini pia utawafanya watilie shaka vyombo vyao vyote vya usalama," aliiambia BBC.
"Ningetarajia kuwaona wakifanya uchunguzi wa kina wa ndani ambao utawavuruga kutokana na vita vinavyowezekana na Israel."
Je, mzozo wa Hezbollah na Israel utaongezeka?
Hezbollah inashirikiana na adui mkubwa wa Israel katika eneo hilo, Iran. Kundi hilo ni sehemu ya Mhimili wa Upinzani wa Tehran na limekuwa likipigana na Israel kwa miezi kadhaa, mara kwa mara zimekuwa zikirushiana roketi katika mpaka wa kaskazini wa Israel. Jamii nzima imehamishwa kutoka pande zote mbili.
Milipuko hiyo imekuja saa chache baada ya baraza la mawaziri la usalama la Israel kufanya kuwarejesha salama wakazi kaskazini mwa nchi hiyo kuwa lengo rasmi la vita.
Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu alimwambia afisa wa Marekani aliyezuru kuwa Israel "itafanya kile kinachohitajika kuhakikisha usalama wake".
Mapema Jumatatu, wakala wa usalama wa ndani wa Israel alisema kuwa umezuia jaribio la Hezbollah la kumuua afisa wa zamani.
Licha ya mvutano huo unaoendelea, wachunguzi wa mambo wanasema hadi sasa pande zote mbili zimelenga kuzuia uhasama bila kuvuka mipaka na kuingia katika vita kamili. Lakini kuna hofu kwamba hali hiyo inaweza kudorora, huku Hezbollah tayari ikitishia kujibu milipuko ya Jumanne.















