Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Chombo cha habari cha Hamas: Tunachojua kumhusu Abu Ubaida
- Author, Ethar Shalaby
- Nafasi, BBD News Arabic
Msemaji rasmi wa tawi la kijeshi la Hamas, Vikosi vya al-Qassam, amekuwa mmoja wa watu mashuhuri katika vita vya Israel na Gaza.
Anajulikana kama "Abu Ubaida", mara nyingi huonekana kwenye mitandao ya kijamii akisambaza ujumbe wa kikundi mtandaoni.
Jina lake la utani linamuashiria Abu Ubaida ibn al-Jarrah, kamanda wa kijeshi wa Kiislamu ambaye alikuwa mmoja wa maswahaba wa Mtume Muhammad.
Abu Ubaida alikua mtu mashuhuri baada ya kamanda wa al-Qassam, Mohammad Al-Deif, kutangaza kuanza kwa "Operesheni ya mafuriko ya Al-Aqsa" - jina lililotolewa na Hamas kwa mashambulio Hamas ya Jumamosi tarehe 7 Oktoba dhidi ya Israel yaliyoua watu 1200 kusini mwa nchi hiyo.
Kilemba(keffiyeh) nyekundu
Hakuna anayejua utambulisho kamili wa Abu Ubaida. Daima huonekana kwenye video huku uso wake ukifunikwa na keffiyeh Nyekundu (kilemba cha kitamaduni cha Wapalestina).
Anasimama kando ya maandishi yaliyonakiliwa kutoka wa Quran anapotangaza kinachoendelea katika operesheni za kijeshi za kundi hilo.
Abu Ubaida anashiriki hotuba zake kupitia chaneli yake ya Telegram, ambayo inasemekana kuzinduliwa mwaka wa 2020. Hana majukwaa mengine ya mitandao ya kijamii inayojulikana.
Hotuba zake za video husambazwa kwenye mitandao ya kijamii na kutangazwa kwenye vituo kadhaa vya habari.
Kulingana na gazeti la Al-Sharq Al-Awasat, gazeti maarufu la kila siku lenye makao yake mjini London, "Abu Ubaida alijulikana kwa mara ya kwanza mwaka 2002 kama mmoja wa maafisa wa nyanjani wa al-Qassam".
Gazeti hilo lilisema alizungumza na vyombo vya habari akiwa amefunika uso wake, akiiga mtindo wa aliyekuwa kiongozi wa Al-Qassam, Imad Aqel, ambaye Israel ilimfunga jela mwaka 1993.
Msemaji wa vikosi vya Al-Qassam
Mnamo 2006, Abu Ubaida aliteuliwa kuwa msemaji rasmi wa Brigedi za al-Qassam. Alinekana hadharani kwa mara ya kwanza tarehe 25 Juni 2006, wakati makundi yenye silaha, ikiwa ni pamoja na Hamas, yalipovamia kituo cha kijeshi cha Israel karibu na mpaka na Gaza.
Operesheni hiyo ilifanyika baada ya kusema kwamba kombora lilitua kwenye nyumba ya familia ya Huda Ghalia - tukio ambalo lilivutia hisia za kimataifa baada ya msichana wa miaka 10 kurekodiwa akikimbia huko akilia na kupiga mayowe kwenye ufuo wa Gaza, akisema "Baba, baba, baba", kisha akaanguka huku akilia kando ya mwili wake.
Wakati wa uvamizi huo, mwanajeshi wa Israel Gilad Shalit alikamatwa, wanajeshi wengine wawili waliuawa na wengine wawili, mbali na Shalit, walijeruhiwa.
Shalit aliachiliwa huru mwaka 2011, baada ya Israel na vuguvugu la Kiislamu la Hamas kukubaliana katika mapatano ambapo zaidi ya Wapalestina 1,000 waliachiliwa huru.
Wakati wa vita vya mwaka 2014 vya Israel na Gaza, Abu Ubaida alidai kukamatwa kwa mwanajeshi wa Israel Shaul Aaron katika hotuba ya televisheni, ingawa Israel ilisema kuwa amekufa.
Utambulisho wa kisiri
Kufichua utambulisho wa Abu Ubaida imekuwa ni shauku kwa wengi. Tarehe 25 Oktoba, msemaji wa jeshi la Israel Avichay Adraee aliweka mtandaoni video inayoonyesha picha ya mtu ambaye alidai kuwa Abu Ubaida.
Adraee alisema jina halisi la mtu huyo lilikuwa "Hudhaifa Samir Abdullah al-Kahlout". Hamas na al-Qassam hawakutoa kauli yoyote kuhusu madai hayo.
Gazeti la Israel la Yedioth Ahronot limeripoti kwamba Abu Ubaida alipokea Shahada ya Uzamili kutoka Kitivo cha Misingi ya Dini katika Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Gaza mwaka 2013.
Linasema aliandika tasnifu yenye kichwa: "Nchi Takatifu kati ya Uyahudi, Ukristo, na Uislamu." na anadai alikuwa anajiandaa kupata shahada ya uzamivu.
Kulingana na gazeti hilo hilo, asili ya Abu Ubaida ni kijiji cha Naliya mjini Gaza kilichukuliwa na Israel mwaka 1948. Lakini sasa, kulingana na ripoti, anaishi Jabaliya kaskazini mashariki mwa Gaza.
Gazeti la Israel linasema nyumba yake ilishambuliwa kwa bomu zaidi ya mara moja na Israel katika miaka ya 2008-2012 na tena katika operesheni ya sasa katika Ukanda wa Gaza.
BBC haijafanikiwa kuthibitisha ripoti hizo, zilizochapishwa katika vyombo vya habari vya pan-Arab na Israel.