Chelsea yatumia pauni milioni 95 kununua wachezaji sita

Chanzo cha picha, Getty Images
- Author, Emlyn Begley
- Nafasi, BBC
Chelsea imekuwa na shughuli nyingi katika soko la usajili, msimu huu wa joto, ikileta wachezaji watano wapya hadi sasa na mmoja yuko njiani.
Wamemsajili nani?
Tosin Adarabioyo

Chanzo cha picha, Getty Images
Beki wa kati Tosin Adarabioyo alijiunga na Chelsea kwa mkataba wa miaka minne baada ya mkataba wake na Fulham kumalizika.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 26, anaweza kuchezea England au Nigeria, amekuwa mmoja wa wachezaji muhimu wa Fulham lakini alikataa mkataba mpya na timu hiyo.
Beki mwenye urefu wa futi 6 na inchi 5 atavaa jezi namba nne - na ana matumaini ya kuchukua nafasi ya beki Thiago Silva.
"Chelsea ni klabu kubwa na huu ni wakati wangu," alisema mchezaji huyo aliyekulia katika akademi ya Manchester City.
Omari Kellyman

Chanzo cha picha, Getty Images
Chelsea imemsajili kiungo wa kati wa Aston Villa na England chini ya umri wa miaka 20 Omari Kellyman kwa thamani ya pauni milioni 19.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 18 alicheza mechi moja tu ya dakika 90 kwa Villa - na kucheza mechi nyingine tano akitokea benchi - baada ya uhamisho wa paunili 600,000 kutoka Derby mwaka 2022.
Kellyman, ambaye pia anaweza kucheza mbele, amesaini mkataba wa miaka sita na Chelsea.
"Natumai, nataweza kuwa mmoja wa wachezaji muhimu wa pembeni. Nataka kuwa mchezaji mkubwa wa klabu hii."
Marc Guiu

Chanzo cha picha, Getty Images
Chelsea imelipa pauni milioni 5 tu kumsajili mshambuliaji, Marc Guiu.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 18, ametokea Barcelona na kujiunga na Chelsea kwa kandarasi ya miaka mitano.
Alifunga mabao mawili katika mechi saba za kikosi cha kwanza cha Barca - ikiwa ni pamoja na bao la sekunde 23 katika mechi yake ya kwanza dhidi ya Athletic Bilbao.
"Ni furaha kubwa kusaini Chelsea. Tangu nikiwa mdogo, ilikuwa ndoto yangu kucheza Ligi Kuu ya Uingereza."
Kiernan Dewsbury-Hall

Chanzo cha picha, Getty Images
Chelsea imelipa pauni milioni 30 kumnunua kiungo wa Leicester City, Kiernan Dewsbury-Hall, mwenye umri wa 25, kwa mkataba wa miaka sita.
Aliingia katika akademi ya Foxes na kuichezea klabu hiyo mara 129, akifunga mabao 17 – na 12 kati ya hayo alifunga katika mechi za kusaka kupanda daraja kuingia Ligi Kuu ya Uingereza msimu uliopita.
Pia alifunga mabao 12 ya ligi msimu uliopita na alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mwaka wa klabu hiyo.
Kocha mpya wa Chelsea Enzo Maresca anamfahamu vyema tangu alipokuwa Leicester msimu uliopita.
“Nilizungumza na Enzo Maresca kuhusu kuongeza mabao zaidi kwenye mechi zangu na mbinu za kufanya hivyo na nimefanikiwa kufanya hivyo,” alisema Dewsbury-Hall.
Leicester hawakutaka kumpoteza, lakini walihitaji pesa ili kutimiza kanuni za kifedha za Ligi Kuu ya Uingereza.
Renato Veiga

Chanzo cha picha, Getty Images
Chelsea pia imemsajili mchezaji wa Basel, Renato Veiga kwa paumi milioni 12 kwa mkataba wa miaka saba.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 20 anaweza kucheza katika safu ya ulinzi ya kati, beki wa kushoto au kiungo. Alijiunga na Basel majira yaliyopita ya joto kwa pauni milioni 4 kutokea Sporting Lisbon, akiwa pia anatakiwa na Burnley.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ureno chini ya miaka 21, alikwenda kwa mkopo katika klabu ya Bundesliga, Augsburg mwaka 2023.
"Nina jiamini niwapo na mpira na ningejielezea kama mchezaji kamili kutokana na uhodari wangu," alisema.
Estevao Willian
Chelsea wamekubali dili la kumnunua winga wa Palmeiras, Estevao Willian kwa dau la awali la pauni milini 29 - atakapo timiza miaka 18.
Mbrazil huyo atatumia mwaka ujao na Palmerias kwani haruhusiwi kuhama nchi akiwa na umri wa miaka 17.
"Estevao ndiye mchezaji bora aliyeibuka katika soka la Brazil tangu Neymar. Unamtazama na unampenda," mkuu wa akademi ya Palmeiras, Joao Paulo Sampaio, aliambia BBC Sport.
Imetafsiriwa na Rashid Abdallah na kuhaririwa na Yusuf Jumah












