Matokeo ya uchaguzi Marekani 2020: Fahamu kile Trump anachoweza kujishughulisha nacho baada ya kuondoka Ikulu

Donald Trump ataendelea kusalia madarakani hadi Januari 20, pale atakapokabidhi madaraka kwa anayemrithi na kuingia kwenye orodha ya waliokuwa marais. Sasa je kipi kinafuata baada ya kufunga ukurasa wa urais?

Jimmy Carter alianza kuegemea kwenye shughuli za misaada ya kibinadamu huku George W Bush akigeukia masuala ya upakaji rangi. Lakini Trump hajawahi kuwa mwanasiasa anayeshikilia utamaduni wa waliomtangulia.

"Donald Trump ameenda kinyume na desturi nyingi za marais," amesema Tim Calkins, Profesa wa masuala ya biashara chuo kikuu cha Northwestern Kellogg.

"Hakuna dalili yoyote ya kutuwezesha kufikiria kuwa Donald Trump atachukua hatua kama ya marais waliotangulia."

Mengine yanayoweza kutokea ni yapi?

Anaweza kugombea tena urais.

Huenda isiwe mwisho wa azma ya kisiasa ya Bwana Trump - anaweza kuwania muhula wa pili wakati wowote.

Cleveland ndio rais pekee aliyeondoka Ikulu na kurejea miaka minne baadaye, alikuwa rais mwaka 1885 na kurejea tena mwaka 1893.

Katiba ya Marekani inaonesha kuwa "hakuna atakayeweza kuchaguliwa tena kwenye ofisi ya rais zaidi ya mara mbili", lakini hakuna kinachohitajika kwa mtu mwenye msimamo mkali.

Waliokuwa wafanyakazi wake wamesema kuwa Bwana Trump huenda akataka kufanya hivyo.

"Huenda akaingia kwenye orodha ya ambao wanawania urais 2024," aliyekuwa mkuu wa wafanyakazi, Mick Mulvaney, alisema hivyo hivi karibuni.

Bwana Trump bila shaka anapenda mikutano ya kampeni na alipata kura milioni 71.5 ambazo zinaonesha anaungwa mkono kisiasa na raia wengi tu wa Marekani.

Pia kumekuwa na uvumi kuwa huenda kijana mkubwa wa rais wa sasa Donald Trump Jr, akawa na nia ya kugombea nafasi hiyo ya juu zaidi.

Kurejea tena kwenye ulingo wa biashara

Kabla ya kuingia kwenye siasa, Bwana Trump alikuwa mfanyabiashara maarufu wa majengo, nyota katika kipindi cha televisheni na pia alikuwa nembo au balozi wa biashara zake.

Huenda akaamua kuanzia pale alipoachia miaka minne iliyopita na kujitosa kwenye ulimwengu wa kibiashara.

Trump ana mali katika maeneo ya Mumbai, Istanbul na Ufilipino - bila kusahau Washington DC na uwanja wa gofu nchini Marekani, Uingereza, Dubai na Indonesia.

Ikiwa atachagua kufuata njia hiyo, basi kufikia Januari, Donald Trump atakuwa na shughuli nyingi za kujishughulisha nazo.

Kuwa tajiri wa vyombo vya habari

Rais Trump sio mgeni kwenye televisheni hasa baada ya kuwa maarufu kwenye kipindi cha moja kw moja.

Hivyobasi kumekuwa na uvumi kuwa huenda akataka kujihusisha na vyombo vya habari ama kwa kuzindua kituo chake cha runinga au kushirikiana na kituo kimoja.

"Bila shaka atakuwa na wafuasi wa kutosha," anasema Henry Schafer, makamu rais wa kampuni ya Q Scores.

Marupurupu ya kustaafu kama rais

Pia Trump atalipwa pesa za uzeeni kama aliyekuwa rais wa marekani - na marupurupu mengine mengi tu baada ya kuondoka madarakani.

Pia waliokuwa marais hupewa ulinzi katika kipindi chote cha maisha yao, wanapata mafao ya kiafya na mengineo.

Na Bwana Trump ambaye sasa hivi ana umri wa miaka 74 huenda akaamua kustaafu.

Anaweza pia kutumia muda wake wa ziada kupumzika katika uwanja wa gofu uliopo Florida.

Lakini Profesa Calkins anasema kwa mtazamo wake haoni kama ataamua kutumia muda mwingi kufanya mambo yake kimya kimya kwasababu kwa kipindi kirefu amekuwa akiangaziwa na vyombo vya habari.

"Sifa za Donald Trump kama yeye sioni zikibadilika na nafkiria tutaendelea kuona Trump kama nembo yak wake mwenyewe aliyoitengeneza tayari duniani," anasema.

Oktoba, Bwana Trump alisema kuwa ikiwa atashindwa kwenye uchaguzi atahisi vibaya mno kiasi cha hata "huenda akaondoka nchini humo".