Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Kesi ya nyaraka za siri iliyomkabili Trump yafutiliwa mbali na jaji wa Florida

Jaji wa Florida ametupilia mbali kesi ya nyaraka za siri za Wizara ya Sheria dhidi ya Donald Trump katika ushindi mkubwa wa rais huyo wa zamani siku chache tu baada ya mtu mwenye silaha kujaribu kumuua.

Muhtasari

  • Trump asema "ataleta nchi pamoja" baada ya kunusurika jaribio la mauaji
  • Mshukiwa mkuu wa mauaji ya wanawake jijini Nairobi akamatwa
  • Watu kadhaa wahofiwa kufariki baada ya bomu lililotegwa kulipuka Mogadishu
  • Polisi wanamsaka meya anayetuhumiwa kuwa jasusi wa China
  • Waziri wa Uingereza ahimiza kusitishwa kwa mapigano mara moja wakati wa ziara yake Israel
  • Argentina yaishinda Colombia na kutwaa taji la 16 la Copa America
  • England yavunjwa moyo baada ya kushindwa na Uhispania katika fainali ya Euro 2024
  • Mshawishi wa Instagram afungwa jela kwa ulanguzi na utumwa
  • IDF yasema kamanda mkuu wa Hamas aliuawa katika shambulio la anga la Israel
  • 'Tunahitaji wamarekani kutuliza joto la kisiasa', Biden asema

Moja kwa moja

Asha Juma

  1. Ruto ashutumu shirika la Kimarekani kwa kufadhili maandamano ya vurugu nchini Kenya

    Rais William Ruto ameushutumu wakfu wa Ford, ambao ni wakfu wa binafsi wa Marekani, kwa kufadhili ghasia wakati wa maandamano dhidi ya serikali.

    Akiongea mjini Nakuru siku ya Jumatatu, Ruto alidai kuwa Wakfu huo ulikodi watu kusababisha ghasia wakati wa maandamano yaliyosababisha uharibifu wa mali na uporaji wa biashara.

    "Nataka niulize watu wa Ford Foundation watuambie hio pesa wanatoa, wanatoa ifanye fujo ndio wapate faida gani?"

    "Tutawaita na tutawaambia kama hawapendi demokrasia nchini Kenya, kama watafadhili vurugu na machafuko tutawaita na tutawaambia wao pia kujirekebisha au waondoke." Alisema Rais Ruto.

    Alisema kuwa serikali yake haitamwacha yeyote anayewasajili vijana wa Kenya ili kusababisha ghasia barabarani wakati wa maandamano ya amani.

  2. Habari za hivi punde, Kesi ya nyaraka za siri iliyomkabili Trump yaondolewa na jaji wa Florida

    Jaji wa Florida ametupilia mbali kesi ya nyaraka za siri za Wizara ya Sheria dhidi ya Donald Trump katika ushindi mkubwa wa rais huyo wa zamani siku chache tu baada ya mtu mwenye silaha kujaribu kumuua.

    Jaji Aileen Cannon amekubali ombi la Trump la kutupilia mbali kesi hiyo kwa msingi kwamba uteuzi wa Wizara ya Sheria wa Mwendesha Mashtaka Maalum Jack Smith unakiuka Kipengele cha Uteuzi cha Katiba ya Marekani.

    Trump alikana mashtaka kadhaa katika kesi hiyo ya kushughulikia nyaraka za siri, ikiwa ni pamoja na kuhifadhi kwa makusudi taarifa za ulinzi wa taifa.

    Makumi ya makablasha yaliyoainishwa yalipatikana katika hoteli ya Trump ya Mar-a-Lago huko Florida, pamoja na kwenye bafu na chumba cha kuhifadhia, baada ya Trump kuondoka Ikulu ya White House mnamo 2021.

    "Mahakama ina hakika kwamba mashtaka ya Wakili Maalum Smith kuhusu hatua hii yanakiuka misingi miwili ya kimuundo ya mpango wetu wa kikatiba, jukumu la Congress katika uteuzi wa maafisa wa kikatiba, na jukumu la Congress katika kuidhinisha matumizi kwa mujibu wa sheria,"

  3. Kwa nini Trump aliulizia viatu vyake baada ya shambulio la risasi?

    Wacha tuangalie maelezo mengine tuliyobaini kutoka kwenye mahojiano ya Trump na New York Post.

    Katika moja ya video za jaribio la mauaji, Trump alisikika akisema: "Nahitaji viatu vyangu." Aliielezea New York Post kwamba maafisa usalama waliomrukia baada ya kupigwa risasi walitumia nguvu sana hadi viatu vyake kudondoka.

    "Na viatu vyangu vilikuwa vimenibana," aliambia gazeti hilo. Trump pia aliwapongeza wafanyakazi wa usalama kwa hatua zao na akawasifu kwa kumpiga risasi mtu aliyejihami kwa silaha.

    Unaweza kusoma;

  4. 'Nilipaswa kuwa nimekufa' asema Trump

    Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump amesema "ilikuwa awe amekufa" baada ya jaribio la kumuua Jumamosi usiku katika mkutano wa hadhara huko Pennsylvania.

    Katika mojawapo ya mahojiano yake ya kwanza tangu kisa hicho, Bw Trump aliambia vyombo vya habari vya kihafidhina vya Marekani kuwa alihisi kuwa ameokolewa "kwa bahati na Mungu". "Jambo la kushangaza zaidi ni kwamba sikugeuza tu [kichwa changu] lakini kugeuka kwa wakati ufaao na kwa kiwango kinachofaa," alisema, akiongeza kuwa risasi ilivyogusa sikio lake ingeweza kumuua kwa urahisi.

    "Ninapaswa kufa, sitakiwi kuwa hapa," alisema. Mtazamaji mmoja aliuawa katika shambulio hilo, huku watu wengine wawili wakijeruhiwa vibaya.

    Mshambuliaji, ambaye pia alikufa, ametajwa kwa jina Thomas Matthew Crooks.

  5. Trump asema "ataleta nchi pamoja" baada ya kunusurika jaribio la mauaji

    Rais wa zamani Donald Trump ametoa moja ya mahojiano yake ya kwanza tangu jaribio la kumuua Jumamosi usiku, akisema ameandika upya kabisa hotuba yake ya mkutano ili kuzingatia ujumbe wa "umoja" badala ya kumkosoa Joe Biden.

    "Hotuba ambayo ningetoa Alhamisi itakuwa ya kufurahisha," aliiambia Washington Examiner.

    "Kama haya hayangetokea, hii ingekuwa mojawapo ya hotuba za kushangaza," alisema pia, akiongeza kuwa ingelenga zaidi sera za Rais Biden.

    "Kusema kweli, itakuwa hotuba tofauti kabisa sasa. Ni nafasi ya kuleta nchi pamoja. Nilipewa nafasi hiyo.”

    Trump pia alisema kwamba "ukweli" wa kile kilichotokea Jumamosi " ndio unaanza tu," na akaelezea wakati alipotazama umati wa watu baada ya kugundua kuwa alikuwa amepigwa risasi.

    “Nguvu iliotoka kwa watu waliokuwepo wakati huo, walisimama tu; ni vigumu kuelezea jinsi nilivyohisi, lakini nilijua ulimwengu ulikuwa unatazama. Nilijua kuwa historia ingehukumu hili, na nilijua lazima niwafahamishe tuko sawa,” alimwambia Mkaguzi.

    Donald Trump amesema "alitakiwa kuwa amefariki", akitaja jaribio la mauaji kuwa "kitu kibaya" kukipitia.

    "Sitakiwi kuwa hapa, ninapaswa kuwa nimekufa," Trump alisema, akizungumza na New York Post alipokuwa akielekea Milwaukee kwa Kongamano la Kitaifa la Republican.

    Trump alivaa bandeji nyeupe iliyofunika sikio lake la kulia lakini wasaidizi wake hawakuruhusu picha zozote kupigwa, lilisema Post.

    "Daktari katika hospitali alisema hajawahi kuona kitu kama hiki, alikitaja kuwa muujiza," Trump aliongeza.

    Soma zaidi:

  6. 'Mshukiwa mkuu' akamatwa baada ya miili kupatikana jalalani Kenya

    Polisi nchini Kenya wamemkamata mwanamume ambaye wamemtaja kama "muuaji wa watu wengi" anayeshukiwa kuhusika na mauaji ya kutisha ya wanawake tisa ambao miili yao iliyokatwakatwa ilipatikana kwenye machimbo ambayo yanatumika kama jalala.

    Polisi wanasema Jomaisi Khalisia, 33, alikiri kuwaua wanawake 42 tangu 2022, akiwemo mkewe .

    Mshukiwa alikamatwa katika baa mapema Jumatatu asubuhi alipokuwa akitazama fainali ya Euro.

    Kumekuwa na mshtuko na ghadhabu nchini Kenya tangu maiti ya kwanza ya miili kupatikana siku ya Ijumaa katika mji mkuu, Nairobi.

    "[Ali]kiri kuwarubuni, kuwaua na kutupa miili ya wanawake 42 katika eneo hilo la taka .Wote waliuawa kati ya 2022 na hivi majuzi Alhamisi," alisema Mohamed Amin, mkuu idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).

    Alisema wamepata ushahidi muhimu katika nyumba ya mtuhumiwa, zikiwemo simu 10, tarakilishi bebe , panga, vitambulisho na mavazi ya kike.

  7. Somalia: Bomu lililotegwa garini laua watu 9 waliokuwa wakitazama fainali ya Euro

    Watu kadhaa wameuawa baada ya bomu lililotegwa ndani ya gari kulipuka nje ya mkahawa maarufu uliokuwa umejaa mashabiki wa soka katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.

    Bomu hilo lililipuka Jumapili usiku saa 22:28 kwa saa za huko wakati walinzi wa Top Coffee walikuwa wakitazama fainali ya kandanda ya Euro 2024 kati ya Uhispania na England.

    Polisi wamesema takriban watu watano waliuawa katika mlipuko huo na wengine 20 kujeruhiwa. Vyanzo vya usalama baadaye vililiambia shirika la habari la AFP kwamba idadi ya waliofariki imeongezeka hadi tisa.

    Kundi la wanajihadi la al-Shabab lilisema lilitekeleza shambulio hilo.

    "Tulisikia mlipuko mkubwa na wa kutisha katika kipindi cha kwanza cha mchezo tuliokuwa tukiutazama. Kila mtu alilazimika kufikiria jinsi ya kujiokoa," mmoja wa walionusurika, Mohamed Muse, aliiambia BBC.

    "Niliona watu katika hatari, watu waliojeruhiwa wakipiga kelele kuomba msaada, na wengine kuchanganyikiwa – ilikuwa hali ya kutisha," aliongeza.

    Mlipuko huo pia uliharibu magari kadhaa na kuharibu majengo pia.

    Al-Shabab, kundi ambalo ni sehemu ya al-Qaeda, linaripotiwa kusema lililenga mahali ambapo maafisa wa usalama na wafanyikazi wa serikali hukutana usiku.

    Eneo hilo liko karibu na Villa Somalia, makazi rasmi ya rais.

    Kundi hilo la kijihadi limefanya mashambulizi mengi ya mabomu katika mji huo na maeneo mengine ya Somalia katika kipindi cha miaka 17 iliyopita.

    Hata hivyo, kumekuwa na utulivu katika miezi ya hivi karibuni huku kukiwa na kuendelea kwa mashambulizi ya vikosi vya usalama vya Somalia dhidi ya kundi hilo ambalo bado linadhibiti maeneo makubwa ya nchi.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Polisi wanamsaka meya anayetuhumiwa kuwa jasusi wa China

    Meya wa mji mdogo nchini Ufilipino ambaye ameshutumiwa kuwa jasusi wa China, ameenda mafichoni, maafisa walisema.

    Polisi hawakuweza kutekeleza kibali cha kukamatwa kwa Alice Guo mwishoni mwa juma kwa kuwa hakupatikana katika anwani zake zote zinazojulikana.

    Vituo vya kulaghai watu vilifichuliwa katika mji wa Bi Guo wa Bamban mnamo mwezi Machi, vikiwa vimefichwa kwenye kasino za mtandaoni zinazohudumia Wachina wa bara.

    Simulizi yake imekuwa kama mchezo wa kuigiza wa televisheni, kwa vile pia aliwahi kuhojiwa kuhusu kuwa mzazi nchini China na tuhuma kwamba alikuwa akifanya kazi kama jasusi wa Beijing.

    Bunge la Seneti liliamuru kukamatwa kwa Bi Guo na baadhi ya watu wa familia yake Ijumaa iliyopita baada ya kupuuza mara mbili wito wa kufika kwenye vikao vya kesi inayomkabili.

    "Jitokeze. Kujificha hakuwezi kufuta ukweli," Seneta Risa Hontiveros, anayeongoza uchunguzi wa bunge kuhusu Bi Guo, alisema kwenye taarifa.

    Bi Guo amekana kutenda makosa hayo. Anadai baba yake Mchina na mama yake Mfilipino walimlea kwenye shamba lao la nguruwe.

    Soma zaidi:

  9. Waziri wa Uingereza ahimiza kusitishwa kwa mapigano mara moja wakati wa ziara ya Israel

    Waziri wa Uingereza David Lammy ametoa wito wa kusitishwa kwa mapigano mara moja huko Gaza wakati wa ziara yake ya kwanza nchini Israel na maeneo ya Palestina kama waziri wa mambo ya nje.

    "Niko hapa kushinikiza kusitishwa kwa mapigano," alisema. "Kupoteza maisha katika miezi michache iliyopita... ni ya kutisha. Inabidi ikome."

    Bw Lammy pia alihimiza kuachiliwa kwa mateka wote wanaoshikiliwa Gaza na kuongezeka kwa misaada katika eneo hilo.

    Waziri huyo mpya aliyechaguliwa alifanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu na Waziri Mkuu wa Mamlaka ya Palestina Mohammad Mustafa siku ya Jumapili.

    Baadaye anatarajiwa kukutana na Rais wa Israel Isaac Herzog na familia za baadhi ya mateka wenye uhusiano na Uingereza.

    "Ni muhimu kwamba, wakati tuko kwenye vita, vita hivyo viendeshwe kwa mujibu wa sheria za kimataifa za kibinadamu," Bw Lammy alisema.

    "Bila shaka nitakuwa nikisisitiza viongozi wa Israel juu ya suala hilo katika siku zijazo."

    Waziri huyo wa mambo ya nje pia alionyesha kufadhaika kutokana na ukosefu wa malori ya misaada ya Uingereza inayoingia Gaza "baada ya miezi na miezi ya kuomba" hilo kufanyika, akirejelea malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa mashirika ya kutoa misaada kuhusu kuzuiwa au kucheleweshwa kwa ukaguzi tata uliowekwa na jeshi la Israel.

    Alisema hali ya kibinadamu huko Gaza ilikuwa "ya kutisha" na kwamba Uingereza itakuwa ikitoa pauni milioni 5.5 za ziada kwa shirika la matibabu la UK-Med kufadhili kazi yake katika eneo hilo.

    Chama cha Labour hivi majuzi kimekabiliwa na msukosuko kutoka kwa baadhi ya wapiga kura Waislamu kuhusu jibu lake kwa mzozo huo, ambao wengi wanauona kuwa hautoshi kuikosoa Israel.

    Serikali mpya sasa inakabiliwa na maamuzi juu ya masuala kadhaa muhimu, ikiwa ni pamoja na kuweka kikomo au kusimamisha uuzaji wa silaha kwa Israel kutokana na raia kupoteza maisha.

    Soma zaidi:

  10. Argentina yaishinda Colombia na kutwaa taji la 16 la Copa America

    Argentina iliishinda Colombia 1-0 na kunyakua taji la kuvunja rekodi la 16 la Copa America lakini mchezo huo ulitatizwa kwa kucheleweshwa kwa dakika 80 kwa sababu ya matatizo nje ya uwanja huko Miami.

    Lautaro Martinez alifunga bao katika kipindi cha pili cha muda wa nyongeza kutoka kwa krosi ya Giovani lo Celso .

    Nahodha Lionel Messi alitokwa machozi alipolazimika kubadilishwa katikati ya kipindi cha pili baada ya kuumia alipokuwa akiutafuta mpira - lakini alikuwa akisherehekea michuano mikuu ya tatu mfululizo ya nchi yake wakati wa kipenga cha mwisho.

    Mchezo wa kwanza ulicheleweshwa kwa sababu ya fujo nje ya Uwanja wa Hard Rock.

    Waandalizi walisema mashabiki wasio na tiketi walijaribu kuingia uwanjani, na kuwaacha mashabiki wengine wakisubiri kwa saa nyingi kwenye joto la Miami ili milango ifunguliwe.

    Mashabiki na maafisa wa polisi na usalama walikabiliana na kuwakamata kwa watu kadhaa. Wafuasi kadhaa walihitaji matibabu kutoka kwa wahudumu wa afya.

  11. England yavunjwa moyo baada ya kushindwa na Uhispania katika fainali ya Euro 2024

    Harakati za England kumaliza maumivu na kukatishwa tamaa kwa miaka 58 ziliishia pabaya walipofungwa na Uhispania kwenye fainali ya Euro 2024 kwenye uwanja wa Olympiastadion mjini Berlin baada ya kufungwa mabao 2-1.

    Kikosi cha Gareth Southgate kilizamishwa na bao la dakika za mwisho la Mikel Oyarzabal na kuwaacha wakiwa wamevunjika moyo tena katika fainali ya pili mfululizo ya Ubingwa wa Ulaya .

    Mawinga chipukizi wa Uhispania walishirikiana kuwapa bao la kuongoza dakika mbili baada ya kipindi cha mapumziko huku pasi ya Lamine Yamal ikifungua nafasi kwa Nico Williams kumshinda kipa wa Uingereza Jordan Pickford na kumaliza kwa kasi ndogo.

    Nahodha wa England Harry Kane hakuwa katika hali nzuri kimchezo akatolewa baada ya saa moja na Cole Palmer - akachukua Kobbie Mainoo - ambaye aliibua matumaini ya kurejea tena kwa bao la mguu wa kushoto baada ya dakika 73.

    Ilikuwa ni Uhispania, hata hivyo, walionyakua ushindi huo dakika nne kabla ya mchezo kumalizika Oyarzabal alipofunga krosi ya Marc Cucurella na kuwaacha England katika hali nyingine ya kungoja taji kuu

    Unaweza pia kusoma

  12. Mshawishi wa Instagram afungwa jela kwa ulanguzi na utumwa

    Wakati wasichana wawili wa Kibrazili waliporipotiwa kutoweka mnamo Septemba 2022, familia zao na Shirika la Upelelezi la Marekani – FBI, walianzisha msako mkali kote Marekani ili kuwapata. Walichojua ni kwamba walikuwa wakiishi na mshawishi wa Instagram Kat Torres.

    Torres sasa amehukumiwa kifungo cha miaka minane jela kwa ulanguzi wa binadamu na utumwa wa mmoja wa wanawake hao.

    BBC pia imeambiwa kuwa mashtaka yamewasilishwa dhidi yake kuhusiana na mwanamke wa pili.

    Je, mwanamitindo huyo wa zamani ambaye aliwekwa kwenye jalada la magazeti ya kimataifa alianzaje kuwahadaa wafuasi wake na kuwarubuni katika ulanguzi wa kingono?

    "Alikuwa kama mwenye kunipa tumaini," anasema Ana, akielezea hisia zake baada ya kuona ukurasa wa Instagram wa Torres mnamo 2017.

    Ana hakuwa mmoja wa wanawake waliopotea waliolengwa katika msako wa FBI - lakini yeye pia alikuwa mwathirika wa kulazimishwa na Torres na angekuwa muhimu kwa uokoaji wao.

    Anasema alivutiwa na historia ya Torres kutoka kuwa mtu masikini wa Kibrazili hadi mwanamitindo wa kimataifa, akishirikiana na waigizaji mashuhuri wa Hollywood.

    "Alionekana kama alikuwa ameshinda ghasia katika utoto wake, unyanyasaji, matukio yote ya kutisha," Ana aliambia Uchunguzi wa BBC Eye na BBC News Brasil.

    Ana mwenyewe alikuwa katika mazingira magumu. Anasema aliteseka utotoni kwa vurugu, alihamia Marekani peke yake kutoka kusini mwa Brazili, na awali alikuwa katika uhusiano wa unyanyasaji.

    Torres alikuwa amechapisha hivi majuzi wasifu wake uitwao A Voz [The Voice], ambamo alidai kuwa angeweza kutabiri kutokana na nguvu zake za kiroho, na alikuwa amehojiwa kwenye vyombo vya habari maarufu vya Brazili.

    “Alikuwa kwenye jalada la magazeti. Alionekana na watu maarufu kama vile Leonardo DiCaprio. Kila kitu nilichoona kilionekana kuwa cha kuaminika, "anasema.

    Ana anasema alivutiwa hasa na mtazamo wa Torres wa kiroho.

    Kitu ambacho Ana hakujua ni kwamba simulizi ya kutia moyo aliyosimulia Torres ilitokana na nusu ukweli na uwongo.

    Soma zaidi:

  13. IDF yasema kamanda mkuu wa Hamas aliuawa katika shambulio la anga la Israel

    Jeshi la Israel linasema kamanda mkuu wa Hamas Rafa Salama aliuawa katika shambulio la anga huko Gaza siku ya Jumamosi. Hata hivyo, Hamas haijathibitisha ripoti hiyo.

    Wizara ya afya inayosimamiwa na Hamas huko Gaza ilisema kuwa shambulio la Israel lilishambulia kambi ya watu waliokimbia makazi yao katika eneo lililotengwa huko Khan Younis, na kuua Wapalestina 90 huku wengine 289 wakijeruhi.

    Israel imesema shambulizi hilo lilikuwa linalenga viongozi wakuu wa Hamas, lakini Hamas inasema madai hayo ni ya "uongo" na yanasaidia "kuhalalisha" shambulio hilo.

    Walioshuhudia walisema waliona takriban "ndege kubwa za kivita tano zikishambulia kwa mabomu katikati ya eneo la Al Mawasi, magharibi mwa Khan Younis".

    Wengi wa waliojeruhiwa walipelekwa katika hospitali ya karibu ya Nasser.

    Hata hivyo, kulingana na maafisa na madaktari, kituo hicho "hakina uwezo tena wa kufanya kazi" kwani madaktari "wamezidiwa na idadi kubwa ya majeruhi".

    Akizungumza na kipindi cha Newshour kwenye BBC World Service, Dkt Mohammed Abu Rayya, ambaye yuko katika hospitali inayoshughulikia matokeo ya shambulio hilo, alisema wengi wa waliojeruhiwa walikuwa wakiuguza majeraha ya vipande vya mabomu.

    Aliongeza ni kama kuwa "kuzimu", kwani wengi wa waathiriwa walikuwa raia, haswa wanawake na watoto.

    Jeshi la Israel lilisema Salama, kamanda wa Brigedi ya Khan Younis, alikuwa mmoja wa "wapangaji" wa shambulio la Oktoba 7 na mshirika wa karibu wa Mohammed Deif, kamanda mkuu wa tawi la kijeshi la Hamas.

    Msemaji wa jeshi alisema kifo cha Salama "kinazuia kwa kiasi kikubwa uwezo wa kijeshi wa Hamas".

    Haijulikani ikiwa Deif aliuawa. Jeshi la Israel lilisema pia alilengwa katika shambulio hilo.

    Deif amekuwa miongoni mwa watu wanaosakwa sana na Israel kwa miongo kadhaa na analaumiwa na mamlaka ya Israel kwa mauaji ya raia na wanajeshi wengi.

    Soma zaidi:

  14. Wamarekani wanafaa kupunguza joto la kisiasa-Biden

    Biden ametoa hotuba kwa taifa baada ya aliyekuwa rais wa nchi hiyo Donald Trump kuponea chupu chupu jaribio la mauaji.

    Biden alianza hotuba yake kwa kuwaambia "Wamarekani wenzake" juu ya "haja ya kutuliza joto la siasa zetu".

    "Milio ya risasi jana kwenye mkutano wa hadhara wa Donald Trump huko Pennsylvania inatutaka sote kurudi nyuma," alisema.

    Biden anamwita mtu aliyefariki kwa kupigwa risasi 'shujaa'

    Katika hotuba yake, Joe Biden kwa mara nyingine tena anatoa rambirambi zake kwa familia ya Corey Compatore, mtu aliyeuawa kwa kupigwa risasi Jumamosi.

    "Corey alikuwa mume, baba, wazima moto wa kujitolea na shujaa, akiilinda familia yake kutokana na risasi hizo," anasema, akiongeza kuwa umma unapaswa kumuweka yeye na familia yake katika maombi yao.

    'Hakuna mahali nchini Marekani kwa vurugu ' - Biden

    Rais Biden amekariri kwamba "vurugu kamwe sio jibu" katika siasa za Marekani, akiorodhesha msururu wa matukio ikiwa ni pamoja na jaribio la mauaji ya Rais wa zamani Donald Trump, shambulio la Januari 6 bungeni na shambulio la spika wa zamani Nancy Pelosi.

    "Hakuna mahali nchini Marekani kwa aina hii ya vurugu - kwa vurugu yoyote ile milele," alisema.

    "Siasa katika nchi hii zimepamba moto, ni wakati wa kuzituliza."

    Soma zaidi:

  15. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 15/7/2024