Wanajeshi wa Marekani wameripotiwa kupotea wakati wa mazoezi ya kijeshi nchini Morocco

Chanzo cha picha, Universal Images Group via Getty Images
Maafisa wawili wa kijeshi wa Marekani wamepotea wakati wa mazoezi ya kijeshi nchini Morocco, kwa mujibu wa kamandi ya kijeshi ya Marekani, US African Command (AFRICOM).
Wanajeshi hao walikuwa wanashiriki katika mazoezi ya kila mwaka ya kijeshi yanayojulikana kama African Lion 2026, ambayo hushirikisha majeshi ya Marekani, washirika wa NATO na mataifa mbalimbali ya Afrika.
Africom ilisema waliripotiwa kupotea Jumamosi karibu na eneo la mafunzo la Cap Draa, lililoko karibu na mji wa Tan Tan.
Operesheni ya utafutaji na uokoaji inaendelea, ikihusisha rasilimali za ardhini, anga na baharini kutoka Marekani, Morocco na nchi nyingine washirika. Mamlaka zinasema lengo kuu ni kuwapata wanajeshi hao na kusaidia familia zao.
Kwa mujibu wa maafisa wa Marekani waliozungumza na vyombo vya habari, tukio hilo linaaminika kuwa ajali na si shambulio la kigaidi au utekaji nyara, huku uchunguzi ukiendelea kubaini kilichotokea.
Zoezi hilo, linalohusisha wanajeshi 5,000 kutoka zaidi ya nchi 40 pamoja na washirika zaidi ya 30 linatarajiwa kuendelea mpaka tarehe 8 mwezi Mei.






