Mashambulizi ya Urusi yaua watu 10, Zelensky akisema Ukraine imelenga meli za mafuta

Maafisa katika maeneo matano nchini humo waliripoti vifo huku Moscow ikiendelea kulenga miji ya Ukraine kwa mashambulizi ya anga ya mara kwa mara.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Lizzy Masinga

  1. Wanajeshi wa Marekani wameripotiwa kupotea wakati wa mazoezi ya kijeshi nchini Morocco

    Mazingira ya Tan Tan, Morocco, ambayo yako karibu na mahali ambapo Wamarekani walipotea

    Chanzo cha picha, Universal Images Group via Getty Images

    Maelezo ya picha, Mazingira ya Tan Tan, Morocco, ambayo yako karibu na mahali ambapo Wamarekani walipotea.

    Maafisa wawili wa kijeshi wa Marekani wamepotea wakati wa mazoezi ya kijeshi nchini Morocco, kwa mujibu wa kamandi ya kijeshi ya Marekani, US African Command (AFRICOM).

    Wanajeshi hao walikuwa wanashiriki katika mazoezi ya kila mwaka ya kijeshi yanayojulikana kama African Lion 2026, ambayo hushirikisha majeshi ya Marekani, washirika wa NATO na mataifa mbalimbali ya Afrika.

    Africom ilisema waliripotiwa kupotea Jumamosi karibu na eneo la mafunzo la Cap Draa, lililoko karibu na mji wa Tan Tan.

    Operesheni ya utafutaji na uokoaji inaendelea, ikihusisha rasilimali za ardhini, anga na baharini kutoka Marekani, Morocco na nchi nyingine washirika. Mamlaka zinasema lengo kuu ni kuwapata wanajeshi hao na kusaidia familia zao.

    Kwa mujibu wa maafisa wa Marekani waliozungumza na vyombo vya habari, tukio hilo linaaminika kuwa ajali na si shambulio la kigaidi au utekaji nyara, huku uchunguzi ukiendelea kubaini kilichotokea.

    Zoezi hilo, linalohusisha wanajeshi 5,000 kutoka zaidi ya nchi 40 pamoja na washirika zaidi ya 30 linatarajiwa kuendelea mpaka tarehe 8 mwezi Mei.

  2. Mashambulizi ya Urusi yaua watu 10, Zelensky akisema Ukraine imelenga meli za mafuta

    Miji ya Ukraine imekuwa ikikumbwa mara kwa mara na mashambulizi ya anga kutoka Urusi

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Miji ya Ukraine imekuwa ikikumbwa mara kwa mara na mashambulizi ya anga kutoka Urusi

    Mashambulizi ya ndege zisizo na rubani na makombora ya Urusi nchini Ukraine yamesababisha vifo vya watu 10 na kujeruhi takribani 76 katika siku moja iliyopita, kulingana na ripoti.

    Maafisa katika maeneo matano nchini humo waliripoti vifo huku Moscow ikiendelea kulenga miji ya Ukraine kwa mashambulizi ya anga ya mara kwa mara.

    Wakati huo huo, Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, alisema kituo cha kuhifadhi mafuta kaskazini-magharibi mwa Urusi kimeharibiwa vibaya, huku meli mbili za mafuta za Urusi zikishambuliwa karibu na bandari ya Bahari Nyeusi ya Novorossiysk.

    Hakuna maelezo kamili kuhusu uharibifu wa meli hizo, lakini Zelensky alisema zilikuwa sehemu ya “kikosi kivuli” cha Urusi kinachotumiwa kukwepa vikwazo vya nchi za Magharibi.

    Jeshi la Ukraine limesema Urusi lilirusha kombora la balistiki na karibu droni 270, lakini nyingi zilidunguliwa.

    Watu watatu waliuawa katika matukio tofauti katika eneo la Kherson, kulingana na gavana, huku wawili wakifa katika kila moja ya maeneo ya Odesa, Donetsk na Zaporizhzhia, na mtu mmoja katika eneo la Sumy.

    Wakati huo huo, Urusi ilisema Ukraine ilirusha ndege zisizo na rubani takribani 334, huku eneo la kaskazini-magharibi la Leningrad likilengwa sana.

    Vituo vya usafirishaji wa mafuta katika eneo hilo na maeneo mengine vimeshambuliwa na Ukraine katika wiki za hivi karibuni, ikiwa ni sehemu ya mashambulizi yaliyofanikiwa dhidi ya miundombinu ya mafuta ya Urusi, ambayo Kyiv inasema yamepunguza mauzo ya nje yenye thamani ya mabilioni ya dola.

  3. Nigeria yamuita balozi wa Afrika Kusini kufuatia mashambulizi dhidi ya raia wake

    Raia wa Afrika Kusini wanawashutumu wageni kwa kuishi nchini humo kinyume cha sheria

    Chanzo cha picha, KIM LUDBROOK/EPA/Shutterstock

    Maelezo ya picha, Raia wa Afrika Kusini wanawashutumu wageni kwa kuishi nchini humo kinyume cha sheria.

    Nigeria imemuita kaimu balozi wa Afrika Kusini kufuatia mlolongo wa mashambulizi ya hivi karibuni dhidi ya raia wa kigeni nchini humo.

    Nigeria imesema itawasilisha rasmi “wasiwasi wake mkubwa” katika mkutano utakaofanyika Jumatatu kuhusu matukio hayo, ikionya kuwa yanaweza kuathiri uhusiano uliopo kati ya nchi hizo mbili, kulingana na taarifa ya wizara ya mambo ya nje.

    Mkutano huo utazingatia maandamano ya hivi karibuni yaliyofanywa na makundi yanayopinga wahamiaji, pamoja na “matukio yaliyothibitishwa ya unyanyasaji dhidi ya raia wa Nigeria na mashambulizi dhidi ya biashara zao.”

    Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya ndani, takribani Wanigeria wawili na Waethiopia wanne wameuawa katika wiki za hivi karibuni, huku pia kukiwa na mashambulizi dhidi ya raia wa nchi nyingine za Afrika.

    Kama nchi iliyoendelea zaidi kiviwanda barani Afrika, Afrika Kusini kwa muda mrefu imekuwa kivutio kwa watu kutoka mataifa mengine ya bara hilo wanaotafuta ajira.

    Rais wa nchi hiyo, Cyril Ramaphosa, amelaani mashambulizi hayo lakini pia amewatahadharisha raia wa kigeni kuheshimu sheria za nchi.

    Katika hotuba yake wiki iliyopita, ikiadhimisha uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia mwaka 1994, alikumbusha Waafrika Kusini msaada waliopata kutoka nchi nyingine za Afrika katika mapambano dhidi ya mfumo wa kibaguzi.

    Hata hivyo, baadhi ya raia wa nchi hiyo wanawashutumu wageni kwa kuishi nchini humo kinyume cha sheria, kuchukua ajira za wenyeji, na kuwa na kujihusisha na uhalifu, hasa biashara ya dawa za kulevya.

    Unaweza kusoma;

  4. Wasiwasi waongezeka kuhusu kuzorota kwa afya ya mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel akiwa kifungoni Iran

    Narges Mohammadi alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa kazi yake ya kutetea haki za binadamu nchini Iran na kupinga ukandamizaji wa wanawake.

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Narges Mohammadi alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa kazi yake ya kutetea haki za binadamu nchini Iran na kupinga ukandamizaji wa wanawake.

    Ndugu wa mwanaharakati wa haki za binadamu wa Iran aliyefungwa jela, Narges Mohammadi, pamoja na Kamati ya Tuzo ya Amani ya Nobel, wametoa wito ahamishiwe katika vituo vya afya vinavyofaa kufuatia kuzorota kwa kasi kwa hali yake ya afya.

    Siku ya Ijumaa, familia yake ilisema mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 54 alipelekwa kutoka gereza lililoko kaskazini-magharibi mwa Iran hadi hospitali ya eneo hilo, wakisema hatua hiyo ilikuwa ya “dakika za mwisho” ambayo huenda imechelewa.

    Kaka yake, anayeishi Norway, aliiambia BBC Jumamosi: “Shinikizo la damu lake limeshuka sana, na hawajaweza kulidhibiti.”

    Narges Mohammadi alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel mwaka 2023. Alikamatwa mwezi Desemba kwa ukosoaji wake dhidi ya mamlaka.

    Mwezi uliopita, kaka yake Hamidreza Mohammadi alisema alipatikana akiwa amepoteza fahamu na wafungwa wenzake katika Gereza la Zanjan kaskazini-magharibi mwa Iran, baada ya kushukiwa kupata mshtuko wa moyo.

    Aliongeza kuwa maafisa wa gereza walikataa kumhamishia hospitalini licha ya historia yake ya matatizo ya moyo, mapafu na shinikizo la damu.

    Siku ya Ijumaa, Taasisi ya Narges Mohammadi, inayoendeshwa na familia yake, ilisema amehamishiwa hospitali katika jimbo la Zanjan “kufuatia kuzorota kwa afya yake.”

    Taarifa hiyo iliongeza kuwa hatua hiyo ilikuja “baada ya siku 140 za kuzuiliwa kiholela na kunyimwa mara kwa mara huduma maalum za afya.”

  5. Ashtakiwa kwa mauaji na unyanyasaji wa kingono dhidi ya mtoto wa miaka mitano

    Lewis

    Chanzo cha picha, Reuters

    Mwanaume mmoja ameshtakiwa kwa mauaji na makosa mawili ya unyanyasaji wa kingono kufuatia kifo cha msichana wa miaka mitano nchini Australia.

    Mwili wa msichana huyo, anayejulikana kama Kumanjayi Little Baby, jina la bandia alilopewa na familia yake kwa sababu za kitamaduni baada ya kifo chake ulipatikana Alhamisi baada ya siku kadhaa za msako mkubwa wa polisi.

    Jefferson Lewis, mwenye umri wa miaka 47, alishtakiwa kwa mauaji yake Jumamosi usiku na anatarajiwa kufikishwa mahakamani Jumanne katika mji wa Darwin.

    Watu watano wamekamatwa kufuatia ghasia za vurugu zilizotokea Alice Springs baada ya kifo cha mtoto huyo.

    Kamishna wa Polisi wa Northern Territory, Martin Dole, alitangaza mashtaka dhidi ya Lewis Jumapili asubuhi.

    “Bado hili ni tukio linaloumiza sana, na mawazo yetu yako pamoja na familia ya Kumanjayi, wapendwa wake na jamii pana iliyoathiriwa kwa kiasi kikubwa na matukio haya,” alisema.

    Dole aliomba jamii iheshimu mchakato wa kisheria.

    Inaripotiwa kuwa Jefferson Lewis alishambuliwa katika mji wa Alice Springs kabla ya kukamatwa Alhamisi.

    Unaweza kusoma;

  6. Meli ya mafuta yatekwa nyara karibu na pwani ya Yemen na kuelekea Somalia

    Ghuba ya Aden

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maharamia wa Kisomali wameiteka nyara meli ya kubeba mafuta karibu na pwani ya Yemen, kulingana na maafisa kadhaa wa usalama wa Somalia waliozungumza na BBC.

    Walinzi pwani wa Yemen awali walisema kuwa meli hiyo, MT Eureka, ilikuwa imetekwa nyara na ilikuwa inaelekea Somalia. Vyanzo vilisema ilitekwa na maharamia katika Ghuba ya Aden, karibu na bandari ya Qana.

    Maharamia hao waliondoka katika eneo la pwani la mbali karibu na mji wa Qandala, uliopo kwenye Ghuba ya Aden, kulingana na maafisa watatu wa usalama kutoka eneo la Puntland waliozungumza na BBC.

    Tukio hili ni la pili la kutekwa kwa meli ya mafuta katika eneo hilo ndani ya kipindi cha siku 10, kufuatia kutekwa kwa meli ya Honor 25 na maharamia wa Kisomali tarehe 22 Aprili.

    Meli ya Honor 25 ilikuwa imebeba mapipa 18,500 ya mafuta yaliyokuwa yakielekea Mogadishu.

    MT Eureka ilikuwa inapeperusha bendera ya taifa la Afrika Magharibi la Togo kabla ya kutekwa, na ilivamiwa na watu wenye silaha saa 5:00 asubuhi kwa saa za huko (03:00 BST), afisa wa usalama aliiambia BBC.

    Kwa sasa meli hiyo inasafiri katika Ghuba ya Aden kati ya Yemen na Somalia.

    Katika tukio jingine tofauti, United Kingdom Maritime Trade Operations (UKMTO) iliripoti Ijumaa kuwa “watu wenye silaha” waliokuwa kwenye boti ndogo walikaribia meli ya mizigo karibu na Al-Mukala, Yemen.

    Unaweza kusoma;

  7. Ujerumani yasema kuondolewa kwa wanajeshi wa Marekani ni jambo lililotabirika,Trump aonya kuhusu kupunguza zaidi vikosi vyake

    Marekani kwa sasa ina zaidi ya wanajeshi 36,000 nchini Ujerumani

    Chanzo cha picha, EPA-EFE/REX/Shutterstock

    Waziri wa ulinzi wa Ujerumani, Boris Pistorius, amesema kuwa uamuzi wa Marekani kuondoa wanajeshi 5,000 kutoka nchini humo ulikuwa “unatarajiwa”, huku muungano wa kijeshi wa NATO ukisema unatafuta ufafanuzi zaidi kutoka Washington.

    Akizungumza na shirika la habari la DPA, Pistorius alisisitiza kuwa “uwepo wa wanajeshi wa Marekani barani Ulaya, na hasa nchini Ujerumani, ni kwa manufaa yetu na pia ni kwa manufaa ya Marekani”.

    Wakati huo huo, msemaji wa NATO, Allison Hart, alisema kuwa muungano huo “unafanya kazi na Marekani kupata maelezo ya uamuzi huo”.

    Alipoulizwa kuhusu kuondolewa kwa wanajeshi hao, Rais wa Marekani Donald Trump alisema: “Tutapunguza kwa kiwango kikubwa, na tutapunguza zaidi ya hao 5,000.” Hata hivyo, hakutoa maelezo zaidi.

    Hatua hiyo ya Washington imekuja baada ya Trump kumkosoa Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz kwa kauli yake kwamba Marekani “imedhalilishwa” na wajumbe wa Iran katika vita vinavyoendelea.

    Kwa sasa, uwepo wa kijeshi wa Marekani nchini Ujerumani unazidi wanajeshi 36,000 walioko kazini, ukiwa ndio mkubwa zaidi barani Ulaya, ukilinganishwa na takribani wanajeshi 12,000 walioko Italia na 10,000 walioko Uingereza.

  8. Habari za asubuhi, karibu katika taarifa zetu za leo