Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Ruto apendekeza ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta Tanga
Rais wa Kenya William Ruto ametoa wito wa ushirikiano wa kikanda na ushirikiano wa kiuchumi, akizitaka Kenya na Tanzania kuimarisha uhusiano wa uwekezaji na kuepuka tofauti zinazogawanya majirani hao wawili.
Akihutubia bunge la Tanzania mjini Dodoma siku ya Jumanne , Ruto amesema kwamba binafsi anaunga mkono juhudi za kuvutia uwekezaji Tanga, ikiwa ni pamoja na pendekezo la ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta, akisema kuwa mradi huo utanufaisha ukanda wa Afrika Mashariki.
"Binafsi, ninasaidia kuleta uwekezaji Tanga," alisema.
"Kama mngekuwa watu wazuri, mngekuwa mnasema asante kwetu Wakenya, tufanye kazi kama Afrika Mashariki.
Kenya iliwahi kumiliki kiwanda cha kusafisha mafuta cha Mombasa, ambacho awali kilijulikana kama Kenya Petroleum Refineries Ltd (KPRL) huko Changamwe, kabla ya kilisitisha shughuli zake za kusafisha mafuta ghafi mnamo Septemba 2013 kutokana na uzembe, gharama kubwa za uendeshaji na ufilisi wa kiufundi.
Baadaye kituo hicho kilichukuliwa na kumilikiwa na Kampuni ya Kenya Pipeline (KPC) ili kutumika kama ghala la bidhaa za petroli zilizosafishwa kutoka nje.
Lakini akizungumza mjini Dodoma, Rais Ruto alisisitiza kwamba maendeleo ya kiuchumi katika nchi moja hayapaswi kuangaliwa kwa kutengwa na majirani zake, akibainisha kuwa Kenya na Tanzania zina mustakabali mmoja.
"Kinachofaa kwa Tanzania ni kizuri kwa Kenya na kinyume chake. Naomba tuwe watu wamoja. Tusiruhusu mazungumzo ya jana yatutenganishe," alisema.
Ruto alisisitiza zaidi kuwa Kenya na Tanzania hazipaswi kuonana kama washindani au wapinzani, bali kama washirika katika maendeleo.
"Tuna hatima ya pamoja," alisema. "Nimeeleza kuwa Wakenya sio adui zenu na kinyume chake.
Umuhimu wa Tanga kumiliki kituo hicho
Kulingana na Ruto, ukaribu wa Tanga na Mombasa, takriban kilomita 190, unatoa faida za vifaa ambazo zinaweza kusaidia kuunganisha miundombinu ya mafuta na usambazaji bora wa bidhaa zilizosafishwa kote kanda.
Ruto amesema mpango huo unaenda zaidi ya usafishaji wa mafuta, akionyesha nia pana ya kuanzisha uwezo wa kikanda wa usindikaji wa madini.
"Tunapojadili Tanga kama kitovu cha kituo hicho cha mafuta ni lazima pia tufikirie kukiweka kituo cha kusafisha madini, akiongezea kwamba sio vyema kwa sisi kuuza malighafi nje ya nchi, kama mkoa ni lazima tuepuke kwa makusudi kusafirisha thamani, ajira na fursa nje ya nchi, badala yake tuzihifadhi na kuzitumia ndani ya nchi, huo ndio mustakabali wa maendeleo yetu," alisema.
Uhusiano wenye mvutano
Uhusiano baina ya Kenya na Tanzania kihistoria umekuwa mchanganyiko wa ushirikiano wa karibu na mivutano ya mara kwa mara, ambayo mara nyingi huelezewa kama "mashindano ya ndugu".
Huku zikishiriki uhusiano wa karibu wa kihistoria, kiutamaduni na kiuchumi, mataifa hayo mawili yamepitia tofauti za kiitikadi—ubepari dhidi ya ujamaa katika miaka ya 1960-70—na migogoro ya kibiashara iliyopelekea Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kuvunjika mwaka 1977, kabla ya kurekebisha uhusiano mwaka 1983.
Mahusiano ya nchi hizo mbili yaliona uhasama, na vikwazo vya mara kwa mara visivyo vya ushuru, kama vile marufuku ya kuuza nje na migogoro ya biashara ya bidhaa kama vile vifaranga na mifugo, ambayo ilizuia ushirikiano wa kiuchumi.
Licha ya kuwa washirika wakuu wa kibiashara, uhusiano huo umekuwa na mizozo ya mara kwa mara badala ya ushirikiano thabiti.