Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Israel yashambulia 'ikijiandaa kwa uwezekano wa kuingia' Lebanon - Mkuu wa jeshi

Mashambulizi ya hivi punde zaidi ya Israel dhidi ya Lebanon ni maandalizi ya uwezekano wa kuingia kwa wanajeshi, mkuu wa jeshi anasema.

Muhtasari

  • Takribani watu 51 wameuawa kwa mashambulizi ya Israel - Wizara ya afya ya Lebanon
  • Hezbollah ina uwezekano wa kuwa na silaha nyingi
  • Mashambulizi ya Israel dhidi ya Hezbollah: Tunachojua kufikia sasa
  • Marekani yazitaka Israel, Lebanon kuepuka vita
  • Kiongozi mkuu wa Iran asema 'Hezbollah ni washindi'
  • Shambulio la Tel Aviv laonesha Hezbollah bado ni tishio
  • Watu 10 wauawa kwa shambulio la Israel nchini Lebanon
  • Sudan imerekodi vifo vingi zaidi vya akina mama duniani- MSF
  • Israel yazuia kombora la Kwanza la Hezbollah lililorushwa Tel Aviv
  • China yalifanyia majaribio kombora la masafa marefu kwa mara ya kwanza baada ya miongo kadhaa
  • Kesi ya 11 dhidi ya Sean 'Diddy' Combs yawasilishwa akiwa bado gerezani
  • Trump aonywa na huduma za usalama Marekani juu ya vitisho vya mauaji ya Iran - kambi yake ya kampeni
  • Starmer awaambia Waingereza waondoke Lebanon mara moja
  • UN yasema wafanyakazi wao ni miongoni mwa waliouawa katika mashambulizi ya anga ya Israel
  • Ryan Routh ashtakiwa kwa jaribio la kumuua Trump
  • Aina mpya ya ‘Papa zimwi’ yagunduliwa katika maji ya New Zealand
  • Mashambulizi ya Israel nchini Lebanon yanasababisha 'mauaji ya watu wengi' waziri wa afya asema

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Israel yashambulia 'ikijiandaa kwa uwezekano wa kuingia' Lebanon - Mkuu wa jeshi

    Mashambulizi ya hivi punde zaidi ya Israel dhidi ya Lebanon ni maandalizi ya uwezekano wa kuingia kwa wanajeshi, mkuu wa jeshi anasema.

    "Unasikia ndege zikiruka juu; tumekuwa tukishambulia siku nzima. Hii ni kuandaa mazingira ya kuingia kwako na kuendelea kuiadhibu Hezbollah," Herzi Halevi aliwaambia wanajeshi.

    "Leo, Hezbollah ilipanua safu yake ya mashambulizi, na baadaye leo, watapata jibu kali sana. Jiandaeni. "Leo, tutaendelea, hatuachi; tunaendelea kuwagonga na kuwapiga kila mahali.

    Lengo liko wazi sana, kuwarudisha salama wakazi wa kaskazini."

    Anaongeza kuwa ili "kufanikisha hilo", jeshi "linatayarisha mchakato wa ujanja, ambayo ina maana kwamba buti zako za kijeshi, buti zako za uendeshaji, zitaingia kwenye eneo la adui, kuingia katika vijiji ambavyo Hezbollah imetayarisha kama vituo vikubwa vya kijeshi".

  2. Takribani watu 51 wameuawa kwa mashambulizi ya Israel - Wizara ya afya ya Lebanon

    Takriban watu 51 waliuawa na zaidi ya 220 walijeruhiwa katika mashambulizi ya Israel huko Lebanon siku ya Jumatano, waziri wa afya wa Lebanon anasema.

    Nalo jeshi la Israel linasema kuwa shabaha 280 za Hezbollah zilishambuliwa.

    Katika taarifa yake ya hivi punde, Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) linasema kuwa ndege zake za kivita zimeshambulia takribani maeneo 280 ya Hezbollah nchini Lebanon siku ya Jumatano.

    Inasema shabaha hizo ni pamoja na majukwaa ya uzinduzi ambapo mashambulizi yalifanyika kaskazini mwa Israel asubuhi, pamoja na maghala ya silaha na miundombinu mingine ya kijeshi.

    Miongoni mwa maeneo yaliyoshambuliwa Jumatano ni shabaha 60 zinazotumiwa na Hezbollah, IDF ilisema katika ripoti ya awali.

  3. Hezbollah ina uwezekano wa kuwa na silaha nyingi,

    Kombora lililorushwa na Hezbollah kuelekea Tel Aviv liliripotiwa kuwa ni aina ya Qadr-1 iliyotengenezwa na Iran, kombora la masafa ya kati ambalo linaweza kubeba kichwa cha vita cha kati ya kilo 700 na kilo 1,000.

    Lingeweza kuharibu mengi ya majengo, kama yasingezuiwa katikati ya Israeli na moja ya mifumo mingi ya ya ulinzi wa anga ya nchi hiyo, na katika tukio hili ni mfumo kuitwa "David's Sling" [uliotumika].

    Hezbollah ina silaha kati ya 100,000 na 150,000, ndege zisizo na rubani na makombora.

    Hadi 10,000 kati ya silaha hizo zinaaminika kuwa ni makombora ya masafa ya kati, yanayoongozwa kwa usahihi, kama vile Fateh-110, ambayo yanaweza kufika Tel Aviv na maeneo mengine yenye idadi kubwa ya watu nchini Israel. (Jerusalem inachukuliwa kuwa shabaha inayolengwa kwa kiwango cha chini kwa sababu ya idadi kubwa ya Wapalestina.)

    Mwezi uliopita, Hezbollah ilitoa video ikijigamba kwa silaha zake kubwa za chini ya ardhi za makombora hayo, na kutishia kuzitumia kuishambulia Israel iwapo vita vitazuka.

    "Operesheni ya Kaskazini ya Israel", iliyozinduliwa wiki hii, inalenga kuharibu silaha nyingi iwezekanavyo, ikiwa ni pamoja na maeneo ambayo Israeli inasema makombora yamefichwa katika nyumba za kibinafsi na karakana.

    Lakini mtandao wa Hezbollah wa mahandaki na mapango, uliojengwa katika mwamba mgumu wa kusini mwa Lebanon, ni mkubwa.

    Licha ya mashambulizi yote ya anga, kuna uwezekano mkubwa wa kuwa na uwezo wa kufyatua makombora mengi katika miji ya Israel, lakini uongozi wake pia unafahamu kuwa kulipiza kisasi itakuwa ni jambo baya kwa Lebanon.

  4. Mashambulizi ya Israel dhidi ya Hezbollah: Tunachojua kufikia sasa

    Takriban watu 15 waliuawa katika wimbi la mashambulizi makubwa ya anga ya Israel katika maeneo ya kusini na katikati mwa Lebanon.

    Ikiwa unajiunga nasi tu, haya ndiyo mambo mengine unayohitaji kujua:

    • Makumi ya watu walijeruhiwa, kulingana na wizara ya afya ya Lebanon, ambayo inasema mashambulizi hayo yalipiga miji ya katikati mwa Lebanon, mbali na mpaka wake na Israeli.
    • Hapo awali, Israel ilisema kuwa ilinasa kombora la balistiki lililorushwa na Hezbollah kuelekea Tel Aviv - roketi ya kwanza kama hiyo kulenga mji mkubwa wa nchi hiyo.
    • Kundi la Shia lenye ushawishi mkubwa linasema kuwa limerusha "dazeni ya makombora" kaskazini mwa Israel.
    • Wazima moto katika eneo hilo walisambaza picha zinazoonyesha ukubwa wa uharibifu wa majengo katika eneo la Safed, ambapo maafisa wanasema hakuna majeruhi walioripotiwa.
    • Maelfu ya watu nchini Lebanon wanaendelea na safari, wakielekea kaskazini kuepuka mashambulizi ya Israel kusini.
    • Jeshi la Israel linasema kuwa limeanzisha mashambulizi dhidi ya maeneo 60 ya Hezbollah kote Lebanon.
  5. Marekani yazitaka Israel, Lebanon kuepuka vita

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken amejitokeza hivi karibuni kwenye Kituo cha Habari cha CBS kuzungumzia kuhusu kuongezeka kwa mvutano nchini Lebanon kufuatia mashambulizi ya Israel.

    Alisema njia bora ya watu kurejea makwao kusini mwa Lebanon na kaskazini mwa Israel sio vita bali kupitia "diplomasia". "Tunalenga hivi sasa katika kuhakikisha kuwa tunaweza kuepuka vita kamili," Blinken alisema.

    Blinken pia aliulizwa kuhusu mazungumzo yanayoendelea ya kusitisha mapigano kati ya Hamas na Israel na kusema kuwa wakati kuna makubaliano, Hamas haijashiriki mazungumzo katika wiki za hivi karibuni.

    "Bado inahitaji maamuzi magumu kwa upande wa Israel, lakini ni njia bora ya kukomesha kile kinachotokea Gaza, kuwatoa mateka," alisema.

    "Lakini pia, kama ulivyosema, itasaidia kaskazini. Itatoa njia kwa Hezbollah kujiondoa na kuruhusu diplomasia kufanya kazi."

  6. Kiongozi mkuu wa Iran asema 'Hezbollah ni washindi'

    "Hezbollah ni washindi," kiongozi mkuu wa Iran alichapisha kwenye akaunti yake rasmi ya X asubuhi ya leo, majibu ya kwanza kutoka kwa Ayatollah Ali Khamenei kuhusu mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon na Hezbollah.

    Hatua hiyo Inakuja huku kukiwa na uvumi kuhusu hadhi ya Iran katika kuunga mkono Hezbollah, chama chenye ushawishi mkubwa cha Waislamu wa madhehebu ya Shia na kundi lenye silaha ambalo limepata uungwaji mkono mkubwa kutoka kwa Iran, kifedha na kijeshi, kwa miaka mingi, hasa inapoonekana Tehran inajaribu kujitenga na nchi za Magharibi na kufikia makubaliano katika mazungumzo ya nyuklia.

    Akizungumza mjini New York siku ya Jumatatu, Rais wa Iran Masoud Pezeshkian alisema kuwa Iran haitafuti vita pana zaidi katika Mashariki ya Kati na kwamba mzozo huo hautakuwa na washindi.

    Na katika mahojiano na shirika la habari la Reuters, mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la uangalizi wa nyuklia, Rafael Grossi alisema kuwa amehisi nia kubwa ya maafisa wa Iran kushirikiana na shirika hilo kwa njia ya maana zaidi baada ya mazungumzo mjini New York, na kwamba anatarajia kusafiri hadi Tehran mwezi Oktoba.

    Haya yote yanazua maswali kuhusu msimamo wa Iran, ikiwa mashambulizi ya Israel dhidi ya Hezbollah yataongezeka na Lebanon kuingia katika vita kamili.

    Unaweza kusoma:

  7. Shambulio la Tel Aviv laonesha Hezbollah bado ni tishio

    Shambulio la leo la Hezbollah, mara ya kwanza kundi hilo lililenga Tel Aviv kwa kombora, linaweza kuwa ujumbe kwa Israeli: wanaweza kuwa wamedhoofika lakini wanasalia kuwa tishio.

    Kundi hilo limekumbwa na wimbi la mashambulizi ambalo halijawahi kushuhudiwa ambalo liliharibu sana uwezo wake wa kufanya kazi, lakini halijazuia uwezo wake wa kupigana.

    Wik iliyopita, shambulio dhidi ya vifaa vya mawasiliano na simu za upepo zilipunguza mawasiliano yao. Kisha, shambulio la anga kwenye ngome yake ya Dahieh, kusini mwa Beirut, ambalo kimsingi lilimaliza safu ya kamandi ya kitengo chake kikuu cha mapigano, Kikosi cha Radwan.

    Na siku ya Jumatatu, kampeni kali na iliyoenea ya anga ikilenga maeneo ya kufyatua roketi na maeneo ya kuhifadhi silaha.

    Mashambulizi hayo ya anga yamesababisha vifo vya takribani watu 500, wakiwemo raia wengi, waziri wa afya wa Lebanon anasema.

    Ilikuwa siku mbaya zaidi nchini Lebanon tangu kumalizika kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe, mnamo 1990.

    Hezbollah imesalia na msimamo mkali, ikiapa kuendelea na mashambulizi yake, huku kukiwa na uvumi kwamba mkakati wa Israel unaweza kujumuisha uvamizi wa ardhini kusini mwa Lebanon, kuunda eneo la amani, kuharibu miundombinu yake na kuwasukuma wapiganaji mbali na mpaka.

    Wakati huo huo, maelfu bado wako kwenye harakati, wakielekea kaskazini kutafuta usalama.

    Unaweza kusoma;

  8. Watu 10 wauawa kwa shambulio la Israel nchini Lebanon

    Wizara ya afya ya Lebanon imesema watu sita wameuawa baada ya mashambulizi ya Israel nchini Lebanon.

    Watu wanne waliuawa na wengine saba kujeruhiwa katika mji wa Joun, katikati mwa Lebanon, wizara hiyo inaongeza. Awali wizara hiyo ilisema watu sita wamefariki katika maeneo mengine mawili.

    Watu watatu waliuawa na kumi na watatu kujeruhiwa katika mji wa Ain Qana, kusini mwa Lebanon, na wengine watatu waliuawa na wengine tisa kujeruhiwa huko Al-Maaysra huko Keserwan, wizara hiyo inaongeza.

    Unaweza kusoma;

  9. Sudan imerekodi vifo vingi zaidi vya akina mama duniani- MSF

    Shirika la madaktari wasio na mipaka Médecins Sans Frontières - MSF, linaonya kuhusu mgogoro mkubwa wa kiafya katika eneo la Sudan Kusini mwa Darfur.

    Katika ripoti mpya, shirika hilo linasema vifo mia moja na kumi na nne (114) vya akina mama vilirekodiwa kati ya Januari na Agosti, huku maelfu ya watoto sasa wakikabiliwa na baa la njaa.

    Shirika hilo linasema wanawake wajawazito, akina mama na watoto wachanga wanakufa kutokana na masuala ya kiafya yanayoweza kuzuilika huku mfumo wa afya wa eneo hilo ukiporomoka.

    MSF inazitaka pande zinazozozana kukomesha unyanyasaji, hasa dhidi ya wanawake na watoto, na kuruhusu misaada ya kuokoa maisha kuwafikia watu waliokimbia makazi yao.

    Ripoti hiyo pia inatoa wito kwa Umoja wa Mataifa kuchukua hatua za haraka ili kuzuia kupoteza maisha zaidi.

    Hii inafuatia ripoti za vyombo vya habari vya ndani kuhusu mashambulizi ya anga ya jeshi la Sudan kwenye uwanja wa ndege huko Darfur Kusini siku ya Jumanne.

    Mashambulizi hayo yanadaiwa kulenga ndege za mizigo zinazopeleka vifaa kwa wanamgambo wa RSF ambao wamekuwa wakipambana na jeshi la Sudan tangu Aprili mwaka jana.

    Vita vya wenyewe kwa wenyewe hadi sasa vimeua maelfu ya watu na mamilioni ya wengine kuyahama makazi yao kote Sudan.

    Soma zaidi:

  10. Israel yazuia kombora la Kwanza la Hezbollah lililorushwa Tel Aviv

    Hezbollah imesema ilirusha kombora la balistiki kuelekea Tel Aviv saa kumi na mbili unusu asubuhi ya leo - ili kuunga mkono "mapigano ya kishujaa na ya heshima" ya Wapalestina katika Ukanda wa Gaza, na "kuilinda Lebanon na watu wake".

    Msemaji huyo alisema wamelenga makao makuu ya shirika la kijasusi la Israel Mossad, wakidai "linahusika na mauaji ya viongozi na kulipua vifaa vya mawasiliano vya umeme na vile visivyotumia umeme".

    Israel imelaumiwa kwa mashambulizi hayo yaliyoanzisha mapigano wiki iliyopita, lakini haijadai kuhusika nayo.

    Chombo cha habari cha Israel Haaretz Ynet kimesema hii ni mara ya kwanza kabisa kwa Hezbollah kulenga eneo la mji mkuu wa Tel Aviv.

    Jeshi la Israel linasema ving'ora vya mashambulizi ya anga vilisikika karibu na Tel Aviv na Israel ya kati, lakini kombora hilo lilinaswa na hakukuwa na ripoti za uharibifu au majeruhi.

    Imetoa ramani hii, ikisema haya yalikuwa maeneo ambayo ving'ora vililia:

    Israel yasema ni 'mara ya kwanza kabisa' kombora la Hezbollah kufika Tel Aviv - AFP

    Msemaji wa jeshi la Israel ameliambia shirika la habari la AFP kwamba "ni mara ya kwanza kwa kombora la Hezbollah kufika eneo la Tel Aviv",

    Kundi linalojihami la Lebanon linasema kuwa lilikuwa likilenga makao makuu ya kijasusi ya Israel, ambayo yako karibu na Tel Aviv.

    Tel Aviv na vitongoji vinavyozunguka jiji hilo ndio eneo la mijini lenye watu wengi zaidi nchini Israeli.

    Soma zaidi:

  11. China yalifanyia majaribio kombora la masafa marefu kwa mara ya kwanza baada ya miongo kadhaa

    China imesema kuwa ilifanikiwa kurusha kombora la balestiki linalovuka mabara (ICBM) lililobeba kichwa cha nyuklia kuelekea Bahari ya Pasifiki.

    Kombora la ICBM lilirushwa saa 08:44 kwa saa za eneo siku ya Jumatano na "lilianguka katika maeneo ya bahari yaliyotarajiwa", wizara ya ulinzi ya Beijing ilisema, na kuongeza kuwa majaribio hayo ni "kawaida" na sehemu ya "mafunzo yake ya kila mwaka".

    Aina ya kombora na njia yake ya kupaa haijafahamika, lakini vyombo vya habari vya serikali ya China vilisema Beijing "imeziarifu nchi zinazohusika mapema".

    Wachambuzi walisema maelezo ya Beijing ya jaribio hilo kama "kawaida" yanashangaza kwa sababu jaribio la mwisho kama hilo lilifanyika mnamo 1980.

    Majaribio ya silaha za nyuklia za China kwa kawaida hufanyika ndani ya nchi na hapo awali ilifanyia majaribio ya mamkombora ya kuvuka mabara ICBM magharibi kwenye Jangwa la Taklamakan katika eneo la Xinjiang.

    "Labda iwe kuna kitu sikielewi, nadhani hii ni mara ya kwanza kutokea - na kutangazwa namna hiyo – katika kipindi cha muda mrefu," Ankit Panda, mtaalamu wa silaha za nyuklia katika jopo la washauri la Carnegie Endowment for International Peace, aliandika kwenye mtandao wa X.

    Aliongeza kuwa maelezo ya Beijing ya jaribio hilo kama "kawaida" na "ya kila mwaka" yalikua yanashangaza, "ikizingatiwa kuwa kawaida hawafanyi kitu cha aina hii na pia sio cha kila mwaka".

    Wizara ya ulinzi ya Japan ilisema hakuna uharibifu wowote kwa meli zake kuanzia alasiri ya Jumatano.

    "Tutaendelea kukusanya na kuchambua habari kuhusu mienendo ya jeshi la China na tutachukua tahadhari zote zinazowezekana katika umakini na ufuatiliaji wetu," wizara ilisema, kulingana na shirika la utangazaji la Japan NHK.

    Pia unaweza kusoma zaidi:

  12. Kesi ya 11 dhidi ya Sean 'Diddy' Combs yawasilishwa akiwa bado gerezani

    Mwanamuziki wa Hip-hop Sean "Diddy" Combs kwa sasa yuko chini ya ulinzi wa serikali akisubiri kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za ulaghai na utumwa wa ngono.

    Kukamatwa kwake wiki iliyopita mjini New York kulitokea huku kukiwa na msururu wa mashtaka ya unyanyasaji wa kijinsia na unyanyasaji wa kimwili, dhidi yake na mengine yakianzia miaka ya 1990.

    Mlalamishi wa 11 na wa hivi punde kujitokeza ni Thalia Graves, anadai Combs na mlinzi wake walimpa dawa za kulevya , kumfunga na kumbaka mnamo 2001, na kurekodi tukio hilo.

    Rapa huyo mzaliwa wa Harlem amekana makosa ya jinai.

    Kesi ya jinai inahusu nini?

    Combs, 54, alikamatwa Jumatatu Septemba 16 katika hoteli ya New York kwa tuhuma za kula njama, kuendesha biashara ya utumwa wa ngono na uhalifu mwingine .

    Waendesha mashtaka wa serikali kuu wamemshutumu kwa "kuunda biashara ya uhalifu" ambapo "aliwanyanyasa, kutishia, na kulazimisha wanawake na wengine walio karibu naye kutimiza tamaa zake za kingono, kulinda sifa yake, na kuficha tabia yake".

    Walisema Combs ametumia dawa za kulevya, vurugu na nguvu ya hadhi yake "kuwavutia waathiriwa wa kike" katika vitendo vya ngono katika karamu zake zinazoitwa "Freak Offs".

    Pia walifichua walikuwa wamepata bunduki, risasi na chupa zaidi ya 1,000 za mafuta wakati wa uvamizi katika nyumba za Combs huko Miami na Los Angeles mnamo Machi.

    Soma zaidi:

  13. Trump aonywa na huduma za usalama Marekani juu ya vitisho vya mauaji ya Iran - kambi yake ya kampeni

    Donald Trump amefahamishwa na idara ya kijasusi ya Marekani kuhusu vitisho kutoka kwa Iran vya kutaka kumuua, kambi yake ya kampeni ilisema.

    Mgombea urais wa chama cha Republican alifahamishwa "kuhusu vitisho vya kweli na mahususi kutoka kwa Iran vya kutaka kumuua katika juhudi za kuyumbisha na kuzusha machafuko nchini Marekani", kambi yake ya kampeni ilisema katika taarifa.

    Haikufafanua madai hayo, na haikufahamika mara moja iwapo vitisho iliyokuwa inarejelea ni vipya au viliripotiwa awali.

    Serikali ya Iran haikujibu mara moja ombi la maoni yake, lakini Tehran hapo awali ilikanusha madai ya Marekani ya kuingilia masuala ya Marekani.

    "Maafisa wa ujasusi wamegundua kuwa mashambulizi haya yanayoendelea na yaliyoratibiwa yameongezeka katika miezi michache iliyopita," mkurugenzi wa mawasiliano wa kambi ya kampeni ya Trump, Steven Cheung alisema katika taarifa hiyo.

    "Maafisa wa utekelezaji wa sheria katika mashirika yote wanafanya kazi kuhakikisha Rais Trump analindwa na uchaguzi hauingiliwi," aliongeza.

    BBC imeenda kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Ujasusi wa Kitaifa nchini Marekani kwa maoni.

    Haya yanawadia baada ya Bw Trump kunusurika katika jaribio la mauaji mnamo Julai 13, alipojeruhiwa na mtu mwingine kuuawa kwa kupigwa risasi kwenye mkutano huko Pennsylvania.

    Nia ya tukio hilo bado haijabainika na bado linachunguzwa.

    Siku chache baadaye, vyombo vya habari vya Marekani viliripoti kwamba maafisa walipokea taarifa za kijasusi kuhusu njama zinazodaiwa kuwa za Iran dhidi ya rais huyo wa zamani.

    Maafisa wa Iran wakati huo walikanusha madai hayo na kusema ni ya "uovu", iliripoti mshirika wa BBC wa Marekani CBS habari.

    "Iwapo 'watamuua Rais Trump,' jambo ambalo linawezekana, ninatumai kuwa Marekani itaiangamiza Iran, kuifuta kabisa kwenye uso wa Dunia - Ikiwa hilo halitafanyika, Viongozi wa Marekani watachukuliwa kuwa waoga 'wasio na ujasiri'!" Bw Trump aliandika kwenye jukwaa lake la Truth Social platform wakati huo.

    Kisha tarehe 15 Septemba, Shirika Maalum la Usalama liliona bunduki ikipenya kwenye uzio katika Klabu ya Gofu ya Kimataifa ya Trump huko West Palm Beach.

    Ofisa wa shirika hilo alifyatua risasi Bw Trump alipokuwa akicheza gofu.

    Soma zaidi:

  14. Starmer awaambia Waingereza waondoke Lebanon mara moja

    Waziri Mkuu amewaambia raia wa Uingereza walioko Lebanon "sasa ni wakati wa kuondoka" baada ya mapigano kushika kasi kati ya Israel na Hezbollah, kundi linalomiliki silaha linaloungwa mkono na Iran ambalo linatawala nchi hiyo.

    Sir Keir Starmer alisema "tunaongeza mipango ya dharura, nadhani ungetarajia hilo kutokana na ongezeko la mapigano", na kuongeza kuwa raia wa Uingereza wanapaswa "kuondoka mara moja."

    Wizara ya Ulinzi inatuma wanajeshi 700 kwenda karibu na Cyprus kujiandaa kwa uwezekano wa kuwahamisha raia wa Uingereza kutoka Lebanon na serikali "inaendelea kutoa ushauri dhidi ya safari zote za kwenda Lebanon".

    Hali nchini humo, ambapo mashambulizi ya Israel yameripotiwa kuua zaidi ya watu 560 wiki hii, inaelezwa kuwa inazidi kuzorota "kwa kasi, na matokeo ni mabaya".

    Waziri wa afya wa Lebanon ameiambia BBC kinachoendelea nchini mwake ni "mauaji", huku hospitali zikijitahidi kukabiliana na idadi ya waliofariki kutokana na mashambulizi ya anga ya Israel kwa siku mbili yanayolenga Hezbollah.

    Alipoulizwa na waandishi wa habari jinsi waziri mkuu wa Uingereza atahakikisha hali hiyo hairudii machafuko katika mji mkuu wa Afghanistan Kabul wakati Taliban walipochukua udhibiti mnamo Agosti 2021, Sir Keir alisema: "Ujumbe muhimu zaidi kutoka kwangu kwa raia wa Uingereza huko Lebanon, ni kuondoka mara moja.

    "Ni muhimu kwamba tumekuwa wazi kabisa: sasa ni wakati wa kuondoka."

    Chanzo kikuu cha serikali kiliongeza kuwa tofauti, kwa sasa, ni kwamba kulikuwa na ndege za kibiashara zinazoondoka Lebanon.

    Mawaziri wamerudia wito wao wa kusitisha mapigano mara moja.

    Waziri wa Ulinzi John Healey alisema: "Tunaendelea kuzihimiza pande zote kurudi nyuma kutoka kwa mzozo ili kuzuia hasara zaidi ya kupoteza maisha.

    “Serikali yetu inahakikisha maandalizi yote yanafanyika kusaidia raia wa Uingereza iwapo hali itazidi kuwa mbaya.

    "Nataka kuwashukuru wafanyikazi wa Uingereza ambao wapo katika eneo hili kwa kujitolea na taaluma yao."

    Healey alifanya mkutano na mawaziri wenzake, wakuu wa kijasusi na wanadiplomasia siku ya Jumanne mchana ili kufanyia kazi mipango ya serikali.

    Soma zaidi:

  15. ‘Wafanyakazi wetu ni miongoni mwa waliouawa katika mashambulizi ya anga ya Israel’ - UN

    Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi linasema mmoja wa wafanyakazi wake na mmoja wa watoto wake waliuawa katika shambulio la anga la Israel mashariki mwa Lebanon - mojawapo ya zaidi ya mashambulizi elfu kama hayo katika muda wa siku mbili zilizopita.

    UNHCR ilisema kuwa nyumba ya Dina Darwiche ilishambuliwa siku ya Jumatatu.

    Mumewe na mwanawe mkubwa waliokolewa na wako hospitalini wakiwa na majeraha mabaya, shirika hilo lilisema.

    Bi Darwiche alikuwa amefanya kazi katika ofisi ya UNHCR ya Bekaa kwa miaka 12.

    Wakati huo huo Ali Basma, ambaye alikuwa amefanya kazi katika ofisi ya UNHCR katika mji wa kusini wa Tiro ambaye anashughulika na usafi, pia aliuawa.

    Katika taarifa, shirika hilo lilisema "limeghadhabishwa na kuhuzunishwa sana" na mauaji yao.

    "Mashambulizi ya anga ya Israel nchini Lebanon sasa yamesababisha mauaji ya mamia ya raia," mkurugenzi wa kimataifa wa UNHCR Filippo Grandi alisema Jumanne.

    "Na ninasikitika sana kuthibitisha kwamba wenzangu wawili wa UNHCR pia waliuawa hapo jana."

    Marafiki wa Bi Darwiche walimtaja kama "mtu mpole na mkarimu zaidi tuliyemjua."

    "Alikuwa amejitolea kwa kazi yake ya kutoa misaada ya kibinadamu na UNHCR kwa muda mrefu niwezavyo kukumbuka," aliandika Profesa Jasmin Lilian Diab, msomi katika Chuo Kikuu cha Lebanon cha Marekani, kwenye mtandao wa X. "Nimevunjika moyo. Nimeumia kabisa."

    Mazishi ya waliouawa yamekuwa yakifanyika kote Lebanon.

    Katika mji wa kusini wa Sidon, Mohammed Hilal alikuwa amekusanyika pamoja na mamia ya waombolezaji wengine kumuaga bintiye katika mazishi ambayo pia yalifanywa kwa ajili ya watu wengine wanane.

    Wanachama watatu wa Hezbollah walikuwa miongoni mwa waliozikwa, kulingana na shirika la habari la Reuters ambalo lilirekodi tukio hilo.

    Soma zaidi:

  16. Ryan Routh ashtakiwa kwa jaribio la kumuua Trump

    Waendesha mashtaka nchini Marekani wamemfungulia mashtaka mwanamume aliyekamatwa karibu na uwanja wa gofu wa Donald Trump wa Florida kwa jaribio la kumuua mgombeaji urais.

    Hili linawadia siku moja baada ya jalada la mahakama kuonyesha Ryan Wesley Routh alikuwa ameandika barua miezi kadhaa iliyopita akisema alikusudia kumuua Trump.

    Routh, 58, tayari anakabiliwa na hadi miaka 20 jela kwa mashtaka mawili yanayohusiana na bunduki.

    Lakini anakabiliwa na kifungo cha juu zaidi cha maisha jela ikiwa atapatikana na hatia kwa mashtaka mapya na makubwa zaidi.

    "Vurugu zinazolenga maafisa wa umma zinahatarisha kila kitu ambacho nchi yetu inasimamia," Mwanasheria Mkuu wa Marekani Merrick Garland alisema katika taarifa, akiapa "kutumia kila chombo kilichopo" kumuwajibisha Routh.

    Trump ameishutumu serikali kwa kushughulikia kesi hiyo vibaya, akiandika katika ujumbe wa mtandao wa kijamii siku ya Jumatatu kwamba wizara ya sheria inapaswa "KUACHA FLORIDA ISHUGHULIKIE KESI HIYO!"

    Lakini Garland alikataa hilo, akiwaambia waandishi wa habari siku ya Jumanne kwamba shirika lake "litatafuta kushirikiana na kupata usaidizi kutoka kwa" maafisa wa serikali "kulingana na sheria".

    Nyaraka za mahakama zinaonyesha kesi hiyo imetolewa bila kufuata mpango maalumu kwa Jaji wa Wilaya ya Marekani Aileen Cannon.

    Bi Cannon ndiye jaji wa Florida Kusini ambaye alipewa kesi ya hati za siri za serikali ya Trump mwaka jana na ambaye aliitupilia mbali mapema mwaka huu. Uamuzi wake kwa sasa uko chini ya rufaa.

    Jaji tofauti mnamo siku ya Jumatatu aliamuru Routh abaki rumande baada ya waendesha mashtaka kuhoji kuwa alikuwa na uwezekano wa kutoroka nchi na hatari kwa jamii.

    Mshukiwa anazuiliwa katika kituo cha kizuizini huko Florida Kusini tangu kukamatwa kwake tarehe 15 Septemba.

    Soma zaidi:

  17. Aina mpya ya ‘Papa zimwi’ yagunduliwa katika maji ya New Zealand

    Wanasayansi wa New Zealand wamegundua aina mpya ya "Papa zimwi" - aina adimu ya samaki ambao ni vigumu sana kuwaona kwa sababu wanaishi kwenye kina kirefu katika Bahari ya Pasifiki.

    Pia anajulikana kama spookfish au chimera, na wana uhusiano wa karibu na papa wa kawaida na samaki wa Ray fish. Hawana magamba na mifupa yao imetengenezwa kwa katileji kabisa.

    Dk Brit Finucci, mmoja wa wanasayansi waliogundua samaki aina ya Australasian Narrow-nosed Spookfish, alisema ugunduzi huo ulikuwa "wa kusisimua".

    "Makazi yao yanawafanya kuwa wagumu kusoma na kufuatilia, ikimaanisha kuwa hatujui mengi kuhusu biolojia yao au hali ya tishio," alisema.

    Dk Finucci na watafiti wengine kutoka Taasisi ya Kitaifa ya Maji na Utafiti wa Anga ya New Zealand (Niwa) walimpata kiumbe huyo katika eneo la sakafu ya bahari linalojulikana kama Chatham Rise, ambalo liko mashariki mwa New Zealand.

    Papa zimwi kwa kawaida huishi kwenye kina cha hadi 2,600m (maili 1.6).

    Dk Finucci alisema spishi hiyo ilitofautishwa na pua yake ndefu isiyo ya kawaida, ambayo inaweza kusheheni nusu ya urefu wa mwili wake.

    Amempa samaki huyo mpya jina la kisayansi: Harriota avia.

    "Avia inamaanisha nyanya kwa Kilatini, nilitaka kumpa taadhima hii kwa sababu aliniunga mkono kwa fahari kupitia kazi yangu kama mwanasayansi," Dk Finucci alielezea.

    Pia unaweza kusoma:

  18. Mashambulizi ya Israel nchini Lebanon yanasababisha 'mauaji ya watu wengi' waziri wa afya asema

    Waziri wa afya wa Lebanon amesema kinachoendelea nchini mwake ni "mauaji", huku hospitali zikijitahidi kukabiliana na idadi ya waliopoteza maisha kutokana na mashambulizi ya anga ya Israel yaliyoenea kwa siku mbili yakilenga kundi la Hezbollah.

    Dkt Firass Abiad aliiambia BBC ni "wazi" kwamba wengi wa watu 550 waliouawa katika mashambulizi ya Jumatatu walikuwa raia, ikiwa ni pamoja na watoto na wanawake.

    Israel ilisema ilishambulia mamia ya maeneo ya Hezbollah, ikilishutumu kundi hilo kwa kuficha silaha katika maeneo ya makazi.

    Siku ya Jumanne, jeshi la Israel lilimuua mkuu wa vikosi vya roketi vya Hezbollah wakati mashambulio hayo yakiendelea, huku Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu akisema kundi hilo lilikuwa linaiongoza Lebanon "kuzimu".

    Hezbollah ilijibu kwa kurusha zaidi ya roketi 300 kaskazini mwa Israel, na kujeruhi watu sita, kulingana na jeshi.

    Ijapokuwa hakuna upande ulionekana kuwa na nia ya kurudi nyuma, Rais wa Marekani Joe Biden aliliambia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwamba mzozo kamili "haukuwa wa maslahi ya mtu yeyote" na kusisitiza kwamba "suluhisho la kidiplomasia bado linawezekana".

    Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres alionya kwamba ulimwengu "hauwezi kumudu Lebanon kuwa Gaza nyingine".

    Takriban mwaka mmoja wa mapigano ya kuvuka mpaka kati ya Israel na Hezbollah yaliyochochewa na vita huko Gaza, yameua mamia ya watu wengi wao wakiwa wapiganaji wa Hezbollah, na maelfu ya wengine kuyahama makazi yao pande zote mbili za mpaka huo.

    Hezbollah imesema inaiunga mkono Hamas na haitakoma hadi kutakapokuwa na usitishaji vita huko Gaza.

    Makundi yote mawili yanaungwa mkono na Iran na yamepigwa marufuku kuwa mashirika ya kigaidi na Israel, Uingereza na nchi nyinginezo.

    Soma zaidi:

  19. Bila shaka hujambo msomaji wetu, karibu katika matangazo ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 25/9/2024