Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Uingereza yaunga mkono mpango wa haki za binadamu unaolenga kuondolewa kwa wahamiaji haramu

Tamko hilo limesainiwa na wanachama wote 46 wa chombo cha kisiasa kinachosimamia mahakama ya haki za binadamu na ambacho ni tofauti kabisa na Umoja wa Ulaya.

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Uingereza yaunga mkono mpango wa haki za binadamu unaolenga kuondolewa kwa wahamiaji haramu

    Uingereza pamoja na mataifa mengine ya Ulaya yamesaini tamko muhimu linalotaka mahakama kutathmini upya namna zinavyotoa maamuzi kuhusu kesi za uhamiaji, katika juhudi za kurahisisha kuwafukuza wahamiaji haramu.

    Makubaliano hayo, yaliyotangazwa katika mkutano uliofanyika Moldova siku ya Ijumaa, yanaonya kuwa demokrasia ya Ulaya inaweza kudhoofishwa ikiwa nchi hazitaweza kukabiliana kwa ufanisi zaidi na usafirishaji haramu wa watu pamoja na shinikizo la kisasa la uhamiaji.

    Tamko hilo linataka nchi wanachama kuachiwa mamlaka makubwa zaidi katika kushughulikia kesi za uhamiaji.

    Akizungumza kabla ya mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza, Yvette Cooper, alieleza makubaliano hayo kuwa ni “mbinu ya busara” na kusema anataka kuhakikisha mifumo hiyo “haitumiwi vibaya kwa njia isiyo ya haki.”

    Tamko hilo jipya si mabadiliko rasmi ya sheria za haki za binadamu, jambo ambalo linaweza kuchukua miaka mingi, bali ni ishara ya kisiasa kutoka kwa nchi zote wanachama kwenda kwa majaji wa haki za binadamu kwamba wanapaswa kuzingatia zaidi maslahi ya umma na demokrasia wanapotoa maamuzi kuhusu kesi za uhamiaji.

    Tamko hilo limesainiwa na wanachama wote 46 wa chombo cha kisiasa kinachosimamia mahakama ya haki za binadamu na ambacho ni tofauti kabisa na Umoja wa Ulaya.

    Waraka huo unasema kuwa changamoto zinazozikabili nchi za Ulaya zimebadilika kwa kiwango kikubwa au hazikutarajiwa wakati mkataba wa haki za binadamu ulipoandaliwa.

  2. Trump amesema “hakutoa ahadi yoyote” kwa Xi Jinping kuhusu Taiwan

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa “hakutoa ahadi yoyote upande wowote” kuhusu Taiwan wakati wa mazungumzo yake na Rais wa China, Xi Jinping.

    Akiwa kwenye safari ya kurejea Washington baada ya mkutano wa siku mbili mjini Beijing, Trump aliwaambia waandishi wa habari kuwa wawili hao “walizungumza sana” kuhusu Taiwan, kisiwa kinachojitawala ambacho China inadai kuwa sehemu ya eneo lake na haijaondoa uwezekano wa kukichukua kwa nguvu.

    Trump alisema Xi aliuliza moja kwa moja kama Marekani ingeilinda Taiwan iwapo kungetokea mzozo, naye akajibu: “Sizungumzii hilo.”

    Rais huyo wa Marekani pia alisema atafanya uamuzi “katika muda mfupi” kuhusu kama ataendelea na mpango uliotangazwa awali wa Marekani kuuza silaha kwa Taiwan, jambo ambalo China imelipinga vikali.

    Taiwan imekuwa mshirika wa muda mrefu wa Marekani, na sheria za Marekani zinaibana Washington kuhakikisha kisiwa hicho kinapata uwezo wa kujilinda.

    Tawala tofauti za Marekani zimekuwa zikijaribu kudumisha usawa wa kidiplomasia kwa kuendelea kuwa na uhusiano na Taiwan huku pia zikijenga mahusiano na Beijing.

    Hata hivyo, usawa huo umeendelea kujaribiwa katika miaka ya hivi karibuni huku China ikiongeza mazoezi ya kijeshi karibu na Taiwan, jambo lililoongeza mvutano katika eneo hilo na kuisumbua Washington.

    Mwishoni mwa mwaka jana, utawala wa Trump ulitangaza mpango wa kuuza silaha kwa Taiwan wenye thamani ya dola bilioni 11 za Marekani, ukiwemo mfumo wa kisasa wa kurusha makombora na aina mbalimbali za makombora mengine.

    Unaweza kusoma;

  3. Mwalimu anayeshukiwa kuwa mnyanyasaji wa watoto anaswa kwa AI

    Mwalimu mstaafu wa michezo nchini Ufaransa anashikiliwa na polisi baada ya kunaswa akifanya mazungumzo ya kingono mtandaoni kwa msichana wa miaka 14.

    Hata hivyo, “msichana” huyo wa miaka 14 hakuwa msichana halisi.

    Alikuwa sura na sauti zilizotengenezwa kwa teknolojia ya akili mnemba, zikisimamiwa na mshawishi maarufu wa mtandaoni wa kiume anayejulikana kwa kuwatega wanaoshukiwa kuwa wabakaji wa watoto.

    Mwalimu huyo wa zamani mwenye umri wa miaka 66, aliyetajwa kama Dominique B, alijisalimisha kwa polisi mashariki mwa Ufaransa siku ya Jumanne, siku moja baada ya mazungumzo yake na “msichana” huyo kurushwa kwenye majukwaa mbalimbali ya mtandaoni.

    Katika video hiyo, Dominique B anaonekana upande mmoja wa skrini akiwa ameketi kwenye kiti, huku upande mwingine akiwa mshawishi huyo anayejulikana kama FINNYZYY, akiwa ametumia sura na sauti ya msichana kupitia teknolojia ya AI.

    Mabadiliko hayo ya picha hayakuwa ya kiwango cha juu sana, mshawishi huyo alilazimika kufunika sehemu ya chini ya kidevu chake ili kuficha ndevu zake lakini yalionekana kutosha kumdanganya mwalimu huyo mstaafu.

    Katika mazungumzo ya dakika 40, yaliyotazamwa moja kwa moja na zaidi ya watu 40,000 na kuonekana karibu mara milioni moja tangu hapo, Dominique B aliomba kukutana na “msichana” huyo katika uwanja wa mpira wa miguu wa Parc des Princes mjini Paris.

    Pia alimuuliza kama angependa kumbusu, kama amewahi kushiriki picha za utupu na marafiki zake, na kama angependa kumuona akiwa utupu.

    Alipokumbushwa kuwa “msichana” huyo ana umri wa miaka 14 tu, mwanaume huyo alipuuza hoja hiyo kwa kusema kwamba wasichana wengi “wadogo kuliko huyo tayari wamewahi kufanya mapenzi.”

    Mwanaume huyo alitambuliwa na baadhi ya watazamaji waliotoa taarifa kwa Pharos, jukwaa la serikali ya Ufaransa la kuripoti maudhui ya mtandaoni yanayohatarisha usalama.

    Kabla mamlaka hazijachukua hatua, Dominique B alijipeleka mwenyewe katika kituo cha polisi cha eneo lake.

    Mwendesha mashtaka wa serikali mjini Vesoul alisema anakabiliwa na mashtaka ya kuomba ngono kwa mtu mwenye umri chini ya miaka 15, pamoja na kuomba picha za mtoto kwa madhumuni ya ponografia.

  4. Trump, Xi wahitimisha mazungumzo yaliyoelezwa kuwa “yenye mafanikio makubwa”

    Rais wa Marekani, Donald Trump, ameondoka Beijing baada ya mkutano wa siku mbili akisema kuwa amefanikisha “makubaliano mazuri ya biashara, yenye manufaa kwa nchi zote mbili,” lakini hadi sasa maelezo machache yametolewa kuhusu kile ambacho mataifa hayo mawili yenye nguvu kubwa duniani yalikubaliana.

    Trump aliwasili kwa mkutano muhimu na kiongozi wa China, Xi Jinping, siku ya Jumatano akiwa ameandamana na wakurugenzi wakuu wa makampuni mbalimbali kutoka sekta za kilimo, usafiri wa anga, magari ya umeme na teknolojia ya akili mnemba (AI).

    Biashara ilikuwa moja ya ajenda kuu licha ya mvutano wa hivi karibuni kuhusu vita vya Iran, huku wafanyabiashara wakitarajia kufikiwa kwa makubaliano muhimu pamoja na kuongezwa kwa muda wa kusitisha ushuru wa bidhaa, ambao unatarajiwa kuisha mwezi Novemba.

    Ziara hiyo ilijaa kauli za urafiki na ishara za kidiplomasia. Trump alipokelewa kwa ratiba maalum iliyojumuisha gwaride la heshima, chakula cha kitaifa na mwaliko wa kutembelea eneo maalum wanakoishi na kufanya kazi viongozi wa Chama cha Kikomunisti cha China.

    Rais huyo wa Marekani alionekana kufurahishwa na mapokezi hayo na akamualika Xi kutembelea White House mwezi Septemba. Trump alisema mazungumzo yalikuwa “yenye mafanikio makubwa,” huku Xi akiita ziara hiyo kuwa “ya kihistoria na yenye alama muhimu.”

    Hata hivyo, hakuna upande uliotangaza mafanikio makubwa ya biashara au mikataba muhimu ya uwekezaji.

    Katika mahojiano na Fox News, Trump alisema kuwa China itawekeza mamia ya mabilioni ya dola kupitia viongozi wa biashara walioandamana naye nchini humo, lakini hakutoa maelezo zaidi.

    Pia alisema China imekubali kuagiza ndege 200 za Boeing, ikiwa ni mara ya kwanza kwa China kununua ndege za biashara zilizotengenezwa Marekani karibu muongo mmoja, ingawa idadi hiyo ni ndogo kuliko ilivyotarajiwa na wachambuzi.

  5. Marekani kumfungulia mashtaka kiongozi wa zamani wa Cuba, Raul Castro

    Msemaji wa Wizara ya Sheria ya Marekani alisema Alhamisi jioni kuwa Marekani inapanga kumfungulia mashtaka aliyekuwa Rais wa Cuba, Raul Castro, ambaye ni ndugu wa kiongozi wa mapinduzi wa Cuba, Fidel Castro.

    Bado haijulikani ni lini hasa mashtaka hayo, ambayo lazima yaidhinishwe na baraza kuu la mahakama yatawasilishwa rasmi.

    Hata hivyo, kwa mujibu wa afisa mmoja wa Idara ya Haki ambaye hakutajwa jina na alinukuliwa na mashirika ya habari, hatua hiyo inaweza kuchukuliwa hivi karibuni.

    Kwa mujibu wa mashirika hayo, kesi dhidi ya Raul Castro inahusishwa na tukio la miaka 30 iliyopita ambapo Cuba iliidungua ndege ya shirika la misaada ya kibinadamu la “Brothers to the Rescue.”

    Ripoti kuhusu uwezekano wa kufunguliwa mashtaka dhidi ya Raul Castro zimeibuka wakati Mkurugenzi wa CIA, John Ratcliffe, alipokuwa mjini Havana kuwasilisha ujumbe kutoka kwa Rais wa Marekani, Donald Trump, kwa viongozi wa Cuba.

    Washington ilisema kuwa Marekani iko “tayari kwa mazungumzo ya kina kuhusu masuala ya uchumi na usalama, lakini tu ikiwa Cuba itafanya mabadiliko ya msingi.”

    Ingawa Cuba ilieleza mkutano huo kama jaribio la kuanzisha mazungumzo, uwezekano wa hatua za kisheria unaonekana kuwa njia ya Marekani kuongeza shinikizo dhidi ya Cuba.

    Unaweza kusoma;

  6. Mlipuko mpya wa virusi vya Ebola waua watu 65 DRC

    Mlipuko wa ugonjwa wa Ebola umeripotiwa katika wilaya ya Ituri mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

    Takriban visa 246 na vifo 65 vimeripotiwa, katika miji ya uchimbaji dhahabu ya Mongwalu na Rwampara, hii ni kulingana na taarifa kutoka Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC).

    Ugonjwa wa Ebola uligunduliwa kwa mara ya kwanza mwaka wa 1976 nchini DRC na inaaminika kuwa ilisambazwa kutoka kwa popo. Huu ni mlipuko wa 17 wa ugonjwa huo hatari nchini humo.

    Ugonjwa huo husambazwa kupitia kugusana wa moja kwa moja, na husababisha kutokwa damu pamoja na kufeli kufanya kazi kwa viungo vya mwili.

    Dalili za ugonjwa huu ni homa, maumivu ya misuli, uchovu, maumivu ya kichwa na koo. Hakuna tiba ya Ebola hadi sasa.

    Unaweza kusoma;

    • Mpelelezi wa virusi ambaye aligundua Ebola mwaka 1976
    • Kwanini waliopona Ebola wanaambiwa waepuke kujamiiana kabla ya siku 90?
  7. Trump na Xi wanakula nini wakati wa chakula cha mchana?

    Rais wa Marekani, Donald Trump na Rais wa China Xi Jinping kwa sasa wanashiriki chakula cha mchana cha kikazi. Kwa mujibu wa Ikulu ya Marekani, menyu yao inajumuisha:

    • Samaki aina ya kamba iliyokaangwa kwa ukoko mkavu na kwa mtindo wa kuchochewa jikoni.
    • Supu ya dagaa yenye samaki aina ya chewa waliokatwakatwa
    • Minofu ya nyama ya ng’ombe iliyokaangwa na kujazwa uyoga aina ya morel
    • Kuku wa Kung Pao na scallops
    • Mboga za kienyeji zilizochemshwa pamoja na machipukizi ya mianzi, uyoga na maharagwe
    • Nyama ya ng’ombe ya mchuzi ndani ya mkate
    • Andazi iliyotengezwa na nyama ya nguruwe na kamba iliyopikwa kwa mvuke
    • Keki ya chokoleti
    • Matunda na aiskrimu
    • Kahawa au chai

    Wakati huo huo, waandishi wa habari wanaosafiri na msafara wa Ikulu ya Marekani wameagiziwa chakula cha McDonald's na kupelekewa kwenye magari yao.

  8. Waitaliano watano wafariki wakati wa kupiga mbizi kwenye mapango ya kisiwa cha Maldives

    Raia watano wa Italia wamefariki katika ajali ya kupiga mbizi (scuba diving) katika kisiwa cha Maldives, wizara ya mambo ya nje mjini Roma imesema.

    Wizara hiyo imesema waogeleaji hao wanaaminika kufariki wakati wakijaribu kuchunguza mapango katika kina cha mita 50 (futi 164), tukio lililotokea katika eneo la Vaavu Atoll.

    Jeshi la Maldives limesema mwili mmoja umepatikana ndani ya pango lililoko takriban mita 60 chini ya maji, huku waogeleaji wengine wanne wakiaminika bado wako eneo hilo.

    Limesema waokoaji wenye vifaa maalum wametumwa eneo la tukio, likieleza kuwa operesheni ya utafutaji ni ya hatari kubwa sana.

    Tukio hilo linaaminika kuwa ajali mbaya zaidi ya kupiga mbizi kuwahi kutokea katika taifa hilo dogo la Bahari ya Hindi, ambalo ni kivutio kikubwa cha watalii kutokana na visiwa vyake vya matumbawe.

    Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya eneo hilo, Waitaliano hao waliingia majini Alhamisi asubuhi.

    Wafanyakazi wa boti ya kupiga mbizi waliokuwa wakisafiri nao waliripoti kutoweka kwao baada ya kushindwa kurejea juu ya maji kwa wakati uliotarajiwa.

    Polisi walisema hali ya hewa ilikuwa mbaya katika eneo hilo, takriban kilomita 100 kusini mwa mji mkuu Malé, na onyo la njano lilitolewa kwa boti za abiria na wavuvi.

    Unaweza kusoma pia:

  9. FBI yatoa zawadi ya dola 200,000 kumtafuta afisa wa zamani wa ujasusi anayedaiwa kuipeleleza Iran

    Kitengo cha kijasusi cha Marekani cha FBI kimetangaza zawadi ya dola 200,000 kwa yeyote atakayetoa taarifa zitakazosaidia kumkamata Monica Witt, afisa wa zamani wa ujasusi wa anga na upelelezi wa kijeshi.

    Katika taarifa iliyotolewa Alhamisi Mei 14, FBI ilieleza kuwa Witt aliwahi kuhudumu katika jeshi la anga la Marekani kati ya mwaka 1997 na 2008, na baadaye kufanya kazi kama mwanakandarasi wa serikali ya Marekani hadi mwaka 2010. Ilisema majukumu yake yalimpa upatikanaji wa taarifa za siri na za juu kabisa kuhusu ujasusi wa kigeni na upelelezi wa kijeshi, ikiwemo utambulisho wa maafisa wa siri wa taasisi za ujasusi za Marekani.

    Kwa mujibu wa FBI, Witt alikimbilia Iran mwaka 2013. Inadaiwa kuwa baadaye alitoa taarifa kwa serikali ya Iran zilizoathiri usalama wa taarifa za siri za ulinzi wa taifa la Marekani na programu zake za kijeshi.

    Aidha, anatuhumiwa kufichua taarifa zilizohatarisha maisha ya wanajeshi wa Marekani walioko nje ya nchi pamoja na familia zao, na pia kuwasaidia Wairani kuwatafuta maafisa wa zamani wa serikali ya Marekani ili washambuliwe.

    FBI imesema kuwa licha ya shtaka dhidi yake, bado hayupo mikononi mwa sheria.

    Mwisho wa taarifa hiyo, FBI imetangaza zawadi hiyo ya dola 200,000 na kuomba ushirikiano wa umma katika kumsaidia kumtafuta na kumkamata afisa huyo wa zamani wa ujasusi.

    Pia unaweza kusoma pia:

  10. Trump: China yataka Mlango wa Hormuz ubaki wazi

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema kuwa China inataka Mlango wa bahari wa Hormuz ubaki wazi, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu kwa usafirishaji wa mafuta.

    Aidha amesema China inanunua kiasi kikubwa cha mafuta kupitia eneo hilo, na hivyo inapendelea shughuli hizo ziendelee bila vikwazo.

    Trump ameongeza kuwa Rais wa China Xi Jinping ameonyesha utayari wa kusaidia kufanikisha makubaliano ya kuhakikisha mlango huo unabaki wazi.

    “Yeyote anayenunua kiasi hicho cha mafuta ana uhusiano fulani nao, lakini alisema angependa kusaidia endapo ataweza,” Trump amesema, akisisitiza kuwa China ingependa kuona Mlango wa Hormuz ukiendelea kuwa wazi.

    Pia Trump amemalizia kwa kusema Marekani na China wana mtazamo unaofanana kuhusu suala la Iran.

    Pia unaweza kusoma:

  11. Bendera ya Israel yapeperushwa katika msikiti wa Al Aqsa

    Waziri wa Usalama wa Kitaifa wa mrengo wa kulia nchini Israel, Itamar Ben-Gvir, amevunja utaratibu wa muda mrefu unaohusu maeneo ya ibada ya dini tofauti katika eneo hilo baada ya kupeperusha bendera ya Israel karibu na Msikiti wa Al Aqsa.

    Video zilizochapishwa zinaonyesha waziri huyo akiinua bendera ya Israel huku wimbo wenye maneno “Msikiti mtukufu wa Al Aqsa uko mikononi mwetu” ukisikika.

    Maelfu ya Waisraeli pia wamefanya maandamano katika eneo hilo wakishiriki tukio la kila mwaka la kidini na kitaifa.

    Maandamano hayo yanayojulikana kama “Flag March” hufanyika kuadhimisha kumbukumbu ya Israel kuteka Jerusalem Mashariki wakati wa vita vya mwaka 1967.

    Mwandishi wa BBC mjini Jerusalem amesema kuwa tukio hilo mara nyingi huambatana na vurugu, misukosuko pamoja na kauli za kibaguzi dhidi ya Wapalestina wanaoishi katika maeneo hayo ya Jerusalem.

    Mwaka huu, makumi ya wanaharakati wa amani kutoka Israel walijaribu kuzuia kile walichokitaja kuwa vitendo vya ukatili vinavyoambatana na maandamano hayo.

    Soma zaidi:

  12. Bei ya mafuta yapanda kwa kiwango cha juu nchini Kenya

    Wakenya wameingiwa na wasiwasi baada ya serikali kuongeza bei ya rejareja ya dizeli kwa Shilingi 46.29 za Kenya kwa lita na petroli kwa Shilingi 16.65 za kenya katika tangazo lililotolea na Mamlaka ya kudhibiti kawi na nishati ya (EPRA).

    Jijini Nairobi, Petroli itauzwa kwa shilingi 214.25 za Kenya, wanaotumia dizeli ikiwalazimu kuinunua kwa shilingi 242.92 za Kenya huku watumiaji wa mafuta ya taa kuipata bidhaa hiyo na shilingi 152.78 za Kenya kwa kila lita kuanzia Alhamisi kwa siku 30 zijazo.

    Kwa mujibu wa wachangunizi wa kiuchumi, ongezeko hilo linatarajiwa kuongeza gharama za utengenezaji na usafirishaji, hali inayoweza kusababisha wawekezaji na wafanyabiashara kuongeza bei za bidhaa kwa wanunuzi.

    Katika taarifa iliyotolewa Alhamisi, EPRA imesema bei ya mafuta ya taa haitabadilika katika kipindi cha bei kitakachoanza leo Mei 15 hadi Juni 14, 2026.

    Hatua hiyo inafuta nafuu iliyoshuhudiwa mwezi uliopita baada ya serikali kupunguza kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kutoka asilimia 13 hadi asilimia 8 kupitia Tangazo la Kisheria Na. 70 la Aprili 15, 2026.

    “Katika kipindi hiki cha tathmini, bei ya juu inayoruhusiwa ya petroli imeongezeka kwa Shilingi 16.65 za Kenya kwa lita na dizeli kwa Shilingi 46.29 za Kenya kwa lita, huku mafuta ya taa yakibaki bila mabadiliko,” EPRA imesema.

    Mamlaka hiyo ilieleza kuwa ongezeko hilo limetokana na kupanda kwa bei za mafuta katika soko la kimataifa pamoja na gharama kubwa za kuagiza mafuta kutoka nje.

    Kwa mujibu wa EPRA, wastani wa gharama ya kuagiza petroli uliongezeka kwa asilimia 10 kutoka dola 823.27 za Marekani kwa mita ya ujazo mwezi Machi 2026 hadi dola 906.23 mwezi Aprili.

    Dizeli ilirekodi ongezeko kubwa zaidi la asilimia 20.32, kutoka dola 1,073.82 hadi dola 1,291.98 kwa mita ya ujazo katika kipindi hicho.

    EPRA ilibainisha kuwa bidhaa za mafuta katika soko la kimataifa huuzwa kwa dola za Marekani, hivyo huathiriwa na mabadiliko ya bei ya mafuta duniani pamoja na viwango vya ubadilishaji fedha za kigeni.

    Bei hizo pia zinajumuisha VAT kwa mujibu wa Sheria ya ushuru wa thamani VAT, Sheria ya Fedha na viwango vipya vya ushuru wa bidhaa.

    Mamlaka hiyo imeongeza kuwa serikali itatumia takriban Shilingi bilioni 5 za Kenya kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Petroli kusaidia kupunguza makali ya ongezeko la bei ya dizeli na mafuta ya taa kwa watumiaji.

    Katika kipindi kilichopita, petroli ilikuwa ikiuzwa kwa Shilingi 197.60 kwa lita pesa za Kenya huku dizeli ikiuzwa kwa Shilingi 196.63 za Kenya baada ya kupunguzwa kwa Shilingi 9.37 na Shilingi 10.21 mtawalia za Kenya.

    Tangazo hili jipya linajiri wakati soko la mafuta duniani likiendelea kubadilika na huku gharama ya maisha ikiendelea kuongezeka.

    Soma zaidi:

  13. Trump asema China sasa kununua mafuta Marekani na kutoipatia silaha Iran

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema mazungumzo ya biashara kati ya Marekani na China “yamekwenda vizuri zaidi kuliko mara ya mwisho”, akieleza kuwa safari hii yalikuwa makubwa zaidi kuliko makubaliano 36 yaliyosainiwa katika mazungumzo yaliyopita.

    Trump amesema China itanunua kiasi kikubwa cha mazao ya kilimo kutoka Marekani, ikiwemo maharage ya soya.

    Alipoulizwa na mtangazaji wa Fox News Sean Hannity kuhusu kile ambacho China inataka kutoka Marekani, Trump alijibu: “Ni mambo mengi sana ya kujadili, lakini yapo mengi,” bila kutoa maelezo zaidi.

    Katika mazungumzo hayo, Trump pia amesema China imekubali kununua mafuta kutoka Marekani.

    “Tutaona meli za China zikielekea Texas, Louisiana na Alaska,” anasema, akiongeza kuwa nishati ndiyo bidhaa ambayo China inaihitaji zaidi.

    “Tunayo nishati isiyo na kikomo,” alisema.

    Sasa zaidi kuhusu vita vya Iran, Trump anasema aliwaambia wenzake wa China kwamba Marekani ilikuwa "ikiwasaidia" kweli.

    "Sidhani kama China inataka Iran iwe na silaha ya nyuklia," Trump anasema.

    Trump pia amedai kuwa Rais wa China Xi Jinping amekubali kununua ndege 200 za kampuni ya Boeing, akieleza hatua hiyo kama “ahadi kubwa”.

    “Ndege 200 kubwa, hiyo ni ajira nyingi. Boeing walitaka 150, lakini wamepata 200,” alisema.

    Mapema, Waziri wa Hazina wa Marekani alikuwa amedokeza uwezekano wa China kutangaza oda kubwa ya ndege za Boeing, akiiambia CNBC kuwa Beijing huenda ikatangaza rasmi ununuzi huo hivi karibuni.

    Trump amehitimisha kwa kusema amefanikisha zaidi kuliko viongozi wengine katika kushughulikia biashara na China, akidai nakisi ya biashara kati ya nchi hizo imepungua kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na ilivyokuwa awali.

    Trump na wafanyibiashara alioandamana nao China watakamilisha ziara yao hii leo.

    Soma zaidi:

  14. Hujambo na karibu kwa matangazo ya moja kwa moja ya Ijumaa ya tarehe 15 Mei 2026.