Sri Lanka: Rais Rajapaksa akubali kuachia ngazi baada ya maelfu ya raia kuvamia makazi yake

Rais wa Sri Lanka Gotabaya Rajapaksa ametangaza kujiuzulu baada ya waandamanaji kuvamia makazi yake rasmi na kuchoma moto nyumba ya waziri mkuu.

Moja kwa moja

  1. Licha ya Rais Rajapaksa kutangaza kujiuzulu, waandamanaji Sri Lanka hawatondoka kwenye makazi yake

    Sri Lanka

    Chanzo cha picha, Google

    Maelezo ya picha, Baadhi ya waandamanaji wakiwa kwenye moja ya vyumba vya makazi ya rais Gotabaya Rajapaksa

    Waandamanaji wamesema hawataondoka na wataendelea kushikilia makaazi ya rais na waziri mkuu wa Sri Lanka hadi viongozi wote wawili watakapojiuzulu rasmi.

    Rais Gotabaya Rajapaksa alisema atajiuzulu tarehe 13 Julai, kulingana na tangazo lililotolewa na spika wa bunge siku ya Jumamosi. Lakini rais mwenyewe hajaonekana au kutoa taarifa kwa umma.

    Maelfu walifika Colombo Jumamosi wakimtaka ajiuzulu baada ya miezi kadhaa ya maandamano. Rais amelaumiwa kwa usimamizi mbaya wa uchumi wa nchi, ambao umesababisha uhaba wa chakula, mafuta na dawa kwa miezi kadhaa.

    Waziri Mkuu Ranil Wickremesinghe pia alisema atajiuzulu kufuatia maandamano ya Jumamosi, ambapo makazi yake ya binafsi yalichomwa moto. Pamoja na kutangazwa kuachia ngazi, lakini waandamanaji wanasalia na mashaka kuhusu nia ya viongozi hao.

  2. 15 wauawa kwa kufukiwa na vifusi vya ghorofa lililoshambuliwa na Urusi mashariki mwa Ukraine

    Russia Attack

    Chanzo cha picha, Reuters

    Takriban watu 15 wameuawa na wengine takriban 20 wanahofiwa kufukiwa na vifusi baada ya roketi za Urusi kushambulia jengo la ghorofa huko Chasiv Yar, mji ulioko mashariki mwa Ukraine, maafisa wanasema.

    Waathiriwa watano wamefanikiwa kuokolewa wakiwa hai. Idadi ya waliofariki ilitolewa na afisa wa huduma za dharura wa Ukraine. Upande mmoja wa jengo hilo la ghorofa tano ulipasuliwa na kuacha mlima wa kifusi.

    Chasiv Yar iko karibu na mji wa Kramatorsk, katika mkoa wa Donetsk. Donetsk ni lengo la kushinikiza Kirusi. Gavana wa eneo hilo Pavlo Kyrylenko alisema uharibifu huo ulisababishwa na roketi za Urusi za Uragan.

    Mtu aliyenusurika aitwaye Lyudmila aliliambia shirika la habari la Reuters "tulikimbia hadi kwenye ghorofa, kulikuwa na vibao vitatu, vya kwanza mahali fulani jikoni. "Pili, hata silikumbuki, kulikuwa na flash, tukakimbia kuelekea lango la pili na kisha moja kwa moja kwenye chumba cha chini. Tulikaa hapo usiku kucha hadi asubuhi."

    Siku ya Jumamosi wizara ya ulinzi ya Urusi iliripoti kwamba vikosi vyake viliharibu eneo lililokuwa limehifadhi ndege za Marekani M777 huko Chasiv Yar. BBC haikuweza kuthibitisha maelezo ya mashambulizi ya Chasiv Yar katika eneo la tukio.

  3. Maelfu waandamana Ikulu ya Marekani kutaka haki ya utoaji mimba isibatilishwe

    Roe v Wade: Thousands march to White House for abortion rights

    Chanzo cha picha, EPA

    Maelfu ya watu wameandamana katika mji mkuu wa Marekani siku ya Jumamosi, kupinga kubatilishwa kwa haki ya utoaji mimba mwezi uliopita. Maandamano hayo yanakuja wiki mbili baada ya Mahakama ya Juu kufuta Roe v Wade - uamuzi ambao ulikuwa umehakikisha utoaji wa mimba nchini kote kwa karibu miaka 50.

    Wakiimba "hatutarudi nyuma", waandamanaji walikusanyika kwenye Ikulu ya White House, huku mvua ikinyesha na wengine wakizuia lango la nje. Takriban watu 10,000 walikusanyika kutoka kote Marekani, waandaaji walisema.

    Lauren Pierce, 33, wakili kutoka Dallas, alikuwa miongoni mwa walioandamana, akisafiri maili 1,300 (2,100km) kuhudhuria maandamano.

    "Hakuna kitu, kwangu, chenye thamani zaidi kupigania kuliko sababu hii - haki yetu ya kimsingi ya kuwa na uhuru wa mwili," alisema. "Ikiwa hiyo inamaanisha nitakamatwa basi nadhani inafaa."

    Jimbo la nyumbani kwa Bi Pierce la Texas ni miongoni mwa majimbo 10 ya Marekani ambapo utoaji mimba tayari umepigwa marufuku. Angalau majimbo mengine kadhaa yanatarajiwa kufuata njia hiyo.

    Wanaharakati wa kupinga utoaji mimba, ambao wengi wao wanaona utoaji ama uavyaji mimba ni "mauaji", wamesherehekea uamuzi wa mahakama na fursa ya kuharamisha utaratibu huo katika maeneo mengine makubwa ya nchi.

  4. Kifo cha waziri mkuu wa zamani Abe: Polisi Japan wakiri kulikua na 'dosari' za kiusalama

    Abe

    Chanzo cha picha, AFP

    Polisi nchini Japan wamekiri kulikuwa na dosari katika usalama wa Waziri Mkuu wa zamani wa Japan Shinzo Abe, ambaye aliuawa kwa kupigwa risasi katika mji wa kusini wa Nara siku ya Ijumaa.

    "Ni jambo lisilopingika kwamba kulikuwa na matatizo katika usalama," alisema mkuu wa polisi wa Nara Tomoaki Onizuka.

    Mtu mwenye bunduki alimfyatulia risasi Abe katika hafla ya kampeni ya kisiasa - uhalifu ambao umeishangaza Japan. Uchaguzi wa Jumapili wa baraza la juu unaendelea kama ilivyopangwa. Upigaji kura ulianza saa 07:00 saa za ndani, ikiwa ni siku mbili tu baada ya kuuawa kwa Abe.

    Wachambuzi wanasema kuuawa kwake kunaweza kuongeza uungwaji mkono kwa chama tawala cha Liberal Democratic Party (LDP), ambacho Abe alikuwa kiongozi na mwenye ushawishi mkubwa.

    Uchaguzi wa baraza la juu la bunge lisilo na nguvu zaidi la Japan kwa kawaida huonekana kama kura ya maoni kuhusu serikali ya sasa. Lakini ushindi mkubwa kwa LDP utaimarisha uwezo wa waziri mkuu wa sasa wa kusukuma sera zake muhimu, ikiwa ni pamoja na kuongezeka maradufu kwa matumizi ya ulinzi.

    Polisi wanasema mshukiwa, aliyetajwa kwa jina la Tetsuya Yamagami, 41, alikuwa na chuki dhidi ya "shirika maalum". Vyombo vya habari vya Japan vinanukuu vyanzo vilivyo karibu na uchunguzi huo, ambavyo vinasema Yamagami aliamini Abe anahusishwa na kundi la kidini ambalo, Yamagami alidai, lilikuwa limemuharibia mama yake maisha na kifedha.

    Mshukiwa amekiri kumpiga risasi Abe na gobole ama bunduki ya kujitengenezea nyumbani, kwa mujibu wa polisi.

  5. 18 wauawa katika mashambulio mawili kwenye vilabu vya pombe huko Afrika Kusini

    Soweto

    Chanzo cha picha, Google

    Watu 14 wameuawa kwa kupigwa risasi kwenye baa ama klabu ya pombe moja huko Soweto usiku wa kuamkia leo, huku wengine tisa wakiwa katika hali mbaya hospitalini.

    Waathiriwa hao wanasemekana kuwa na umri wa kati ya miaka 19-35. Polisi wamesema washambuliaji kadhaa walikuwa wakifyatulia risasi watu bila mpangilio katika baa ya Orlando East kabla ya kukimbia eneo la tukio kwa kutumia gari ndogo nyeupe ya kukodisha (taxi).

    Makasha ya risasi za bunduki na bastola zilipatikana katika eneo la tukio. Mkuu wa polisi wa eneo la Gauteng, Luteni Jenerali Mawela ameambia BBC kwamba ufyatuaji risasi huo unaonekana kuwa "shambulio la damu kali dhidi ya walinzi wasio na hatia wa baa" na kwamba sababu ya ufyatuaji huo bado haijajulikana.

    Katika tukio lingine, watu wanne walipigwa risasi na kufa katika baa nyingine huko Pietermaritzburg, katika jimbo la Kwa-Zulu Natal. Pia sababu za shambulia hilo hazijulikani bado.

    Kwa mubiju wa vyombo vya ndani vya Afrika Kusini, matukio haya yanakuja wiki mbili tu baada ya vijana wengine 21 kukutwa wamekufa baa katika eneo lingine la East London. Vijana hao hawakukutwa na jeraha lolote.

  6. Sri Lanka: Rais Rajapaksa akubali kuachia ngazi baada ya maelfu ya raia kuvamia makazi yake

    Sri lanka

    Chanzo cha picha, AFP

    Rais wa Sri Lanka Gotabaya Rajapaksa ametangaza kujiuzulu baada ya waandamanaji kuvamia makazi yake rasmi na kuchoma moto nyumba ya waziri mkuu.

    Si Waziri Mkuu wala rais waliokuwa kwenye majengo wakati huo yakivamiwa. Mamia kwa maelfu waliwasili katika mji mkuu wa Colombo, wakimtaka Bw Rajapaksa ajiuzulu baada ya miezi kadhaa ya maandamano kuhusu hali mbaya na usimamizi mbovu wa kiuchumi.

    Bw Rajapaksa atajiuzulu tarehe 13 Julai. Waziri Mkuu Wickremesinghe amekubali kujiuzulu pia. Spika wa bunge alisema rais ameamua kujiuzulu "ili kuhakikisha makabidhiano ya amani ya mamlaka" na kutoa wito kwa umma "kuheshimu sheria". Tangazo hilo liliibua furaha na kupigwa kwa mafataki ya sherehe katika jiji hilo.

    Mmoja wa waandamanaji, Fiona Sirmana, ambaye alikuwa akiandamana kwenye nyumba ya rais, alisema ni wakati wa "kuwaondoa rais na waziri mkuu na kuwa na enzi mpya kwa Sri Lanka".

    "Ninasikitika hawakujiuzulu mapema kwa sababu kama wangeondoka mapema kusingekuwa na uharibifu wowote," aliiambia Reuters.

    Makumi ya watu walijeruhiwa katika maandamano ya Jumamosi, na msemaji wa hospitali kuu ya Colombo ameliambia shirika la habari la AFP kwamba watu watatu walikuwa wakitibiwa majeraha ya risasi.

    Sri Lanka inakabiliwa na mfumuko mkubwawa bei na inatatizika kuagiza chakula, mafuta na dawa kutoka nje kutokana na mzozo mbaya zaidi wa kiuchumi nchini humo kuwahi kutokea katika kipindi cha miaka 70.