Twitter Nigeria: Kampuni za simu zaagizwa kufungia mtandao wa Twitter

Chanzo cha picha, Reuters
Serikali ya Nigeria imeziagiza kampuni za simu nchini humo kuzuia upatikanaji wa Twitter, taarifa kutoka kwa shirika la linalowakilisha sekta hiyo imesema.
Bado inapatikana kwenye mitandao mingine ya wi-fi.
Hii ni baada ya serikali kutangaza kwamba itafungia huduma za Twitter nchini humo "kwa muda usiojilikana".
Marufuku hiyo imetokana na "kuongezeka kwa matumizi ya mtandaokwa shughuli zinazohujumu kuwepo kwa Nigeria kama taifa lililoundwa kama shirikisho ", ilisema taarifa.
Twitter ilisema tangazo la Ijumaa lililotolewa na Waziri wa Mawasiliano Lai Mohammed ni la "kusikitisha sana".
Kufikia Jumamosi asubuhi, waandishi wa BBC mjini Lagos na Abuja walisema wameshindwa kufikia Twitter kupitia mitandao miwili mikuu ya simu: MTN na Airtel. Mingine pia imeathiriwa.
Twitter kwa sasa inapatikana kupitia mitandao mingine ya wi-fi , lakini njia hiyo ni nadra sana kutumiwa kupata za intaneti nchini Nigeria.
Watu wamekuwa wakitafuta maneno kama "VPN" ambayo yamepata umaarufu ghafla, kulingana na mtandao wa Trendsmap ambao unafuatilia masuala ambayo watu wanatafuta na kujadili mitandaoni.
VPN - ama Virtual Private Network -inawawezesha watu kufikia huduma za intaneti kutoka nchi nyingine, na imekuwa ikitumiwa katika baadhi za nchi zinazokabiliwa na marufuku kama hiyo.
Kuondolewa kwa ujumbe wa Buhari Twitter
Hatua ya serikali inakuja siku kadhaa baaada ya ujumbe wa Rais Muhammadu Buhari kuondolewa Twitter kwa kukiuka kanuni za mtandao huo, ijapokuwa suala hilo halikugusiwa katika taarifa yake.
Bwana Mohammed ambaye aliwahi kukosoa hatua ya mtandao huo mkubwa wa kijamii wa Marekani kuondoa ujumbe wake, na kuutaja kuwa "upendeleo".
Ujumbe uliotumwa na Bwana Buhari Juni mosi,uliaangazia vita vya wenyewe kwa wenyewe mwaka 1967-70 na kuwachukulia hatua "wale wanaofanya vibaya leo" kwa kutumia "lugha ambayo wataielewa".
Msemaji wa Twitter alisema wakati ujumbe huo ulipotumwa "ulikiuka Sheria za Twitter".
Katika taarifa siku ya Ijumaa, kampuni hiyo- ambayo mwezi Aprili ilitangaza makao yake makuu mapya barani Afrika yatakuwa nchi jirani ya Ghana -ailisema "inachunguza na itatoa taarifa wakati itakapopata maelezo zaidi" kuhusu marufuku ya Nigeria.
Serikali haijatoa maelezo jinsi marufuku hiyo itakavyotekelezwa, au jinsi Twitter ilivyohujumu uwepo wa kiushirika wa Nigeria.













