'Itakuwa jambo jema kama Rais Kagame atasaidia upatikanaji wa haki' – Tshisekedi

Chanzo cha picha, DRC Presidency
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) Felix Tshisekedi ametofautina na Rais wa Rwanda Paul Kagame juu ya ripoti ambayo inashutumu wanajeshi wa Rwanda kwa kutekeleza ukatili DRC.
Akizungumza na shirika la habari la AFP Jumatano, Bwana Tshisekedi alisema kuwa taarifa ya "Mapping report" iliyotolewa na wataalamu wa Umoja wa Mataifa (UN) haikutengenezwa na raia wa Congo, hivyo basi, "haina upendeleo."
Bwana Tshisekedi alisema kuwa lazima haki itendeke kwa waathirika wa ukatili huo ulioangaziwa na ripoti hiyo ya UN ya mwaka 2010.
Ripoti hiyo, ambayo inapingwa na Rais Paul Kagame, iliangazia ukiukwaji mkubwa dhidi ya sheria ya kimataifa ya haki za binadamu kati ya mwaka 1993 na 2003. Hata hvyo, Rwanda na nchi zingine zilizotajwa zimekanusha madai katika ripoti hiyo.
Katika mahojiano na shirika la habari la AFP Jumatano, Bwana Tshisekedi alisema haki lazima itendeke kwa waathirika wote waliopoteza maisha yao huko DR Congo na katika eneo hilo.
"Kwa hiyo kwangu, itakuwa ishara nzuri kwa Rais Kagame kutoa ushirikiano katika hilo, kwasababu hadi kufikia hatua hii bado hakuna shutuma zozote …na ikiwa wale anao watetea hawana makosa, haki itawaondolea lawama," Bwana Tshisekedi amezungumza na shirika la AFP.
Bwana Tshisekedi alisema kwamba yeye hamjibu Bwana Kagame, ambaye awali alisema kuwa ripoti hiyo "ni njama ya kisiasa".
Jumatatu, Bwana Kagame alielezea shirika la France24 huko Paris kwamba "hakuna uhalifu ulitendwa [mashariki mwa DR Congo] - sio na waliotajwa au na nchi zilizotajwa".
Marasi hao wawili pia wametofautiana juu ya Denis Mukwege, Daktari wa DR Congo aliyeshinda tuzo ya amani ya Nobel ambaye amejitolea kuhakikisha haki inapatikana kwa waathirika waliotajwa kwenye ripoti.
Bwana Tshisekedi alimuelezea Dr Mukwege kama "Fahari ya taifa lake…kwa kazi yake kwa waathiriwa, huku Rais wa Rwanda akisema alikuwa "chombo cha nguvu isiyoonekana … amearifiwa cha kusema kitakachoshawishi maoni ya watu ".
Tshisekedi alisema nini?
Kuhusu suala la ripoti ya Umoja wa Mataifa ya 'Mapping report', alisema hatamjibu Rais Paul Kagame.
Alichotaka yeye ni haki itendeke kwa waliopoteza maisha Congo.
Tshisekedi alisema lengo lake ni kubadilisha historia mbaya ya Afrika "kwa sababuu ni aibu kuishi na jirani ambaye anahisi haustahili heshima". "Nataka amani kwa watu wangu na jirani zangu..."
Kwa Dkt. Denis Mukwege, Tshisekedi aliongeza kuwa: "Wewe unafanya wengi kuwa na shauku, n ani tu tunaye muamini kwasababu ya kazi anayofanya kwa walokandamizwa."
Tshisekedi ameahidi kuwa yaliyoangaziwa katika ripoti hiyo yatawasilishwa katika mahakama ya Congo, katika mahakama maalum au kwenye mfumo wa kukabiliana na kesi za uhalifu.
"... Cha muhimu ni kumaliza mzunguko huu wa maovu na kusonga mbele kwa maslahi mema ya mataifa haya mawili," alisema.













