Donald Trump na familia yake wachunguzwa kwa kudaiwa kukwepa kodi

Mwanasheria wa Trump amesema madai hayo ni ya uongo

Chanzo cha picha, AFP/Getty Images

Maelezo ya picha, Mwanasheria wa Trump amesema madai hayo ni ya uongo

Maafisa nchini Marekani katika jimbo la New York wamesema wamelazimika kuchunguza madai kwamba Rais Donald Trump alisaidia familia yake kukwepa kodi ya mamilioni ya dola katika miaka ya 1990.

Ripoti iliyochapishwa na gazeti la New York Times imemshutumu Rais Trump kwa kuhusika na mpango wa ulipaji kodi ubabaishaji pamoja na udanganyifu ili kuficha makadirio yanayomhusu yeye pamoja na ndugu na wazazi wake.

Ikulu ya White House imetupilia mbali madai hayo kuwa ni ya upotoshaji.

Msemaji wa White House Sara Sanders ameongeza kusema malipo yote yote yalikuwa yakikaguliwa na kupitishwa na mamlaka za kodi kwa miaka mingi iliyopita.

Rais Trump bado hajasema lolote kuhusu madai hayo lakini mwanasheria wake Charles Harder amekana vikali mteja wake kutenda kosa lolote.

Amesema hakuna udanganyifu au ukwepaji wa kodi uliofanywa na yoyote na kusema taarifa ambazo gazeti la New York limeegemea ni za madai uongo na yasiyo sahihi.

Gazeti hilo la New York Times katika taarifa yake limesema pamoja na kwamba Rais Trump amekuwa akijinadi kuwa ubilionea wake unatokana na jitihada zake binafsi, lakini amekuwa akipokea mamilioni ya dola kutoka rasilimali za wazazi wake tangu akiwa na umri wa miaka mitatu.

Donald Trump na babake Fred Trump Julai 1988 at The Plaza Hotel in New York City

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Babake Donald Trump, Fred Trump (kulia) alijipatia utajiri mkubwa kwa kuwekeza katika viwanja na majumba New York

Limesema katika umri wa miaka mitatu alikuwa na mapato yapatayo dola laki mbili kwa mwaka kutoka kwa rasilimali za wazazi wake na baadae akawa milionea akiwa umri wa miaka minane.

Gazeti hilo limekwenda mbali zaidi na kusema fedha nyingi alizipata kutokana na kuwasaidia wazazi wake kukwepa kodi.

Limesema yeye na ndugu zake waliunda kampuni bandia na kujipatia mamilioni ya dola kama zawadi kutoka kwa wazazi wake.