Buriani King Majuto: Mwili wa mchekeshaji mkongwe wa Tanzania wazikwa Tanga

Mwili wa mchekeshaji mkongwe wa Tanzania wazikwa Tanga

Hatimaye mwili wa muigizaji wa vichekesho Amri Athumani maarufu kama Mzee King Majuto umehifadhiwa nyumbao kwake huko Donge, Tanga nchini Tanzania.

Kabla ya kuhifadhiwa wmili huo ulisafirishwa jana usiku hadi Tanga ambapo ulisimamishwa njiani kuwapa mashabiki fursaya kutoa heshima zao za mwisho.

Dua ya kuaga mwili wa marehemu huyo aliyefariki Jumatano usiku akitibiwa katika hospitali ya taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam ilifanyika katika ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam

Umati wa watu uliohudhuria mazishi ya King Majuto Tanga
Baadhi ya viongozi waliohudhuria maziko ya King majuto mjini Tanga
Viongozi wa dini waliongoza shughuli ya maziko

Miongoni mwa waliohudhuria ni Rais wa Tanzania Dkt John Magufuli.

Leo ibada ya mazishi inatarajiwa kuanza mwendo wa saa sita mchana katika msikiti wa Nuruguda uliopo karibu na nyumbani kwake.

Baadaye mwili wake utazikwa kijiji cha Kiruku yalipo mashamba yake nje kidogo ya jiji la Tanga.

Watu waliohudhuria maziko ya mchekeshaji King majuto mjini Tanga

Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi la Tanzania, mwili ulipowasili nyumbani kwa Mzee Majuto mwendo wa saa moja unusu usiku, kuliibuka vilio huku wanawake wengi wakizimia.

Mwili ulisimamishwa katika vijiji 14 na mashabiki wakitaka kutoa heshima ya mwisho.

Magufuli akitoa heshima za mwisho katika jeneza lenye mwili wa King Majuto

Chanzo cha picha, IKULU, TANZANIA

Maelezo ya picha, Magufuli akitoa heshima za mwisho katika jeneza lenye mwili wa King Majuto

Akiwa kama mfalme wa tasnia ya maigizo ya uchekeshaji nchini Tanzania na Afrika Mashariki, Mzee Majuto aliweza kujizolea umaarufu mkubwa kupitia namna ambavyo alikua akiigiza na kuwa miongoni mwa watu wenye mvuto mkubwa miongoni mwa wasanii.

Afya ya Mzee Majuto ilizorota zaidi mwanzoni mwa mwaka 2018 ambapo awali alipelekwa nchini India kwa matibabu baada ya Rais wa Tanzania John Magufuli na wapenzi wa sanaa ya Mzee Majuto kumchangia ili kunusuru uhai wake kabla ya baadae kurejea nchini Tanzania.

Awali alidaiwa kuugua ugonjwa wa henia na baadaye tezi dume.

Magufuli na Kikwete

Chanzo cha picha, IKULU, TANZANIA

Januari mwaka huu, Mzee majuto alifanyiwa upasuaji wa tezi dume katika hospitali ya Tumaini jijini Dar es Salaam.

Kidonda cha upasuaji wa henia kiliendelea kumtatiza na alilazwa kwa mara nyingine katika hospitali hiyo katikati ya mwezi Aprili.

Mei 4, mwaka huu mwigizaji huyo alisafirishwa kwenda India kupata matibabu katika hospitali ya Apollo, jijini New Delhi.

Juni 23, mwaka huu alirejea nchini Tanzania baada ya kupata matibabu yaliyokuwa yakigharamiwa na Serikali na moja kwa moja alipelekwa Muhimbili kwa ajili ya uangalizi kabla ya kuruhusiwa kuondoka na kisha kurudishwa tena Julai 31 hospitalini hapo.

Historia yake ya uigizaji

Wiki chache zilizopita taarifa za uongo za kifo chake zilisambaa mitandaoni kabla ya familia yake kukanusha mara kwa mara.

Majuto aliyezaliwa mkoani Tanga Kaskazini mwa Tanzania mwaka 1948 alianza kuigiza akiwa na umri wa miaka tisa.

Amecheza kwa mafanikio makubwa kwenye tamthiliya kama vile Mama Nitilie, Kondakta na nyinginezo nyingi zilizompa umaarufu mkubwa.

Kabla ya kifo chake tayari alikwisha wasamehe baadhi ya waandaaji na wasambazaji ambao inasemekana walikua wakimdhulumu mamilioni ya fedha baada ya waziri anayehusika na sanaa nchini Tanzania Harisson Mwakyembe kutishia kuwashitaki watu hao.

Atabaki kuwa nembo ya tasnia ya uigizaji wa vichekesho nchini Tanzania hata baada ya kifo chake.

Risala za rambirambi

Rais Magufuli aliwaongoza Watanzania kutuma risala za rambirambi.

Alisema King Majuto atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa na wa muda mrefu alioutoa kupitia sanaa ya uigizaji na uchekeshaji, ambapo alishiriki kuelimisha jamii, kuendeleza na kukuza sanaa na kuunga mkono juhudi za chama na Serikali katika kuhimiza maendeleo.

Magufuli

"King Majuto alikuwa kielelezo cha safari ndefu ya sanaa kwa nchi yetu, kwa muda wote amedhihirisha kipaji, ujuzi na uwezo wa hali ya juu katika uigizaji na uchekeshaji na hivyo kuwa kipenzi cha Watanzania na wasanii wenzake, hatutasahau ucheshi wake, upendo na uzalendo kwa nchi yake wakati wote wa uhai wake," amesema Rais Magufuli.

Kiongozi huyo wa nchi alimjulia hali msanii King Majuto alipokuwa amelazwa katika hospitali ya Tumaini jijini Dar es salaam 31 Januari, 2018.

Kiongozi wa chama cha upinzani cha ACT Wazalendo, ambaye pia ni mbunge wa Kigoma-Ujiji Zitto Kabwe amesema: "Nimepokea Taarifa ya msiba wa Mzee Majuto kwa masikitiko makubwa sana. Tumshukuru Mola kwa uwezo wake na kuwaombea wafiwa kwa mola awape subra."

Msanii maarufu wa bongo fleva Naseeb Abdul akijulikana zaidi kama Diamond Platnumz, ameandika kuwa Mzee Majuto ni mfalme ambae ataishi mioyoni mwa wengi daima.

Diamond

Chanzo cha picha, Instagram

Msanii Ali Kiba naye ameandika: "Ewe Mwenyezi Mungu hakika Mzee Wetu Amri Bin Athuman (King Majuto) yuko katika dhima yako na kamba ya ujirani wako, basi mkinge na fitina ya kaburi na dhabu ya moto nawe ndiwe mstahiki wa utekelezaji na ukweli msamehe na umrehemu hakika Wewe ni mwingi wa kusamehe, mwingi wa kurehemu. Amin."

Vanessa Mdee ni miongoni mwa walioandika ujumbe wa kumuomboleza kwenye mitandao ya kijamii

Chanzo cha picha, Instagram

Maelezo ya picha, Vanessa Mdee ni miongoni mwa walioandika ujumbe wa kumuomboleza kwenye mitandao ya kijamii