Je wanaume wako tayari kutumia dawa za uzazi wa mpango Kenya ?

Chanzo cha picha, Getty Images
Kenya imechaguliwa kuwa sehemu ya utafiti wa vidonge vya uzazi wa mpango kwa wanaume.
Nchi nyingine zinazoungana na Kenya ni Uingereza, Italia na Chile ambapo wanaume watatakiwa kunywa kidonge kimoja kila mwezi.
Taasisi ya taifa ya maendeleo ya afya ya mtoto ilitengeneza kidonge kwa ajili ya kuwahimiza wanaume kutumia njia za uzazi wa mpango.
Inaelezwa kuwa mwanaume anayetumia kidonge anatarajiwa kupunguza idadi ya mbegu za kiume ndani ya saa 72 na kupunguza uwezekano wa kutungisha mimba.
Jaribio hili linatarajiwa kufanyika kwa miaka minne, wataalamu wakisema kuwa mpango huu unahitaji jitihada za pamoja za jinsia zote ili kufikisha lengo la asilimia 70.
ingawa kumekuwa na msukumo kwa wakenya kukubali kidonge hicho, mpango huo umekosolewa swala la maadili na madhara yake baada ya dawa hizo kuwafikia vijana hali ambayo inadaiwa kuwa vitendo vya ngono vitaongezeka miongoni mwao.

Chanzo cha picha, AFP
Njia za uzazi wa mpango zilianzishwa kwa mara ya kwanza nchini Kenya mwaka 1967,vidonge hivyo vilianza kutumika kwa wingi mwaka 2004 .
Wataalam wa afya wanasema vidonge hivyo ni salama na hazina madhara yeyote kwa mwanaume wakati wa kujamiiana
Utafiti uliochukua mwezi mmoja katika chuo kikuu cha kitabibu cha Washington kiliwahusisha wanaume 83 waliomaliza majaribio mbali na 100 waliochaguliwa.
Wanaume walikuwa na umri wa kati ya miaka 18 na 50.
Je vidonge hivi vina madhara gani?
Watu tisa pekee walioshiriki kwenye utafiti huo walieleza kuwa wamepunguza hamu ya kujamiiana, wanane walipata miwasho kwenye ngozi
Pia kuna walioripoti kuongezeka uzito wanasayansi wakisema hali hiyo si hatarishi.
Kidonge hicho kimeripotiwa kutokuwa na madhara kwenye figo au kuathiri ufanyaji kazi wake, tofauti na iliporipotiwa wakati wa majaribio ya dawa ya uzazi wa mpango ya wanawake ambayo mpaka leo kuna changamoto hizo














