Jiwe kubwa la barafu lavutia watalii Newfoundland

Chanzo cha picha, Reuters
Eneo la Newfoundland, Canada limekuwa kivutio kikubwa cha watalii baada ya kutokea kwa siwa kubwa la barafu ufukweni.
Kituo cha habari cha CBC News cha Canada kinasema kwamba katika wikendi ya Pasaka, barabara kuu ya Southern Shore karibu na mji wa Ferryland ilifungwa baada ya wapiga picha - wataalamu na watu wa kawaida - kufika kwa wingi kupiga picha jiwe hilo la barafu.

Chanzo cha picha, Reuters
Eneo hilo linalopatikana katikati ya Newfoundland na Labrador hufahamika kama "njia kuu ya mawe ya barafu" kutokana na idadi kubwa ya masiwa ya barafu ambayo hupitia eneo hilo kila majira ya kuchipua unapofika kutoka eneo la Arctic.
Mawe hayo mara nyingi huwa yamevunjika na kuwa vipande vya vidogo vya barafu na husalia kwenye bahari hadi mwishoni mwa majira ya kuchipua na mapema majira ya joto.
Lakini dalili zinaonesha jiwe hili kubwa limekwama na huenda lisihame, kwa mujibu wa meya wa eneo hilo Adrian Kavanagh.

Chanzo cha picha, Reuters
Jiwe hilo ni kubwa na limekwama kwenye ufukwe, jambo linalowapa watu fursa nzuri sana ya kupiga picha.
Masiwa ya barafu mara nyingi huwa na sehemu yake kubwa chini ya maji na ni sehemu ndogo tu ya ncha yake ambayo huonekana juu ya maji.
Hii huifanya kuwa rahisi kwa masiwa hayo kukwama yanapokuwa karibu na ufukwe.

Chanzo cha picha, Reuters
Picha za Reuters












