Jurgen Klopp amwambia Mourinho ''sina haja na Man United yako''

Liverpool inacheza dhidi ya man United katika mechi ya kirafiki ya maandalizi ya msimu ujao.

Chanzo cha picha, Getty Images

Mkufunzi wa Liverpool Jurgen Klopp amesema kuwa mojawapo ya malengo yake maishani ni kumfanya Mkufunzi wa Manchester united Jose Mourino kutabasamu, baada ya Mourinho kusema kwamba Liverpool inapaswa kushinda ligi ya Uingereza msimu huu.

Mourinho alisema kuwa klabu hiyo ya Anfield ina nafasi nzuri ya kushinda taji hilo baada ya kutumia £170m kununua wachezaji mwisho wa msimu uliopita.

Lakini Klopp amepinga matamshi hayo kabla mechi ya Jumapili kati ya miamba hiyo ya Uingereza mjini Michigan kuwania taji la kimataifa.

''Ni ulimwengu huru na sina tatizo na Jose Mourinho'', alisema raia huyo wa Ujerumani.

''Tunawajibika kwa mashabiki wetu, wamiliki wa timu zetu na sio mtu mwengine yeyote, Sina haja na Man United''.

Majibu hayo ya Klopp yanafuatia maoni ya Mourinho kwamba Liverpool itakuwa imeweka rekodi mpya ya Uingereza msimu huu baada ya kutumia kitita cha £250m katika kipindi cha miezi 12 iliopita.

Takwimu hizo zinashirikisha rekodi ya dunia ya dau la £66.8m waliolipa kumsajili kipa wa Roma Alisson na £75m walizotumia kumsaini beki wa Southampton Virgil van Dijk mwezi Januari.

Mkufunzi wa Liverpool Jurgen Klopp

Msimu huu kiungo wa kati wa Guinea Naby Keita amewasili kutoka klabu ya RB Leipzig kwa dau la £50m, kiungo wa kati wa Brazil Fabinho amejiunga kutoka Monaco katika mkataba unaodaiwa kuwa na thamani ya £40m, na winga wa Uswizi Xherdan Shaqiri pia amejiunga na klabu hiyo kwa dau la £13m kutoka Stoke.

Hatahivyo Liverpool pia ilijipatia kitita cha £142m baada ya kumuuza Philippe Coutinho Barcelona mwezi Januari.

Alipoulizwa kuhusu matumizi ya Liverpool, Mourinho alisema: Sioni timu nyengine katika ligi ya Uingereza itakayoweza kufikia kiwango kama hicho-timu ambayo ilifika fainali ya kombe la vilabu bingwa , lazima ujue kwamba ni wawaniaji wakubwa .Lazima ushinde.

Alipoulizwa iwapo ni lazima ashinde ligi msimu huu , Klopp alisema: Sidhani. Je nitafutwa iwapo nitashindwa? Itategemea mchezo tutakao kuwa tukicheza.