Idadi ya kesi zilizothibitishwa za Ebola nchini Uganda imeongezeka hadi 31. Kifo kimoja zaidi pia kimerekodiwa, na kufanya jumla ya vifo vilivyothibitishwa kufikia sita.
Moja kwa moja
Mwandishi Tsitsi Dangarembga apatikana na hatia ya 'kuchochea vurugu'
Mwandishi mashuhuri wa Zimbabwe Tsitsi Dangarembga
amepatikana na hatia ya kuchochea ghasia kwa kubeba mabango katika maandamano
ya kuipinga serikali miaka miwili iliyopita.
Amehukumiwa
pamoja na rafiki yake Julie Barnes. Wanawake wote wawili walikuwa wamebeba
mabango ya kutaka mageuzi ya kisiasa katika maandamano hayo mjini Harare,
ambayo mamlaka iliyataja kuwa ni ukiukaji wa masharti ya virusi vya corona na uchochezi wa ghasia za
umma.
Hakimu Alhamisi
alisema picha zao wakiandamana zilisambazwa kwenye mitandao ya kijamii na
zingeweza kuchochea uvunjifu wa amani kwa kuhimiza umma kwa ujumla kushiriki.
Hukumu yao bado
haijatangazwa.
Mashirika ya
kutetea haki za binadamu yanasema kesi hiyo ni sehemu ya msako unaoendelea
dhidi ya wakosoaji wa serikali na wanaharakati.
Mnamo 2020,
kitabu cha Dangarembga This Mournable Body kiliorodheshwa kwa Tuzo la Booker.
Kwa Picha: Kimbunga Ian chasababisha mafuriko na uharibifu Marekani
Picha zaidi zachapishwa kuhusu uharibifu mkubwa uliosababishwa na Kimbunga Ian Marekani
Chanzo cha picha, Getty Images
Maelezo ya picha, Waokoaji wakiwasaidia raia waliojikuta katika mafuriko
Chanzo cha picha, Getty Images
Chanzo cha picha, Getty Images
Chanzo cha picha, Getty Images
Chanzo cha picha, Getty Images
Idadi ya walioambukizwa Ebola Uganda yafikia 31
Chanzo cha picha, EPA
Maelezo ya picha, Ebola DR Congo
Idadi ya kesi zilizothibitishwa za Ebola nchini Uganda
imeongezeka hadi 31. Kifo kimoja zaidi pia kimerekodiwa, na kufanya jumla ya
vifo vilivyothibitishwa kufikia sita.
Mmoja wa wafanyikazi sita wa afya ambao waliambukizwa virusi
hivi sasa yuko katika hali mbaya, kulingana na habari kutoka kwa wizara ya afya
ya nchi.
Rais wa Uganda amekaidi wito wa wafanyikazi wa afya kuweka
eneo la kati lililoathiriwa na Ebola chini ya karantini ili kuzuia virusi
kuenea kwa nchi nzima.
Akizungumza katika runinga ya kitaifa Jumatano, amesema
hakuna hatua kama hizo zinahitajika kwa sababu Ebola haipatikani kwa njia ya
hewa, na akasema maabara itaundwa katika kitovu cha virusi ili kuharakisha
upimaji wa wagonjwa.
Wakati huo huo, Shirika la Afya Ulimwenguni linaamini kwamba
mlipuko wa Ebola nchini Uganda huenda uligunduliwa kuchelewa, ikizingatiwa
kwamba mtu wa kwanza kuugua alionyesha dalili mnamo Agosti lakini mlipuko huo
haukutangazwa hadi mwishoni mwa Septemba.
Wataalamu wa afya duniani wanasema ni jambo lisilowezekana
kufikiri Ebola itatokomezwa, lakini sasa ni rahisi kuzuia maambukizi.
Malkia Elizabeth II: Sababu ya kifo cha Malkia yatolewa
Chanzo cha picha, Getty Images
Maelezo ya picha, Malkia Elizabeth
Malkia Elizabeth
II alikufa kutokana na uzee, kulingana na dondoo kutoka kwa cheti chake cha
kifo.
Inasema alikufa
saa 15:10 BST katika Jumba la Balmoral huko Scotland mnamo 8 Septemba – akiwa na
umri wa miaka 96.
Rekodi za Kitaifa
za Scotland zilichapisha cheti hicho siku ya Alhamisi.
Hati hiyo
ilisainiwa na binti yake, Bintimfalme Anne.
Kifo hicho kilirekodiwa tarehe 16 Septemba na Msajili Mkuu
wa Scotland.
Cheti chake cha kifo pia kina jina la baba yake, Mfalme George
VI, na mama, Elizabeth Bowes-Lyon.
BBC News ilithibitisha kifo hicho saa 18:31 BST mnamo tarehe
8 Septemba kufuatia taarifa kutoka kwa Familia ya Kifalme.
Taarifa hiyo ilisomeka: "Malkia alikufa kwa amani huko
Balmoral mchana huu."
Chanzo cha picha, National Record Scotland
Maelezo ya picha, Cheti cha kifo cha malkia Elizabeth II
Manowari za Kirusi zadaiwa kuonekana eneo ambapo bomba la gesi la Nord Stream linavuja
Maafisa wa ujasusi wa nchi za Magharibi wanadai kuwa meli za kivita za Urusi na nyambizi zilionekana katika eneo ambalo bomba la gesi la Nord Stream liliharibiwa Jumatatu na Jumanne iliyopita, kulingana na chombo cha habari cha CNN.
Wataalamu wana hakika kwamba bomba la gesi lililokatwa liliathiriwa na mfululizo wa milipuko ya chini ya maji, ambayo ilisababisha kuvuja kwa gesi. Ilifanyika Jumatatu kwenye sehemu tatu za bomba kwenye pwani ya Denmark na Uswidi, na Jumatano jioni Walinzi wa Pwani wa Uswidi walifanikiwa kugundua sehemu ya nne iliokuwa ikivuja.
Vyanzo vya habari vilivyoripoti uwepo wa nyambizi za Urusi katika eneo lililoharibiwa vinasisitiza kuwa hii haithibitishi kuhusika kwa Urusi katika hujuma hiyo. Walakini, wamesema kwamba ugunduzi huo utazingatiwa na timu ya wachunguzi.
Mmoja wa wawakilishi wa kijeshi wa Denmark pia alisema kuwa meli za Kirusi husafiri mara kwa mara kupitia Eneo lililoathirika na ushiriki wao katika uharibifu hauonekani kuwa wa wazi.
Maelezo ya picha, Bomba la gesi la Nord Stream
Habari za hivi punde, Urusi kunyakua rasmi maeneo manne zaidi ya Ukraine
Chanzo cha picha, Getty Images
Rais wa Urusi Vladimir Putin atafanya hafla ya utiaji saini siku ya Ijumaa na kunyakua rasmi maeneo manne zaidi ya Ukraine baada ya kura za maoni zilizolaaniwa na Ukraine na Magharibi kuwa ni za udanganyifu.
Maafisa wanaoungwa mkono na Urusi hapo awali walidai kuwa zoezi hilo la siku tano lilipata karibu kuungwa mkono na watu wengi. Kura zinazojulikana zilifanyika Luhansk na Donetsk upande wa mashariki, na huko Zaporizhzhia na Kherson kusini.
Rais wa Urusi atatoa hotuba kuu huko Kremlin. Jukwaa tayari limeandaliwa katika uwanja wa Red Square Moscow, huku mabango yakitangaza maeneo hayo manne kama sehemu ya Urusi na tamasha lililopangwa kufanyika jioni hiyo.
Tukio hilo linaangazia hatua ya Urusi kutwaa Crimea mwaka wa 2014, ambayo pia ilifuatia kura ya maoni iliyokataliwa na kutangazwa na hotuba ya ushindi wa urais kutoka jukwaani.
Unyakuzi huo wa awali haujawahi kutambuliwa na walio wengi wa jumuiya ya kimataifa. Hakuna uthibitisho kwamba Bw Putin anapanga anwani sawa ya nje.
"Kesho saa 15:00 (12:00GMT) katika Ukumbi wa St George wa Jumba la Grand Kremlin hafla ya kutia saini itafanyika ili kujumuisha maeneo mapya nchini Urusi," alisema msemaji Dmitry Peskov.
Viongozi wawili wanaotaka kujitenga wanaoungwa mkono na Urusi kutoka mashariki pia wanatarajiwa kushiriki. Rais wa Urusi anatarajiwa kutoa hotuba tofauti kwa baraza la juu la bunge tarehe 4 Oktoba, siku tatu kabla ya kutimiza miaka 70.
Bunge pia litakuwa na jukumu la kuidhinisha unyakuzi wa Urusi, ambao umekataliwa na wengi wa jumuiya ya kimataifa. Hakuna ufuatiliaji huru wa mchakato ulifanyika na kulikuwa na akaunti za maafisa wa uchaguzi wakienda nyumba kwa nyumba wakisindikizwa na askari wenye silaha.
Marekani imesema itaiwekea Urusi vikwazo kwa sababu ya kura za maoni zilizoandaliwa, huku nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya zikizingatia hatua ya nane, ikiwa ni pamoja na vikwazo kwa yeyote atakayehusika katika kura hizo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Annalena Baerbock alisema siku ya Alhamisi kwamba watu katika mikoa inayokaliwa kwa mabavu ya Ukraine wamechukuliwa kutoka katika makazi yao na sehemu zao za kazi kwa vitisho na wakati mwingine kwa mtutu wa bunduki. "
Hii ni kinyume cha uchaguzi huru na wa haki. Na hii ni kinyume cha amani, ni amani iliyoamriwa," alisema.
Zoezi hilo lilianza katika 15% ya eneo la Ukraine Ijumaa iliyopita kwa notisi ya siku chache tu.
Vyombo vya habari vya serikali ya Urusi vilisema kuwa matumizi ya walinzi wenye silaha yalikuwa kwa madhumuni ya usalama, lakini ilikuwa wazi kuwa ilikuwa na athari ya kuwatisha wakaazi. "Lazima ujibu kwa maneno na askari aweke alama kwenye karatasi na kulihifadhi," mwanamke mmoja huko Enerhodar aliambia BBC.
Watu kumi na tisa wafariki Morocco baada ya kunywa pombe ya sumu
Chanzo cha picha, Getty Images
Maelezo ya picha, Sheria ya Morocco unazuia mauzo ya pombe kwa Waislamu
Takriban watu 19
wamefariki baada ya kunywa pombe kwenye duka la kando ya barabara katika mji wa
kaskazini wa Morocco Ksar el-Kebir.
Makumi ya watu
wengine walipelekwa hospitalini wakiwa katika hali mahututi, huku wawili
wakilazwa katika chumba cha wagonjwa wa dharura, vyombo vya habari
vimeripotiwa.
Mwanaume mmoja mwenye umri wa miaka 48 amekamatwa
kuhusiana na tukio hilo. Polisi wanasema wamekamata lita 50 za pombe kwenye duka hilo.
Kuuza pombe kwa
Waislamu imekatazwa nchini Morocco, lakini mara nyingi huuzwa kwa siri katika
migahawa.
Mwezi Agosti, watu
wanane walifariki baada ya kunywa pombe yenye sumu katika jimbo la kaskazini la
Oriental, na takriban watu 20 walifariki
Julai mwaka jana katika katika tukio sawa
na hilo katika mji wa Oujda mashariki mwa Morocco.
Wanafunzi wafanya maandamano ya kupinga Muungano wa Ulaya juu ya mzozo wa mafuta wa Uganda
Chanzo cha picha, Patience Atuhaire / BBC
Mamia
ya wanafunzi wa Uganda wanaandamana dhidi ya bunge la Ulaya, baada ya kupinga mradi
wa mafuta baina ya nchi hiyo nan chi Jirani ya Tanzania.
Wabunge wa EU mapema mwezi
huu walipitisha azimio wakionya kuhusu ukiukaji wa haki za binadamu na hatari
za kijamii na mazingira zinazoweza kusababishwa na mradi huo.
Wanafunzi hao wanaandamana
mjini Kampala kufikisha hoja yao kwa ubalozi wa EU.
Maandamano hayo
yanaonekana kuidhinishwa na taifa na wanafunzi wanatembea huku wakisindikizwa
na polisi.
Wakati
ujenzi wa bomba hilo la mafuta lenye urefu wa km 1,443 (maili 896) kutoka Ziwa
Albert magharibi mwa Uganda hadi kwenye bandari ya Tanga nchini Tanzania kwenye bahari ya Hindi.
Chanzo cha picha, Patience Atuhaire / BBC
Habari za hivi punde, Félicien Kabuga ashindwa kuhudhuria ufunguzi wa kesi
Chanzo cha picha, UN-IRMCT
Mmoja wa
washukiwa wakuu wa mauaji ya kimbari ya 1994 nchini amekataa kuhudhuria kesi
yake katika mahakama ya kimataifa ya jinai ICC mjiniThe Hague, lakini majaji wameamua kwamba kesi yake itandelea.
Félicien Kabuga
anashitakiwa kwa mauaji ya na uhalifu dhidi ya binadamu ambapo watu zaidi ya 800,000
– wengi wao wakiwa ni watu wa jamii ya Watutsi.
Kabuga ambaye alikuwa wakati mmoja mtu tajiri zaidi nchini
Rwanda, anashitakiwa kwa kuchochea mauaji kupitia kituo cha redio
alichokimiliki cha RTLM , kufadhili na kuwapatia silaha wanamgambo wa
Interahamwe waliotekeleza mauaji hayo.
Bw
Kabuga mwenye umri wa miaka 80 na ushee, amekana mashitaka
Mchungaji mzungu aliyepanga mauaji ya kimbari ya weusi afungwa maisha
Chanzo cha picha, National Prosecuting Authority
Maelezo ya picha, Harry Knoesen alisema Mungu God wanted him to do it
Mchungaji
aliyeamini kuwa wazungu ni watu bora zaidi kuliko watu wengine ambaye alipanga njama ya
mauaji ya kimbari dhidi ya raia Weusi wa
Afrika Kusini na mapinduzi nchini humo amefungwa jela maisha.
Harry Knoesen, mwenye umri
wa miaka 64, alikuwa kiongozi wa kikundi cha mrengo wa kulia na aliongoza
mipango ya kuipindua serikali tarehe 28 Novembakwa kutumia silaha aina ya AK-47, gurunedi za kurushwa kwa mkono na kufyatua
maroketi.
Knoesen alitaka hata
kutumia silaha za kibaiolojia kuwamaliza kabisa watu Weusi, mahakama ya juu
zaidi ya Mpumalanga iliambiwa.
"Alitaka kuhalalisha Imani
zake kwa misingi ya dini, akidai kwamba Mungu alimteua ili arejeshe tena Afrika
Kusini kwa watu weupe," alisema msemaji wa mamlaka ya ue mashitaka ya
taifa Monica Nyuswa.
Kwa ujumla, Knoesen amepewa
hukumu mbili za maisha pamoja na miaka 21 jela kwa makosa ya 21 ya uhalifu.
Urusi na Ukraine: Mkutano wa kuunga mkono kutwaliwa kwa majimbo ya Ukraine waandaliwa mjini Moscow
Chanzo cha picha, Reuters
Shirika
la habari la Reuters limechapishapicha ya jukwaa lililojengwa katika medani ya Red
Square mjini Moscow kwa ajili ya mkutano wa kuunga mkono kutwaliwa kwa majimbo
yaliyovamiwa na Urusi nchini Ukraine. Kulingana na vyombo vya habari vya Urusi,
mkutano huo utafanyika tarehe 30 Septemba.
Kulingana na picha hizo,
tukio hilo litafanyika chini ya kauli mbiu kama inayosema "Donetsk, Lugansk, Zaporozhye, Kherson.
Russia" na "Donetsk, Lugansk,
Zaporozhye, Kherson. Pamoja daima."
Chanzo cha picha, Reuters
Maandalizi
ya"tamasha la -mkutano " yameripotiwa
na vyanzo vya shirika la habari la Urusi TASS. Taarifa kuwa tarehe 30 Septemba
eneo hilo linalofahamika kama Red Square litakuwa limefungwa pia imethibitishwa
na ofisi ya meya wa mji wa Moscow.
Mapema Jumatatu, BBC
iliripoti ikinukuu vyanzo vyake kwamba Rais Vladmir huenda akazungumza katika
mkutano huu.
Kulingana na taarifa ya gazeti, siku hiyo,
kiongozi huyo wa Urusi huenda akakutana na viongozi waliojitangazia ‘’tawala’ ’kwenye
majimbo ya Ukraine yaliyovamiwa na Urusi. Jumatano,
picha zao zilionekana huku wakiwa karibu na ndege mjini Moscow.
Kulingana na vyanzo vya habari vya Urusi, bunge la taifa la Urusi huenda
likapiga kura kwa ajili ya kujitenga kwa maeneo yaliyovamiwa tarehe 3 Oktoba, na
Baraza la shirikisho litaidhinisha uamuazi huo siku moja baadaye.
Mamlaka za Urusi ziliendesha ‘’kura ya maoni’’ juu ya maeno ya Ukraine
yaliyo chini yake juu ya kujiunga na Urusi. Ukraine na washirika wake wa Magharibiwamesema kuwa utaratibu huo ambao,
uliandaliwa katika hali za kivita na uvamizi wa Urusi hauwezi kuwa halali kisheria.
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky aliitaja "kura ya maoni" maigizo,
ambayo matokeo yake yalikuwa yanajulikana na waandaaji mapema.
Chanzo cha picha, Reuters
Gereza la ajabu ambamo watu wanafungwa pingu kwa hiari
Chanzo cha picha, Getty Images
Gereza moja katika jimbo laUttarakhand nchini
India limeanza kuwaadhibu wafungwa kwa namna ya kipekee kama njia mojawapo ya
kuzuia baadhi ya matatizo ya kijamii.
Utawala wa gereza
hilo, lililopo katika mji wa Haldwani, umeanza mpango wa kuwaruhusu watu wa
kawaida kufungwa ndani yake, bila kuhukumiwa na mahakama. Wanaofungwa katika gereza hilo hufungwa pingu wakati wote.
Yeyote anayeomba kufungwa
ndani yake hutozwa garama ya rupia 500 kwa usiku mmoja, pesa ambazo nis awa na
dola nane na nusu.
Afisa mkuu wa gereza
hilo amesema kuwa ameanzisha mpangi huu wa ajabu ili kuwanusu watu kupitia
adhabu kalikwa baadhi ya uhalifu.
Watu wengi wanaoishi nchini
India huenda katika gereza hilo ili kuzuia makosa ambayo wameambiwa na watabiri
kuwa wanaweza kutokea siku zijazo, baada ya kuomba ushauri kutoka kwao.
Chanzo cha picha, Getty Images
Maelezo ya picha, Gereza la Haldwaniliko karibu na mlima wa Nainital,lilijengwa mwaka 1903.
Watabiri , ambao maarufu katika utamaduni nchini India, huwaambia baadhi ya watu kuwa watafungwa gerezani kwa muda fulani katika siku za usoni, kwahivyo ni vyema wajitolee kufungwa gerezani kwa kipindi fulani.
Mpango huu wa kuwafunga watu kwa hiari yao ulianza katika gereza maalumu ambalo lilitengenezwa ili kila mtu awe huru kuingia gerezani kwa hiari kwa muda anaotaka, na anayefungwa hulipa gharama ya siku alizofungwa pale.
Gereza hilo lina vyumba sita kwa ajili ya wahudumu wa gereza, lakini vyumba hivyo sasa vimeandaliwa kwa ajili ya watu wanaotaka kufungwa kwa hiari , ambao wanaamini kwa kufanya hivyo uhalifu wao ambao wangeufanya siku zijazo utaondolewa.
Habari za hivi punde, Félicien Kabuga alikuwa na jukumu 'kubwa' katika mauaji ya kimbari ya Rwanda - Mwendesha mashitaka ICC
Chanzo cha picha, AFP
Maelezo ya picha, Félicien Kabuga alikamatwa mjini Paris Ufaransa miaka miwili iliyopita baada ya kuepuka kukamatwa kwa muda mrefu t
Mwendesha mashitaka katika kesi ya mmoja wa washukiwa wakuu wa mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka
1994 inayoendelea katika mahakama ya kimataifa ya jinai ICC amesema kuwa Félicien Kabuga alikuwa na jukumu 'kubwa' katika mauaji ya kimbari ya Rwa nda
Bwana Félicien
Kabuga anashitakiwa kwa mauaji ya halaiki na uhalifu mwingine dhidi ya binadamu
kwa nafasi yake katika mauaji ya watu wapatao 800,000 - wengi wao wakiwa ni wa jamii ya Watutsi.
Kabuga ambaye alikuwa
wakati mmoja mtu tajiri zaidi nchini Rwanda, anashitakiwa kwa kuchochea mauaji
kupitia kituo cha redio alichokimiliki cha RTLM , kufadhili na kuwapatia silaha
wanamgambo wa Interahamwe waliotekeleza mauaji hayo.
Bw Kabuga mwenye umri wa miaka 80 na ushee, amekana mashitaka.
Alikamatwa mjini Paris Ufaransa miaka miwili iliyopita baada ya kuepuka
kukamatwa kwa muda mrefu.
Kwa umri wake, mawakili wake walidai afya yake ni mbaya kuweza kuhudhuria
kesi lakini majaji wameamua kuendelea na kesi yake lakini kwa vipindi vifupi
vifupi vya kesi.
Waendesha mashitaka wanatarajiwa kuwaita zaidi ya mashahidi 50 katika kesi
hiyo inayoweza kudumu kwa miaka.
Manusura wa mauaji ya kimbari nchini Rwanda wametoa wito haki ya kisheria itendeke haraka, wakihofia kuwa anaweza
kufariki huku ikidhaniwa kuwa hana hatia.
Unaweza pia kusoma:
Félicien Kabuga: Mshukiwa mkuu wa mauaji ya kimbari Rwanda akamatwa
Félicien Kabuga: 'Huo wote ni uongo, sikumuua Mtutsi yeyote'
Nyumba milioni 2 zaachwa bila umeme kwa Kimbunga Ian, Florida
Chanzo cha picha, Reuters
Maelezo ya picha, Picha ya jiji la Fort Myers lililofurika Jumatano hii
Kimbunga Ian
kiliwasili magharibi mwa Florida Jumatano kama kimbunga cha 4 chenye upepo wa
zaidi ya kilomita 240 kwa saa, na kusababisha mafuriko mabaya katika maeneo
kadhaa.
Kimbunga Ian
kilitua karibu na Cayo Costa, kusini-magharibi mwa peninsula, kama kimbunga ‘’hatari
sana’’ saa 3:05 usiku kwa saa za huko (7:05 pm GMT), kulingana na Kituo cha
Kitaifa cha Vimbunga cha Marekani
Kimbunga
hicho kilisababisha dhoruba iliyopanda mita kadhaa kwenda juu ambacho kilifurika
maeneo makubwa ya pwani ya kusini magharibi mwa Florida.
Chanzo cha picha, Getty Images
Zaidi ya nyumba milioni 2 hazikuwa na umeme katika jimbo lote, kati ya jumla ya milioni 11, huku maafa zaidi yakitarajiwa wakati dhoruba ikiendelea.
‘’Ni mojawapo ya vimbunga vitano vibaya zaidi kukumba eneo la Florida,’’ Gavana wa Florida Ron DeSantis alisema katika mkutano wa wanahabari Jumatano alasiri.
Anthony Reynes, mtaalam wa hali ya hewa katika NHC huko Miami, aliambia BBC kwamba dhoruba hiyo huenda ikawa ya kihistoria.
‘’Ni dhoruba kubwa na itachukua muda kudhoofika kadiri inavyoendelea kusonga.
Coolio: Rapa wa wimbo wa Gangsta's Paradise afariki akiwa na umri wa miaka 59
Chanzo cha picha, Getty Images
Rapa wa Marekani Coolio, anayefahamika kwa wimbo wa Gangsta's Paradise, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 59.
Meneja wake wa muda mrefu Jarez Posey aliviambia vyombo vya habari vya Marekani kuwa msanii huyo alipatikana akiwa hajitambui kwenye sakafu ya bafuni katika nyumba ya rafiki yake huko Los Angeles.
Coolio alianza kufanya muziki miaka ya 1980, lakini aliimarisha nafasi yake katika historia ya hip hop alipotoa wimbo wa Gangsta's Paradise mnamo 1995.
Sababu kamili ya kifo chake siku ya Jumatano bado haijawekwa wazi. Hata hivyo Posey aliiambia TMZ, ambayo iliripoti habari hiyo kwa mara ya kwanza, kwamba wahudumu wa afya waliamini kuwa huenda alipatwa na mshtuko wa moyo.
Coolio, ambaye jina lake halisi lilikuwa Artis Leon Ivey Jr, alishinda Grammy kupitia wimbo wake wa Gangsta's Paradise, ambao ilitumika katika filamu ya Dangerous Minds iliyochezwa na Michelle Pfeiffer.
Wimbo huo mbaya unaendelea kusikilizwa na watu wengi na umesikiliwa na zaidi ya watu bilioni moja kwenye Spotify, kwa mujibu wa tovuti hiyo.
Zaidi ya kazi yake iliyochukua miongo minne alirekodi Albamu nane na kushinda Tuzo ya Muziki za American Music Award na Tuzo tatu za Muziki za Video za MTV.
Vibao vyake vingine ni pamoja na Fantastic Voyage, Rollin' With My Homies, 1, 2, 3, 4 (Sumpin' New), na Too Hot.
Mbwa wanaweza kutambua hali ya msongo wa mawazo kupitia pumzi ya binadamu
Chanzo cha picha, QUEEN'S UNIVERSITY, BELFAST
Mbwa wanaofugwa majumbani wamethibitisha kwa mara nyingine jinsi wanavyoweka hisia zetu vizuri, hii limebainishwa katika jaribio la kisayansi la kunusa.
Wanasayansi waligundua kwamba mbwa wanaweza kunusa msongo wa mawazo katika pumzi zetu na jasho.
Mbwa wanne waliotolea na wamiliki wao walifundishwa "kuchagua" moja ya makopo matatu ya harufu.
Na katika zaidi ya majaribio 650 kati ya 700, walifanikiwa kutambua sampuli ya jasho au pumzi ambayo ilikuwa imechukuliwa kutoka kwa mtu mwenye mawazo.
Watafiti, katika Chuo Kikuu cha Queen's University Belfast, wanatumai utafiti wao, uliochapishwa katika jarida la Plos One, utasaidia katika kutoa mafunzo ya mbwa wa tiba. Mbwa huishi duniani kupitia harufu.
Na uwezo wao nyeti sana wa kugundua harufu tayari unatumika kugundua dawa, vilipuzi na magonjwa, pamoja na saratani fulani, kisukari na hata Covid.
"Tulikuwa na ushahidi mwingi kwamba mbwa wanaweza kutambua harufu kutoka kwa wanadamu ambayo inahusishwa na hali fulani za matibabu au ugonjwa - lakini hatuna ushahidi mwingi kwamba wanaweza kunusa tofauti katika hali zetu za kisaikolojia," mtafiti mkuu Clara Wilson alisema.
Watu 36 wa kujitolea waliripoti viwango vyao vya msongo kabla na baada ya kumaliza tatizo gumu la hisabati.
Kila moja anaweza kuwa na sampuli ya jasho lao au pumzi kutoka kabla au - kama shinikizo la damu na mapigo ya moyo pia yameongezeka baada ya hapo.
Ebola Uganda: Museveni aondoa uwezekano wa kuweka karantini
Chanzo cha picha, AFP
Rais wa Uganda Yoweri Museveni amesema hakuna haja ya kuweka vikwazo katika maeneo hatarishi ya Ebola katika eneo la kati kwa sababu ugonjwa huo unaosababishwa na virusi hautokei hewani.
Ebola huenezwa kwa njia ya kugusana na mtu aliyeambukizwa au sehemu zilizoambukizwa na kinyesi cha binadamu.
Chama cha wafanyikazi wa matibabu nchini humu awali kilitoa wito kwa eneo lililoathiriwa kuwekwa karantini ili kukomesha kuenea zaidi kwa homa ya kuvuja damu.
Bw Museveni alisema serikali yake ina uwezo wa kudhibiti janga hilo kutokana na uzoefu wa awali wa milipuko kama hiyo.
Hii ni mara ya nne kwa Ebola kuzuka nchini Uganda. Alisema wataalam wa afya ambao hapo awali walishughulikia milipuko ya Ebola wametumwa katika eneo lililoathiriwa.
Kwa sasa inachukua saa 24 kwa sampuli kufanyiwa uchunguzi na matokeo ya maabara kutolewa.
Rais alisema serikali itafungua maabara katika makao makuu ya wilaya ya Mubende, kitovu cha mlipuko huo, ili kuharakisha usindikaji wa sampuli.
Wahudumu sita wa afya waliomtibu mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 24 ambaye baadaye alitambuliwa kuwa kisa cha kwanza, wamepimwa na kukutwa na Ebola.
Jumla ya watu 24 wamethibitishwa kuambukizwa na virusi hivyo nchini humo, watano kati yao wamefariki tangu kuzuka kwa ugonjwa huo wiki iliyopita.
Karibu katika matangazo ya moja kwa moja leo Alhamisi 29.09.2022