Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Makumi wakamatwa baada ya Bobi Wine kuteuliwa rasmi kugombea Urais Uganda

Karibu watu 50 wamekamatwa nchini Uganda kufuatia sarakasi zilizoshuhudiwa katika mji mkuu wa Kampala baada ya mwanasiasa wa Bobi Wine kuidhinishwa kugombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwezi Januari mwaka 2021.

Moja kwa moja

Asha Juma

  1. Polisi ya Uganda yawakamata makumi ya watu katika uteuzi wa urais

    Karibu watu 50 wamekamatwa nchini Uganda kufuatia sarakasi zilizoshuhudiwa katika mji mkuu wa Kampala baada ya mwanasiasa wa Bobi Wine kuidhinishwa kugombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwezi Januari mwaka 2021.

    Baada ya makabiliano ya saa kadhaa, Bobi Wine,ambaye jina lake halisi ni Robert Kyagulanyi, alilazimishwa kuingia katika gari la polisi punde baada ya uteuzi wake wa urais kuidhinishwa na kupelekwa nyumbani kwake.

    Lakini alipofika nyumbani alikataa kushuka kutoka kwa gari la polisi, akisistiza kuwa anataka kwenda katika makao makuu ya chama kuzidua ilani yake .

    Akizungumza na wafuasi wake nyumbani kwake ,Bw. Kyagulanyi alisema polisi waliwapulizia maji ya pili pili machoni yyeye na viongozi wenzake.

    Maafisha watatu wa polisi walijeruhiwa katika pata shika hiyo.

    Kuanzia mapema asubuhi ya Jumanne, polisi waliojihami walipelekwa katika barabra ambazo Bw. Kyagulanyi alitarajiwa kupitia kuelekea kituo cha uteuzi.

    Wagombea uraisi wanatakiwa kuandamana wajumbe wachache, kama sehemu ya kudhibiti kuenea kwa virusi vya corona.

    Lakini baadhi yao walifanya maandamano yaliyovutia mikusanyiko ya watu.

    Wafuasi wa Bw. Kyagulanyi walitawanywa kwa kutumia vitoa machozi.

    Wagombea 11 wanawania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu wa Uganda miongoni mwao Yoweri Museveni na majenerali wake wawili wa zamani waliokuwa naye vitani kabla ya aingie madarakani.

    Tume ya uchaguzi ya Uganda imepiga marufuku mikutano ya kampeni,na wagombea wanatakiwa kufanya kampeni zao kupitia vyombo vya habaro au mitandao ya kijamii.

  2. Raia wauawa na watu waliokuwa na silaha Ethiopia

    Wanaume waliokuwa na silaha wameua watu karibu 32 na kuchoma moto nyumba katika shambulio baya huko magharibi mwa Ethiopia, maafisa wamesema.

    Mamlaka ya eneo imesema kuwa waasi wa Jeshi la Oromo Liberation Army linafaa kulaumiwa kwa shambulizi hilo lililotokea jimbo la Oromia.

    Wakazi wamesema kuwa makumi ya watu walikusanywa na kuuliwa huku mifugo yao ikiibwa.

    Waziri Mkuu Abiy Ahmed amesema huenda shambulizi hilo limehusika na suala la ukabila. Ghasia za kikabila zimekuwa zikiongezeka tangu alipoingia madarakani Aprili 2018.

    Afisa wa eneo aliiambia timu ya BBC kwamba kuna timu iliyotumwa Guliso – eneo la tukio – kufanya uchunguzi huku ikikisiwa kwamba idadi ya waliokufa huenda ikaongezeka.

    Tume ya Haki za Binadamu Ethiopia imesema watu wa kabila la Amharic, kundi ambalo ni la pili kwa ukubwa limelengwa kwenye shambulio hilo lililofanyika Jumapili.

    Aidha, mwenyekiti wa tume ya Umoja wa Afrika, Moussa Faki Mahamat, ameshtumu mauaji hayo.

    Katika taarifa yake, Bwana Faki Mahamat, amewasihi "kujizuia kufanya fujo" na kutoa wito wa majadiliano.

  3. Zitto adaiwa kukamatwa na polisi

    Kiongozi wa ACT- Wazalendo Zitto Kabwe anadaiwa kuzuiliwa na polisi katika kituo cha polisi cha Kati.

    Chama chake kimethibitisha kuwa Bwana Zitto alikamatwa alipokuwa amekwenda kumjulia hali mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe.

    Awali, Polisi jijini Dar es Salaam iliwataka wanasiasa wa upinzani Zitto Kabwe na Halima Mdee kujisalimisha polisi.

    Taarifa kutoka kwa Kamanda wa polisi kanda maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa ilibainisha kuwa jeshi hilo linaendelea kuwasaka wanasiasa wa upinzani kwa tuhuma za kuhamasisha maandamano.

  4. 'Bobi Wine abebwa na polisi punde baada ya kuteuliwa kugombea Urais'

    Mgombea urais Robert Kyagulanyi, maarufu kama Bobi Wine, alibebwa na polisi baada ya kuthibitishwa kuwa mgombea na tume ya uchaguzi, kulingana na mwandishi wa habari wa BBC Patience Atuhaire.

    Bobi Wine alichukuliwa juu juu na polisi punde tu baada ya kumalizika kwa shughuli ya uteuzi wake na kupelekwa moja kwa moja hadi nyumbani kwake,' Atuhaire amesema.

    Wafuasi wa mwanasiasa huyo walikuwa wamekusanyika nje ya kituo cha uteuzi pamoja huku wengine wakiwa wanamsubiri barabarani.

    Awali, polisi walikuwa wametangaza masharti makali juu ya idadi ya wafuasi wanaoruhusiwa kuandamana na mgombea urais hadi tume ya uchaguzi kuwasilisha stakabadhi zake.

    Wafuasi wake waliokuwa wamekusanyika katika makao makuu ya chama chake cha National Unity Platform kwa ajili ya kuzinduliwa kwa manifesti yao walitawanywa kwa vitoza machozi.

    Bobi Wine anakabiliana na wagombea wengine tisa kwenye kinyang’anyiro hicho akiwemo rais aliye madarakani Yoweri Museveni katika uchaguzi wa mwaka ujao.

  5. Zitto Kabwe, Halima Mdee watakiwa kujisalimisha kwa polisi

    Polisi jijini Dar es Salaam imewataka wanasiasa wa upinzani Zitto Kabwe na Halima Mdee kujisalimisha polisi.

    Taarifa kutoka kwa Kamanda wa polisi kanda ya maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa inabainisha kuwa jeshi hilo linaendelea kuwasaka wanasiasa wa upinzani kwa tuhuma za kuhamasisha maandamano.

    Mambosasa amesema kuwa jeshi la polisi linawashikilia watu kadhaa wakiwemo viongozi wa chama cha Chadema ambao ni Freeman Mbowe, Godbless Lema na Boniface Jacob.

    Awali, Gazeti la Habari Leo nchini humo liliandika kuwa, Mahakama imesema viongozi wa upinzani waliokamatwa wanakabiliwa na mashtaka matatu.

    Shitaka la kwanza likiwa ni kuongoza genge la wahalifu, shitaka la pili ni kula njama na la tatu ni kufanya mikusanyiko bila kibali.

  6. Wanakijiji wakatwa vichwa na wanamgambo wa Kiislamu Msumbiji

    Taarifa kutoka Msumbiji zinasema kuwa wanamgambo wa Kiislamu wamevamia vijiji kaskazini mwa eneo la Muidumbe mkoa wa Cabo Delgado Jumamosi na Jumapili.

    Vyombo vya habari vya eneo vimesema kuwa wanakijiji walikatwa vichwa na mali zao kuharibiwa.

    Akizungumza na BBC, msemaji polisi wa eneo alikanusha madai kuwa kuna wanavijiji ambao bado wanashikiliwa na wanamgambo wa jihadi.

    Kundi hilo la wanamgambo ambao wenyeji wanalifamau kama al-Shabab, limekuwa likidhibiti maeneo ya msingi ya kaskazini mwa Mocímboa da Praia tangu mwezi Agosti.

    Pia zaidi ya watu 1,500 wameuawa huku theluthi moja ya watu wakilazimika kuhama makazi yao katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

  7. Robert Kyagulanyi ameteuliwa rasmi kugombea Urais Uganda

    Robert Kyagulanyi ameteuliwa rasmi kugombea Urais nchini Uganda.

    Sasa ni rasmi kuwa Bobi Wine atakabiliana na Rais Yoweri Museveni katika uchaguzi mkuu mwaka ujao mwaka 2021.

    Baada ya stakabadhi zake kukaguliwa, mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi, Justice Simon Byabakama alisema “Tumethibitisha stakabadhi zilizowasilishwa na mgombea kwamba ametimiza vigezo vyote vya uteuzi.”

    Bobi Wine pia alikumbushwa kwamba mikusanyiko ya umma bado imepigwa marufuku na kwamba kampeni zake zote zitaendeshwa kulingana na miongozo ya Tume ya Uchaguzi.

    Bobi Wine amewaambia wafuasi wake katika ujumbe wa Twitter kuwa sasa "wanaingia katika kipindi muhimu cha kutafuta ukombozi wao".

    Bobi Wine aliwasili kwenye kituo cha uteuzi akiwa ameandamana na mke wake.

    Rais Museveni nchini Uganda ni miongoni mwa viongozi waliohudumu kwa muda mrefu huku katiba ya nchi yao ikibadilishwa kumuwezesha kugombea kwa mara ya sita mwaka 2021.

  8. Bobi Wine awasili katika kituo cha uteuzi

    Mgombea wa upinzani nchini Uganda Robert Kyagulanyi, maarufu kama Bobi Wine, amewasili katika kituo cha uteuzi cha Kyambogo mjini Kampala.

    Polisi wamerusha vitoza machozi kutawanya wafuasi wake waliojitokeza kuwa naye siku ya uteuzi wake.

    Polisi na maafisa wa jeshi wanalinda usalama maeneo ya nje ya jengo hilo.

    Bobi anawasilisha makaratasi yake ya uteuzi kwa tume ya uchaguzi ili aweze kukabiliana na Rais Yoweri Museveni katika uchaguzi mkuu mwaka ujao.

    Hadi kufikia sasa, wagombea 10 wanawania nafasi ya Urais. Wengine ni pamoja na aliyekuwa Kamanda wa Jeshi Jenerali Mugisha Muntu aliyekuwa Waziri wa Usalama Henry Tumukunde.

    Mgombea mmoja Patrick Amuriat amekamatwa katika makao makuu ya chama chake cha Democratic Change (FDC).

  9. Viongozi 20 wa Chadema wakamatwa Singida

    Viongozi wengine 20 wa chama cha upinzani nchini Tanzania Chadema wamekamatwa mkoani singida, katikati mwa Tanzania.

    Gazeti la Habari Leo nchini humo limeandika kuwa, Mahakama imesema washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka matatu.

    Shitaka la kwanza likiwa ni kuongoza genge la wahalifu, shitaka la pili ni kula njama na la tatu ni kufanya mikusanyiko bila kibali.

    Wakati huohuo viongozi wakuu wa chama hicho wakiwa wameshikiliwa na polisi jijini Dar es Salaam baada ya kutangaza kupanga maandamano ya amani siku ya Jumatatu ili kuonesha kutokubaliana na matokeo ya uchaguzi.

    Polisi walisema wamemkamata mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani Chadema bwana Freeman Mbowe pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema na aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Ubungo Jijini Dar es Salaam Boniface Jacob.

    Na aliyegombea nafasi ya urais kupitia chama hicho Tundu Lissu, alikamatwa jana na kuachiwa baada ya muda mfupi.

  10. Mgombea urais akamatwa Uganda

    Mgombea urais nchini Uganda Patrick Amuriat amekamatwa katika mji mkuu wa Kampala, makao makuu ya chama chake cha Forum for Democratic Change (FDC).

    Wanajeshi na maafisa wa polisi walikuwa wamezungumza ofisi za chama chake kwa mujibu na gazeti la Daily Monitor.

    Bwana Amuriat alikuwa ameahidi kukiuka masharti yaliowekwa na Tume ya Uchaguzi nchini humo ya kufika kwenye shughuli ya uteuzi na wagombea 10 pekee ambao amepangiwa kuwasilisha makaratasi yake kwa ajili ya uteuzi leo mchana.

    Msimamo wa chama hicho ulitolewa licha ya jeshi la polisi jana usiku kusema kuwa liko tayari kukabiliana na yeyote atakayekiuka masharti ya tume ya uchaguzi.

  11. Upinzani Ivory Coast 'kuandaa uchaguzi mpya'

    Upinzani nchini Ivory Coast umesema kuwa unaunda serikali ya mpito baada ya kususia uchaguzi wa urais Jumamosi kwa sababu ya uamuzi wa Rais Alassane Ouattara wa kuwania muhula wa tatu.

    "Moja ya majukumu ya serikali ya mpito itakuwa kuandaa uchaguzi wa haki, uwazi na wenye kujumuisha kila mmoja", kiongozi wa upinzani Pascal Affi N'Guessan amesema.

    Aliongeza kuwa baraza la taifa la mpito limeundwa ambalo litamteua aliyekuwa rais wa nchi hiyo Henri Konan Bédié, kuongoza serikali ya mpito ambaye pia ni kiongoni wa chama cha Democratic huko Ivory Coast.

    "Kumuendeleza Bwana Ouattara kama kiongozi wa taifa kuna uwezekano mkubwa wa kusababisha vita vya ndani kwa ndani,” Bwana N'Guessan amesema.

    Chama tawala kimeonya upinzani dhidi ya jaribo lolote la kusababisha vurugu nchini humo.

    Takriban watu 9 wameuawa wakati wa uchaguzi, huku waandamanji wa upinzani wakijaribu kuzuia watu kupiga kura.

  12. Polisi wasambazwa Kampala huku Bobi Wine akitarajiwa kuteuliwa kuwa mgombea urais

    Leo ni siku ya pili ya zoezi la uteuzi wa wagombea wa kiti cha urais nchini Uganda, ambapo mpinzani mkuu Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobi Wine anatarajiwa kuteuliwa.

    Kulingana na mwandishi wa BBC Issaac Mumena, Bobi Wine anatarajiwa kuteuliwa majira ya asubuhi.

    Wakati huohuo Ubalozi wa Marekani Kampala umetoa tahadhari ya usalama kwa raia wake mjini Kampala.

    Ubalozi huo umeshauri raia wake kujizuia kufika maeneo ya mji wa Kampala na karibu na eneo la Kyambogo kwasababu ya uwezekano wa kutokea kwa ghasia Jumanne kunakohusishwa na shughuli ya uteuzi wa urais.

    Kabla ya kutoka nyumbani kwake, Bobi Wine alisema kuwa atazungumza na vyombo vya habari na amekubali kwenda na watu 10 kama inavyotakiwa na Tume ya Uchaguzi ya Uganda.

    Hata hivyo, inasemekana kwamba jeshi la polisi limezunguka ofisi za chama cha Bobi Wine cha National Unity Platform, NUP.

    Pia hali ya usalama imeimarishwa katika mji wa Kampala na vitongoji vyake.

    Hapo jana rais Yoweri Museveni alikuwa miongoni mwa walioteuliwa na kupata fursa nyengine ya kutetea kiti chake kwa muhula mwingine.

  13. Karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja hii leo ikiwa ni tarehe 03/11/2020.