IG wa Kenya akanusha kuhusika kwa polisi katika utekaji nyara wa mhariri wa kampuni ya Standard
Chanzo cha picha, NPS
Maelezo ya picha, Inspekta Jenerali wa Polisi Kenya Douglas Kanja
Huduma ya
Kitaifa ya Polisi nchini Kenya (NPS)
imekana kuhusika na kutekwa nyara kwa Mhariri msaidizi wa Standard Group Alex
Kiprotich, ikisema imeanzisha uchunguzi ili kubaini utambulisho wa watu wenye
silaha waliomkamata kando ya Barabara ya Gilgil Kwenda Nakuru.
Katika
taarifa iliyotolewa Jumatano, msemaji wa NPS Muchiri Nyaga amesema Inspekta
Jenerali wa Polisi Douglas Kanja alikuwa ameagiza Kitengo cha Kupambana na
Utekaji nyara kuchunguza tukio hilo mara moja, ikiwa ni pamoja na utambulisho
wa watu wenye silaha nzito wanaoonekana wakiwaamuru wasafiri kutoka kwenye gari
la Kiprotich.
"NPS
inachukulia utekaji nyara kwa uzito mkubwa, kwani makosa haya makubwa
yanatishia maisha, uhuru na usalama wa Wakenya," Nyaga alisema.
Ruto aagiza msako dhidi ya wachuuzi wa kigeni ili kuwalinda wafanyabiashara wa ndani
Chanzo cha picha, State House
Maelezo ya picha, Rais William Ruto
Rais William
Ruto amewaamuru raia wa kigeni wanaojihusisha na shughuli za uuzaji wa bidhaa
za biashara ndogo ndogo nchini Kenya kuacha, akisema serikali itachukua hatua
ya kuwalinda wafanyabiashara wa ndani kutokana na ushindani usio wa haki.
Akizungumza
baada ya kukutana na wafanyabiashara wa Biashara ndogo, ndogo na za Kati (MSME)
katika Ikulu ya Nairobi, Jumatano, Septemba 2, Ruto alirejelea wasiwasi
ulioibuka kwamba baadhi ya wageni wameanzisha biashara zinazouza bidhaa kama
vile duvet na bidhaa zingine, wakishindana moja kwa moja na wachuuzi wa ndani
na wafanyabiashara wadogo.
Rais alisema
Muswada uliopo mbele ya Bunge hivi sasa unalenga kuwazuia raia wa kigeni
kujihusisha na shughuli fulani za biashara nchini Kenya.
Alitoa wito
kwa wafanyabiashara na wadau wengine kujadili sheria iliyopendekezwa kabla ya
kupitishwa ili kuhakikisha kwamba mianya yoyote inayowaruhusu wageni
kujihusisha na biashara za uchuuzi na biashara zingine ndogo ndogo imeziba.
"Tuna
Muswada Bungeni kwamba kuna baadhi ya shughuli za biashara ambazo wageni
hawawezi kufanya nchini Kenya. Kwa mujibu wa sheria, nataka mketi chini na
wafanyibiashara waangalie kwa sababu hatujapitisha ili tufunge mianya yote ili
mtu asitoke China kuja kuwa mchuuzi," Ruto alisema.
Rais alisema
kwamba hata wakati serikali inasubiri Bunge lifikirie na kupitisha sheria
iliyopendekezwa, hatua za kiutawala zitachukuliwa kushughulikia raia wa kigeni
wanaofanya kazi kama wachuuzi na wafanyabiashara wadogo.
Iran yashambulia kambi za kijeshi za Marekani Kuwait
Chanzo cha picha, Reuters
Kumekuwa na
ripoti za mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani za Iran kwenye
kambi za Marekani huko Kuwait
Saa moja
baada ya jeshi la Kuwait kutangaza katika taarifa kwamba mifumo yake ya ulinzi
wa anga ilikuwa imeshirikishwa ili kurudisha kutungua mashambulizi ya ndege
zisizo na rubani na makombora yanayotoka Iran, shirika la habari la Tasnim,
karibu na Walinzi wa Mapinduzi, liliandika: "Kambi za Marekani huko Kuwait
zilishambuliwa na makombora na ndege zisizo na rubani za Iran."
Shirika la
habari halikutoa maelezo zaidi kuhusu tukio hilo, na CENTCOM - Amri Kuu ya
jeshi la Marekani - bado haijajibu ripoti hizo.
Udhibiti
mkali katika nchi za Ghuba ya Uajemi umefanya iwe vigumu sana kwa vyombo vya
habari kupata ufikiaji wa moja kwa moja kwenye maeneo yaliyoshambuliwa, na
Marekani imeweka vikwazo kwenye uchapishaji wa picha za setilaiti za maeneo
haya.
Siku ya
Jumatano, Tasnim ilichapisha picha za angani zinazohusishwa na mashambulizi
yake ya Jumanne kwenye kambi za Marekani huko Jordan, ikidai kuonyesha athari
zilizoachwa na mashambulizi haya.
Trump aweka sura yake katika sarafu ya dola 1 ya Marekani
Chanzo cha picha, Reuters
Picha ya
Donald Trump imeingia kwenye sarafu ya Marekani – ikiwa mara ya kwanza kwa rais
aliye hai kuonekana kwenye sarafu ya Marekani katika karne moja.
Siku ya
Jumatano, Kampuni ya Marekani ya Mint ilizindua sarafu ya ukumbusho ya $1 yenye
picha ya Trump pamoja na maneno "Kwa Mungu tunamwamini", kusherehekea
maadhimisho ya miaka 250 ya Marekani.
Sarafu ya
toleo maalum ina "roho, fahari, na urithi wa taifa linalokaribia
maadhimisho yake muhimu", Kampuni ya Marekani ya Mint ilisema.
Sarafu hizo
- zenye bei ya $61 (£45) kwa roll ya 25 na mfuko wa 100 kwa $154.50 -
"hazikuwepo kwa sasa" kwenye tovuti ya Kampuni ya Marekani ya Mint
ndani ya saa chache baada ya kuanza kuuzwa.
BBC
imewasiliana na Kampuni ya Marekani ya Mint, Hazina na Ikulu kwa maelezo zaidi.
Sarafu hiyo
"imeundwa kusherehekea hatua hii muhimu ya kitaifa" kwa "muundo
wa maadhimisho ya kizazi kimoja unaokusudiwa kuwa nyongeza bora kwa sarafu za
kisasa," Kampuni ya Marekani ya Mint ilisema.
Pia zinauzwa
katika mashine za kuuza bidhaa katika duka la US Mint huko Washington DC.
Ingawa
sarafu hizo zina rangi ya dhahabu hazina dhahabu yoyote halisi. Kulingana na US
Mint, sarafu hizo zinasharikisha 88.5% ya shaba huku asilimia iliosalia
ikiundwa na zinki, manganese na nikeli.
Israel yafichua "mipango iliyoandaliwa" ya kuwafukuza Wapalestina kutoka Ukanda wa Gaza
Chanzo cha picha, AFP via Getty
Waziri wa
Ulinzi wa Israeli Yisrael Katz amefichua kwamba Israeli ina mipango tayari ya
kuwaondoa Wapalestina kutoka Ukanda wa Gaza, lakini inasubiri Marekani kufikia
makubaliano kuhusu wapi Wagaza watahamishiwa.
Katika
mkutano na waandishi wa habari Jumatano, Katz alisema: "Hatimaye hakuna
suluhisho halisi kwa Gaza bila uhamiaji huu," akiongeza kuwa serikali ya
Israeli "imepanga na iko tayari kuwaondoa, kwa njia ya baharini, kwa njia
ya anga, na kwa kila njia inayowezekana."
Wakati huo
huo, Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu amesema kwamba nchi yake haina
mpango wa kujiondoa kutoka eneo lolote lililo chini ya udhibiti wa kijeshi
katika Ukanda wa Gaza, akisisitiza udhibiti wa Israeli juu ya eneo hilo.
Netanyahu
alitoa matamshi hayo wakati wa ziara yake Jumatano kwa vikosi vya Israeli huko
Gaza.
Hii ilikuwa
ziara ya kwanza ya uwanjani ya Netanyahu tangu makubaliano ya kusitisha
mapigano yatangazwe Oktoba iliyopita.
Shambulio la Iran dhidi ya meli ya mafuta ya Saudia laua mabaharia wawili wa Ufilipino - Saudia
Chanzo cha picha, Reuters
Saudi Arabia
imelaani kile ilichosema ni shambulio la Iran dhidi ya meli kubwa ya mafuta
inayomilikiwa na Saudi Arabia Jumatatu usiku na kuwaua mabaharia wawili wa
Ufilipino.
Kampuni ya
kitaifa ya meli ya Saudi Arabia, Bahri, ilithibitisha Jumatano kwamba meli yake
ya Sidr "ilihusika katika tukio la utovu wa usalama wakati ikipitia
Mlango-Bahari wa Hormuz".
Sidr
ilipigwa na makombora kaskazini mwa rasi ya Musandam ya Oman, kulingana na
makampuni ya usalama wa baharini.
Meli kubwa
ya mafuta inayomilikiwa na Korea Kusini, Senegal Prosperity, iliripotiwa
kupigwa mashariki mwa Musandam wakati huo huo.
Iran
haijajibu madai ya Saudi Arabia. Lakini ilisema mapema kwamba meli mbili za
mafuta zilishika moto baada ya kugonga mabomu zikitumia njia isiyoidhinishwa
kupitia mlango-bahari.
Habari za
vifo vya mabaharia hao zilikuja baada ya jeshi la Marekani kutekeleza wimbi la
mashambulizi ya angani dhidi ya Iran na vikosi vya Iran kulenga kambi za
Marekani katika nchi jirani za Kiarabu kwa makombora na ndege zisizo na rubani
katika ufyatulianaji wao mkubwa wa risasi tangu Julai.
Siku ya
Jumatano waziri wa afya wa Iran alisema watu 18 waliuawa na 108 kujeruhiwa
katika mashambulizi ya Marekani.
Iran
imeishutumu Marekani kwa "uhalifu wa kivita" kutokana na shambulio liliowaua
watu wanne wakiwemo watoto wawili kwenye sherehe ya harusi katika mji wa kusini
wa Sirik. Jeshi la Marekani lilisema linachunguza ripoti hizo.
Taarifa ya
kampuni ya meli Bahri ilisema "tukio la usalama" ambalo halijatajwa
lililoathiri Sidr lilitokea katika Mlango-Bahari wa Hormuz yapata saa 23:40 kwa
saa za huko (19:40 GMT) Jumatatu.
"Ni kwa
huzuni kubwa kwamba Bahri inathibitisha kufariki kwa mabaharia wake wawili wa
Ufilipino kutokana na tukio hilo," iliongeza.
"Kampuni
inatoa rambirambi zake za dhati na salamu za rambirambi kwa familia zao,
wapendwa wao, na wafanyakazi wenzao wakati huu mgumu."
EU na Nato zaionya Urusi baada ya taifa hilo 'kuanzisha' mgogoro mpya dhidi ya Ujerumani
Chanzo cha picha, Reuters
Wakuu wa
Nato na Tume ya Ulaya wameonya kwamba Urusi inazidisha uchokozi wake na wameapa
kuikabili iwapo itaendelea.
"Shambulio
la Leipzig linaashiria uchokozi mpya katika
ardhi ya Umoja wa Ulaya unaohusishwa moja kwa moja na Urusi," alisema Rais
wa Tume hiyo Ursula von der Leyen, siku moja baada ya Ujerumani kulaumu Urusi
kwa shambulio la ndege isiyo na rubani mwezi uliopita kwenye uwanja wa ndege wa
Leipzig.
"Lazima
tuchukue hatua na hiyo ina maana kujibu uzembe wa Urusi haraka na kwa njia bora
zaidi," von der Leyen alisema.
Katibu Mkuu
wa Nato Mark Rutte amesema muungano mzima, ambao unajumuisha Marekani, unasimama
"kwa mshikamano kamili na Ujerumani".
Urusi
imekataa shutuma za Ujerumani kwamba ndege isiyo na rubani iliyobeba vilipuzi
ililenga ndege ya mizigo ya Ukraine kwa makusudi mnamo tarehe 4 Agosti.
Ndege hiyo
iliharibiwa na roboti katika uwanja wa ndege wa Leipzig/Halle na ndege ya pili
isiyo na rubani inadhaniwa kugongana na ndege nyingine ya mizigo.
Ndege ya
tatu isiyo na rubani iliripotiwa kupatikana siku 10 baadaye katika uwanja wa
ndege, ambao ni kitovu muhimu cha Nato na hutumiwa mara kwa mara na ndege ya
usafiri ya Antonov ya Ukraine.
Ni hadi
Jumanne ambapo serikali ya Ujerumani ilisema uchunguzi wa polisi na uchunguzi
wa kijasusi umethibitisha kwamba Urusi ilihusika na matukio hayo.
Waziri wa
mambo ya ndani alisema kwamba umbo la ndege isiyo na rubani, vipengele vyake,
vilipuzi na kifyatulio chake , vyote vilijulikana kutoka Urusi.