Shambulizi la Palma Msumbiji: Kwanini kujihusisha kwa kundi la IS kunatiliwa chumvi

Chanzo cha picha, EPA
Uvamizi wa hivi karibuni uliofanywa na wanamgambo katika mji wa Palma nchini Msumbiji kuligonga vichwa vya habari duniani kwasababu raia wa kigeni waliuawa na pia kwa kuwa kundi la Islamic State lilikiri kutekeleza mauaji hayo, na kupelekea mgawanyiko mkali kuhusu jinsi mgogoro wa miaka minne nchini humo unastahili kutathminiwa, fuatili mtazamo wa mchambuzi Dkt. Joseph Hanlon.

Palma siku zote umekuwa mji mtulivu wenye shughuli za uvuvi lakini lilikuwa hadi mwaka jana ulipobadilishwa na kuwa kitovu kinachostawi cha sekta ya gesi.
Kampuni ya Ufaransa ya Total ilianza ujenzi wa mradi huyo wa dola bilioni 20 ambao utakuwa ndio hifadhi ya pili ya gesi kwa ukubwa Afrika.
Kampuni ya Total ilikuwa inajenga ukuta pamoja na uwanja wa ndege na gati yao katika rasi ya Afungi umbali wa kilomita 10 kusini mwa Palma. Lakini wanakandarasi wote walikuwa wanaishi eneo la Palma, ambalo lilikuwa limeanza kushuhudia ongezeko la majengo ya hoteli, benki na yadi za ujenzi.
Wanamgambo walipoingia eneo hilo Machi 24, walikuwa wanashambulia mji unaokua kwa haraka ambao raia wa kigeni wamewekeza na wenye zaidi ya wafanyakazi 1,000 wa kigeni wakihusishwa na sekta ya gesi.
Wiki mbili tu kabla ya shambulizi hilo, Marekani ilikuwa imetaja wanamgambo wa eneo hilo kama "ISIS wa Msumbiji" na kulibaini kama Shirika la Kigeni la Kigaidi.
Siku nne baada ya shambulizi, kundi la Islamic State lenye kuhusishwa na shirika la habari la Amaq lilitoa taarifa likidai kuwa wapiganaji wake wamevamia mji wa Palma na kuharibu ofisi za serikali na benki.
Kundi la IS lilidai kuhusika na shambulizi hilo
Taarifa za IS ziligonga vichwa vya habari.
Shirika la habari la CBS lililitaja kama "Uvamizi wa wanamgambo wa Isis" huku mamia ya wafanyakazi wa kigeni wakijawa na hofu. Gazeti la Daily Mirror la Uingereza liliandika "Ugaidi wa Isis" na "mauaji ya halaiki ya jihadi". Gazeti la UK Times awali lilikuwa limeandika wanamgambo wa Isis wavamia mji wenye raia wa kigeni Msumbiji.
Lakini siku hiyo hiyo, kabla baadhi ya magazeti kuandika vichwa vyao vya habari, dai la kundi la IS kutekeleza shambulizi hilo lilifutwa.
Jasmine Opperman, mchambuzi wa maeneo yenye mgogoro Afrika ambaye amekuwa akifuatilia wanamgambo hao kwa karibu katika mkoa Cabo Delgado nchini Msumbiji, alionesha kuwa video na picha hazikuwa za eneo la Palma, bali kutoka Mocimboa da Praia, kilomita 65 kuelekea kusini.

Chanzo cha picha, EPA
Moja ya kile kinachofanywa na wanamgambo sasa hivi katika mashambulizi ni kusitisha mawasiliano yote kwa kutumia mundu kukata kebo.
Mji wa Palma, mawasiliano ya simu yalikatizwa dakika 30 kabla ya kuanza kwa shambulizi. Kwahiyo, wanamgambo wa IS na kituo cha habari cha Amaq hawakuwa na taarifa za uvamizi huo. Pamoja na picha za uwongo, na taarifa ambazo hazikuwa na ukweli wowote, zilikuwa zimeshachapichwa katika vyombo vya habari vya kimataifa.
Madai hayo pia yalikuwa ya kwanza kuhusu Msumbiji kutoka kwa IS au Amaq katika kipindi cha miezi mitano.
Mwaka 2019, wanamgambo walishirikiana na kundi la IS na kuonekana kupata umaarufu na pia walituma video kupitia simu za mkononi. Waliendelea kusisitiza kuwa walilenga serikali na hivyo basi kukawa na picha zinazoonesha wanamgambo walioshika bendera zao nyeusi za IS mbele ya jengo la utawala wa eneo lililochomeka.
Lakini wanamgambo waliendelea kutumia jina walilopewa na watu wa eneo, al-Shabab, lenye kumaanisha "vijana" na halina uhusiano wowote na kundi la al-Shabab lenye makao yake nchini Somalia.
Acled, wafuatiliaji wa karibu wanaoaminiwa katika mgogoro wa Cabo Delgado, walihitimisha katika ripoti ya hivi karibuni kuwa: "Hakuna ushahidi kutokana na shambulizi la Palma kwamba kundi la IS linadhibiti eneo la kimkakati la wanamgambo."
Wanamgambo hao ni kina nani?
Wanamgambo hao ni wa dini ya Kiislamu kutoka eneo la pwani la Cabo Delgado, waliosajiliwa na wahubiri wa eneo kwa ujumbe wao kuwa Sharia, yaani Sheria ya Kiislamu italeta usawa na kila mmoja atakuwa na mgao wake katika utajiri za mali za eneo siku za usoni.

Chanzo cha picha, EPA
Shambulizi la kwanza lilikuwa mwaka 2017, Mocimboa da Praia, mji pekee na bandari kaskazini mwa eneo. Ujumbe huo na ahadi ya ajira na pesa kwa vijana kulichochea wanaume kujiunga na kundi hilo la wanamgambo ambalo lilipata uungwaji mkono kutoka kwa jamii ya eneo.
Vita hivyo vilienea katika wilaya sita na miji mikubwa - kote isipokuwa mji wa Palma - ilishambuliwa na kukaliwa na kundi hili wakati fulani. Wanamgabo hao walidhibiti mji wa Mocimboa da Praia na kuondoka kwa kipindi cha mwaka mmoja pekee.
Taarifa kulingana na mahojiano na wanawake waliotoroka katika mji wa Palma ilichapishwa Aprili 12 na João Feijó, mkurugenzi wa Shirika la Waangalizi wa Maeneo ya Vijijini Msumbiji.
Wanawake hao walibaini kuwa baadhi ya viongozi ni Watanzania, baadhi yao wakidai kuwa ni IS na Wasomali ambao walisema wao sio IS lakini ni sehemu ya kundi ambalo halijabainiwa.
Mji huo uliporwa na jeshi
Kile ambacho wachambuzi wanakubaliana kwa kauli moja ni kuwa kundi hilo lilianza kama la eneo na kuwa wanamgambo wa kigeni na IS walijiunga nao baadaye. Na pia tofauti ni katika kuangazia umuhimu wa hilo.
Mtazamo wa Marekani ni kwamba kundi la IS limeteka nyara kundi hilo la wanamgambo na sasa hivi ndilo linaloliongoza.
Mtazamo wa watafitii wengi wa Msumbiji ni kuwa kuna wanamgambo wa kigeni na pia wanamgambo wa IS waliojiunga nao lakini kundi hilo linalojiita al-Shabab bado linaendeshwa na malengo ya wenyeji.
Na hilo limesababisha mgawanyiko mkubwa.

Chanzo cha picha, Dyck Advisory Group/Handout via REUTERS
Wanamgambo hao walisafiri hadi mji wa Palma bila pingamizi yoyote licha ya kwamba kulikuwa kumetolewa onyo kwa kipindi cha miezi miwili la kutokea kwa shambulizi baada ya mvua kuisha, na serikali ikaahidi kampuni ya Total kulinda mji wa Palma.
Jeshi na polisi wamepata mafunzo duni, hawana vifaa na pia ni wafisadi.
Wanamgambo hao kwa kipindi kirefu hawajawahi kuvamia walipo wanakandarasi ya kampuni ya Total na wiki ya kwanza ya Aprili, baada ya washambuliaji kuondoka mji wa Palma, jeshi likapora mji huo na kuingia kwenye maeneo ya wanakandarasi.
Hili lilijitokeza kupitia picha zilizochukuliwa kwa juu na pia kutokana na taarifa za wanakandarasi walioshuhudia hilo na hata maafisa wa eneo wenye hasira.
Maslahi ya kigeni katika kuhusisha IS
Kuna msukumo mkubwa wa jeshi kuchukua hatua.
Katika mkutano na wanahabari uliofanyika Machi 11, John T Godfrey, Mjumbe maalum wa Marekani kwa niaba ya Muungano wa Dunia unaolenga kukabiliana na Isis, alisema: "Lazima tukabiliane na kundi la Isis Afrika." Marekani inataka kujihusisha na eneo la Cabo Delgado kukabiliana na IS "shughuli za kigaidi" zinazoendelea huko.
Ureno inatuma wanajeshi wake na kama kingozi wa sasa hivi wa Baraza la Ulaya inapigania EU ikubali kuingilia kati mgogoro huo.
Jeshi la Afrika Kusini tayari linashika doria eneo la pwani na pia lingependa kuingia katika eneo la ardhini.
Na hapo ndio jukumu la IS linapokuwa la kila mmoja.

Hakuna nchi ambayo inaweza kutoa usaidizi wa kijeshi kwa Msumbiji kukabiliana na kundi hilo lenyewe. Lakini vita ambavyo ni adui wa dunia kama vile IS ndio vinavyotoa sababu ya hatua kama hizo kuchukuliwa.
Kwa maneno mengine, IS na Marekani zinaonekana kuwa na maslahi yanayoendana katika kuendelea umuhimu kundi la Jihadi.
Afrika Kusini nayo ilionya kuwa wanaoendeleza kundi la IS huku kiwango cha umaskini kikiendelea kuwa vile Cape Town, IS huenda wakatumia eneo la Cabo Delgado kama msingi wa kuhamia eneo la kusini, kwahiyo, Afrika Kusini inastahili kutuma wanajeshi. Lakini ikiwa wanamgambo hao ni vuguvugu la eneo tu, hakuna haja ya hatua hiyo.
Serikali ya Msumbiji ya Frelimo ina wasiwasi mkubwa kuwa wageni na hata vyombo vya habari vya eneo, hawafuatilii chanzo cha vita hivyo na kuangazia vile ambavyo kundi la Frelimo limekuwa tajiri huku watu wa kawaida eneo la Cabo Delgado wakiendelea kuwa maskini.
Aprili 7 Rais Filipe Nyusi alisema kuwa Msumbiji inahitaji usaidizi "katika vita dhidi ya ugaidi". Lakini akaongeza kuwa: "Wale wanaowasili kutoka nchi za kigeni hawatachukua nafasi yetu, badala yake watatuunga mkono. Ni suala la kiutawala."

Chanzo cha picha, AFP
Hata hivyo, mahojiano na wanawake waliotoroka wanamgammbo huko eneo la Palma wanaonesha kuwa na mtazamo tofauti kuhusu serikali.
Wanasema kuwa wapiganaji wana machungu kweli na serikali na kinachowapa msukumo ni vitu vya dunia - ajira na pesa. Lakini wengependa kuachana na kundi hilo kama kungekuwa na mbadala.

Maelezo zaidi kuhusu mzozo wa Msumbiji:














