'Musiuze pombe kwenye vikombe vya kunywa chai', migahawa yaonywa Afrika Kusini

Two women in South Africa drinking tea

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Je anayokunywa ni chai au pombe?

Waziri anayesimamia maafisa wa polisi Afrika Kusini ameonya migahawa dhidi ya kuficha ukweli kwa kutumia vikombe vya kunywa chai kuwekea pombe wakati huu ambapo uuzaji wa pombe umepigwa tena marufuku.

Rais Cyril Ramaphosa amesema "tabia mbovu" zinazosababishwa na unywaji wa pombe ndio chanzo cha kuongezeka kwa usambaaji wa virusi vya corona wakati anatangaza marufuku hiyo Jumatatu.

Mlipuko mpya wa virusi vya corona unaosambaa kwa kasi ya juu nchini Afrika Kusini umeshuhudiwa nchini Afrika Kusini kwa kipindi cha wiki mbili.

Wakati anachukua hatu hiyo, pia amepiga marufuku mikusanyiko wakati wa mazishi, saa za kutotoka nje ni kuanzia saa tatu usiku hadi kumi na mbili asubuhi, na kuagiza maduka yote, baa na maeneo mengine kufungwa kufikia saa mbili usiku.

Police Minister Bheki Cele

Chanzo cha picha, AFP

Maelezo ya picha, Waziri anayesimamia maafisa wa polisi Bheki Cele ameonya migahawa dhidi ya kutumia mbinu za kijanja kunywa pombe iliyopigwa marufuku

Akizungumza katika mkutano na wanahabari,waziri Bheki Cele alisema migahawa itakayokiuka agizo hilo itapoteza leseni na wamiliki kushtakiwa.

"Musiweke pombe kwenye vikombe vya kunywa chai migahawani. Musiweke pombe kwenye chumba za vinywaji zilizoandikwa kinywaji hiki hakina pombe kabisa. Tunajua ujanja munaotumia," Bwana Cele amesema.

"Ikiwa tutaona kuna kitu tofauti kwenye vikombe vya kunywa chai - tutahakikisha munapoteza leseni zenu."

Inasemekana kwamba kuna baadhi ya migahawa ambayo imekuwa ikitumia mbinu janja kuuza pombe licha ya kupigwa marufuku hiyo ambayo itaendelea kutekelezwa hadi katikati ya Januari .