Maporomoko mengine ya ardhi yakumba Kenya na Uganda

Chanzo cha picha, Wizara ya Mambo ya ndani Kenya
- Author, Laillah Mohammed
- Nafasi, BBC News Swahili
- Akiripoti kutoka, Nairobi
- Muda wa kusoma: Dakika 3
Zaidi ya watu 40 wamefariki kufuatia maporomoko ya ardhi katika maeneo ya milimani yanayopakana na Kenya na Uganda.
Wafanyakazi wa serikali na mashirika ya kutoa huduma za dharura kutoka pande zote mbili wametumwa katika maeneo yaliyoathiriwa kusaidia katika shughuli ya uokoaji.
Maporomoko hayo ya matope yamechangiwa na kuendelea kunyesha kwa mvua kubwa
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Kenya, Kipchumba Murkomen, ametoa wito kwa wakaazi katika eneo hilo kuwa waangalifu hasa wale wanaoishi sehemu za milima na kuwagiza mamlaka katika eneo hilo kuwahamisha watu walio hatarini hadi maeneo ya juu.
Nchini Uganda, watu 18 walithibitishwa kufariki na Shirika la Msalaba Mwekundu kufuatia msururu wa maporomoko ya ardhi katika eneo linalopakana na Kenya.
Maporomoko manne ya ardhi yametokea katika siku za hivi karibuni na kusababisha vifo na watu kadhaa kupotea au kujeruhiwa.
Kulingana na shirika la Msalaba Mwekundu nchini Kenya kufikia sasa watu 2 wamejeruhiwa na kukimbizwa hospitalini kutoka eneo la Kibendo Keiyo Kaskazini, Kaunti ya Elgeyo Marakwet.
Hii inafuatia maporomoko mengine mabaya ya ardhi yaliyotokea tarehe Jumamosi tarehe 1 Novemba ambayo yalisababisha vifo vya watu 26, kuwajeruhi makumi ya watu. Kulingana na wizara ya elimu, 14 kati ya waliofariki wamethibitishwa kuwa wanafunzi. Watu 25 hawajulikani walipo.
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Siku ya Jumamosi Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen alisema pia kwamba watu 25 wameokolewa kwenye maporomoko hayo yaliyosababishwa na mvua kubwa inayonyesha katika maeneo tofauti nchini Kenya.
''Shughuli za uokoaji bado zinaendelea, huku watu 30 wakiripotiwa kutojulikana walipo. Majeruhi wamesafirishwa kwa ndege hadi katika hospitali kuu ya rufaa ya Moi iliyopo jijini Eldoret,'' alisema Murkomen alipozuru eneo la tukio lililopo katika bonde la Kerio katika eneo bunge la Marakwet Mashariki.
Shirika la msalaba mwekundu ambalo linashirikiana na asasi za kiusalama kusimamia shughuli za uokoaji liemsema kwamba juhudi za uokoaji zimetatizwa na hali mbaya ya eneo la tukio kufuatia uharibifu wa majumba kwa tope na maji iliyotokea kwenye milima kijijini Chesongoch.
''Juhudi za kuawafikia waathiriwa zimetatizwa na kuharibiwa kwa barabara na maji ya mafuriko yaliyojaa katika eneo kubwa , lakini wahudumu wetu wanaendelea kufanya kazi bila kuchoka kuwafikia wenye kuhitaji msaada,' ilisema ujumbe wa msalaba mwekundu uliochapishwa kwenye mtandao wa kijamii wa X.

Chanzo cha picha, Wizara ya Mambo ya ndani Kenya
Kwa sasa polisi na shirika la msalaba mwekundu wanapiga doria katika eneo hilo kwa kutumia ndege aina ya helikopta ili kuweza kuwatambua waathiriwa waliohai walipo.
Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen amesema kwamba vikosi vya kitengo maalum cha uokoaji kutoka jeshi la Kenya KDF linashirikiana na polisi , wahudumu wengine wa dharura kusaidia kuwatafuta waliopotea na pia kutafuta ikiw akuna miiili iliyozikwa ardhini na tope.
Mvua kubwa inaripotiwa kunyesha usiku wa kuamkia Jumamosi Novemba 1 na kusababisha maji kujaa katika maeno yaliyo chini yam ilima katika bondo hilo la Kerio.

Usafiri katika eneo la tukio umesimamishwa kwa muda kwa sababu ya maji yaliyojaa kote na mapormoko ya ardhi. Wakazi wameombwa kutopanga safari ambazo zio za dharura kwa sasa hadi hali iwe nzuri. Maji wa mafuriko na maporomoko ya usiku wa kuamkia Jumamosi hii yalisomba baadhi ya nyumba katika eneo hilo.
Familia zilizoathirika zinapokea misaada ya mahali pa kulala, maji safi, dawa na chakula.
Idara ya utabiri wa hali ya hewa ya Kenya imesema kwamba maporomoko ya ardhi huenda yakatokea katika kaunti angalau 30 ambazo zinashuhudiwa viwango vya juu vya mvuwa.
Ajali hii inatokea siku chache tu baada ya ajali inyine kutokea nchini Uganda ambapo watu tisa walifariki, wakiwemo Watoto waliokutwa na mauti walipozikwa na mapormoko ya ardhi yaliyotokea katika maeneo mawili yaliyipo mashariki mwa Uganda.
Mapormoko hayo yalitokea katika miji ya milimani ya Bukwo na Kween usiku wa Jumatano October 29 kutokana na mvua kubwa iliyonyesha magharibi mwa Kenya na Mashariki mwa Uganda
Hii sio mara ya kwanza kwa ajali kama hii kutokea katika eneo hilo katika muda wa muongo mmoja uliopita.
Watu 20 walifariki kwenye mkasa uliotokea katika bonde hilo hilo la Kerio mnamo 2013, huku wengine 132 wakifariki kwenye ajali nyingine mbaya ya maporomoko ya ardhi mnamo 2018 ambapo watu 225,000 walipoteza makazi ya baada ya kusombwa na maji, kuzikwa na tope au kuharibiwa kabisa kutokana na mvua kubwa iliyonyesha kati ya Machi na Agosti mwaka huo.












