“Mtoto wetu wa kiume alifariki. Ila tutatumia mbegu zake kupata mjukuu”

xc

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Wanandoa hao wanasema walifika kortini kwa sababu walitaka kuendeleza "urithi" wa mtoto wao.
    • Author, Geeta Pandey
    • Nafasi, BBC
  • Muda wa kusoma: Dakika 5

Wanandoa wawili nchini India wana furaha baada ya mahakama kuamuru hospitali kuwakabidhi sampuli ya mbegu za kiume zilizogandishwa za mtoto wao aliyeaga dunia, ili wapate mjukuu kupitia mwanamke atakayebeba ujauzito kwa mbegu hizo.

Amri ya kihistoria ya Mahakama Kuu ya Delhi ilikuja baada ya vita vya kisheria vya miaka minne.

“Tulipata bahati mbaya ya kumpoteza mtoto wetu. Lakini mahakama imetupa zawadi ya thamani sana,” anasema Harbir Kaur, mama wa marehemu.

Bi Kaur na mumewe Gurvinder Singh waliwasilisha ombi mahakamani baada ya Hospitali ya Ganga Ram ya Delhi kukataa kutoa mbegu za mtoto wao mwezi Desemba 2020, ambazo zilikuwa zimehifadhiwa katika maabara ya hospitali.

Mwana wa wanandoa hao mwenye umri wa miaka 30, Preet Inder Singh, aligunduliwa na saratani ya damu Juni 2020 na alilazwa hospitalini kwa matibabu.

"Kabla hajaanza matibabu ya tiba-kemikali, hospitali ilimshauri ahifadhi mbegu zake kwani matibabu hayo yanaweza kuathiri vibaya ubora wa mbegu zake," wakili wa familia hiyo, Gurvinder Singh aliambia BBC.

Preet Inder, ambaye hakuwa ameoa, alikubali na mbegu zake ziligandishwa tarehe 27 Juni 2020. Alifariki mapema mwezi Septemba.

Miezi michache baadaye, wazazi hao wenye huzuni walipotaka kupewa mbegu ya mwana wao, hospitali ilikataa ombi lao. Ndipo wanandoa hao wakawasilisha ombi katika Mahakama Kuu ya Delhi.

Hukumu ya Mahakama

e

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Hakuna makubaliano ya kimataifa kuhusu suala la uzazi baada ya kifo
Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Wanandoa hao walio na umri wa miaka 60, waliambia mahakama watamlea mtoto yeyote atakayezaliwa kwa kutumia mbegu za mtoto wao. Na watakapo fariki, binti zao wawili wametoa ahadi mahakamani watamshughulikia kikamilifu mtoto huyo.

Katika agizo lake wiki iliyopita, Jaji Prathiba Singh alisema "chini ya sheria ya India, hakuna marufuku ya uzazi baada ya mtu kufa" ikiwa mmiliki wa manii alitoa idhini.

Aliongeza kuwa wazazi wana haki ya kupata sampuli hiyo kwani kukosekana kwa mke au watoto – wazazi wanakuwa warithi halali chini ya Sheria ya Urithi wa Kihindu.

Familia hiyo iliamua itatumia mbegu zake baada ya mwanamke ambaye ni jamaa na familia hiyo kukubali kubeba mimba. Na wameamua kuleweka jambo hilo ndani ya familia kwani chini ya sheria ya India, kubeba mimba kwa sababu za kibiashara ni kinyume cha sheria.

Mahakamani, hakimu alitoa mfano wa kesi ya 2018 ya mwanamke mwenye umri wa miaka 48 katika mji wa magharibi mwa India wa Pune ambaye alipata wajukuu mapacha kwa njia ya uzazi kwa kutumia mbegu za mtoto wake mwenye umri wa miaka 27, aliyefariki kwa saratani ya ubongo huko Ujerumani.

Mwanawe ambaye hakuwa ameoa, alitoa idhini kwa mama yake na dadake kutumia mbegu zake baada ya kifo chake na hospitali ya Ujerumani iliwakabidhi mbegu hizo.

Pia mfano wa kesi ya mwaka 2019 ulitolewa, ambapo Mahakama Kuu ya New York iliwaruhusu wazazi wa mwanajeshi mwenye umri wa miaka 21 aliyefariki kwenye ajali ya kuteleza kwenye theluji, kutumia mbegu zake zilizogandishwa kupata mjukuu.

Katika agizo lake, Jaji Singh pia alitaja kesi kadhaa za uzazi baada ya kifo, ikiwa ni pamoja na kesi ya 2002 kutoka Israel ambapo wazazi wa mwanajeshi mwenye umri wa miaka 19 aliyeuawa huko Gaza, walipata kibali cha kisheria kutumia mbegu za mtoto wao kupata mtoto kupitia mwanamke aliyekubali kubeba ujauzito.

Marekani, Uingereza, Japani, Jamhuri ya Czech na baadhi ya nchi huruhusu uzazi baada ya kifo kwa idhini iliyoandikwa. Australia inaweka sharti la ziada la kusubiri baada ya kipindi cha mwaka mmoja baada ya kifo ili kuruhusu hisia za kuondokewa kutulia.

Lakini kitendo hiki kimepigwa marufuku katika nchi kadhaa kama vile Italia, Sweden, Switzerland, Ufaransa, Malaysia, Pakistani, Hungaria na Slovenia, na nchi nyingi Kusini mwa Asia - Sri Lanka, Nepal, Bhutan na Bangladesh - hawana miongozo.

Na hata katika nchi ambazo zina sheria za uzazi baada ya kifo, kesi nyingi huhusisha mke au mpenzi ambaye anataka kutumia mbegu za mwenza wake ili kupata ujauzito.

Idadi ya wazazi wanaotafuta mbegu za wana wao imeongezeka nchini Israel, na kadiri mzozo na Urusi unavyozidi kuongezeka, wanajeshi nchini Ukraine wanapewa huduma ya kuhifadhi mbegu za kiume bila malipo.

Vita vya Kisheria

dfc

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Kliniki za uzazi nchini Ukraine zinatoa huduma ya bure ya kuhifadhi mbegu za kiume kwa wanajeshi

Kama Jaji Singh alivyobainisha katika agizo lake, hakuna makubaliano ya kimataifa kuhusu suala hilo.

Hospitali ya Ganga Ram ilisema kisheria wanaweza kutoa mbegu hizo kwa mwenza wake pekee. Walisema mahakamani kuwa hakuna sheria au miongozo iliyo wazi ambayo inaruhusu kutolewa mbegu za mwanaume aliyekufa ambaye hajaoa kwa wazazi wake au warithi wake.

Serikali ya India pia ilipinga ombi la wanandoa hao, ikisema sheria ya kubeba ujauzito kupitia mbegu chini India inakusudia kuwasaidia tu wanandoa au wanawake wasio na uwezo wa kuzaa, na sio watu ambao wanataka kupata mjukuu.

Mamlaka pia ilisema Preet Inder alikuwa hajaoa – Sheria ya India ya 2021 inazuia watu wasio na wenza kupata watoto kupitia uzazi wa aina hiyo - na hakuwa ameacha kibali chochote cha maandishi au cha mdomo kwa matumizi ya mbegu zake zilizogandishwa ili wazazi wake wawe na haki ya moja kwa moja ya kuzitumia.

Bi Aggarwal, wakili wa wanandoa hao, alidai mahakamani kwamba alipokuwa akijaza fomu ya kuhifadhi mbegu hizo, Preet Inder alieleza wazi ni kwa madhumuni ya kutungishia ujauzito.

Fomu hiyo, ilikuwa na nambari za simu za baba na marehemu, na hilo lilimaanisha idhini. Bi Aggarwal alidokeza kuwa baba huyo amekuwa akiilipa maabara kwa ajili ya kuhifadhi mbegu hizo.

Jaji Singh alikubaliana na hoja ya Bi Aggarwal kwamba Preet Inder alikuwa ametoa idhini ya mbegu zake kutumika kwa madhumuni ya kupata watoto.

“Hakuwa ameoa na hakuwa na mwenza yeyote. Alikusudia mbegu hizo zitumike ili kupata mtoto.”

Agizo la mahakama, Bi Kaur anasema, limempa "mwanga wa matumaini," kwamba "tutaweza kumrudisha mtoto wetu."

Imetafsiriwa na Rashid Abdallah na kutafsiriwa na Yusuf Jumah