Shepherd Bushiri:Mchungaji milionea aiomba dunia iingilie kati kesi dhidi yake.

Chanzo cha picha, TWITTER
Nabii milionea Shepherd Bushiri ametuma ujumbe kwa Jumuiya ya nchi zilizoko kusini mwa Afrika SADC, Bara la Afrika na dunia nzima akidai iingilie kati katika kesi inayomkabili yeye na mke wake nchini Afrika Kusini.
Nabii huyo ambaye ni raia wa Malawi pamoja na mke wake Mary wanashitakiwa kwa makosa 419 ikiwa ni pamoja na utakatishaji wa fedha Afrika kusini.
Katika ujumbe wake Nabii huyo maarufu, amesema kuwa kesi yake haiwezi kuendeshwa kwa haki nchini Afrika kusini, kutokana na kauli alizozitoa Waziri wa ndani wa Afrika Kusini Dkt Aaron Motsoaledi alizozitoa kwa kamati ya bunge Jumanne kuhusiana na kanisa lake.
'' La kusikitisha ni kwamba waziri alizungumzia kesi yetu inayotarajiwa kufanyika pamoja na michakato iliyopo ndani ya wizara ambayo ana mamlaka nayo, waziri aliieleza tume kuhusU mchakato ambao unatumiwa na idara yake wa kuwafuatilia watu wanaoingia na kuondoka Afrika Kusini na mchakato unaofuatwa na idara katika utoaji wa vibali'', ulisema ujumbe wa Nabii Bushiri.

Chanzo cha picha, Twitter
Nabii Bushiri anasema: ''Hii ni moja ya michakato ambayo mimi na mke wangu tunapaswa kuifuata wakati imeingiliwa na mahakama ya juu nchini Afrika Kusini, ambayo pia waziri ameashirika kuwa alisikitika wakati haki zetu zilipolindwa na mahakama.''
Kwa mujibu wa taarifa hiyo Nabii Bushiri anasema Waziri wa mambo ya ndani alisema kuwa kibali chake na cha mkewe si vya kudumu kuishi Afrika Kusini ni vya muda mfupi kwa hivyo kuishi kwao nchini humo ni ukiukaji wa sheria kwasababu ''mimi na mke wangu hatukuwasilisha taarifa stahiki kwa idara yake ili kutoa vibali, wizara yake ilitoa vibali vya kuishi kimakosa, na hivyo kuamua kufuta vibali hivyo'', imesema taarifa ya Nabii Bushiri kwa dunia.

Chanzo cha picha, Twitter
Kulingana na maelezo yake, Nabii huyo ambaye ni raia wa Malawi anadai mchakato huo wa wizara ya mambo ya ndani tayari umemuhukumu kabla hajawasilisha maelezo yake kuhusu ni kwanini vibali vyao havipaswi kufutwa kwasababu hawakufanya kosa lolote, anasema.
''Waziri alisema kuwa mimi na mke wangu tunamiliki paspoti tano tofauti kila mmoja wetu. Anataka kuonesha kuwa hizi ni paspoti zenye majina tofauti na maelezo mengine, hili ni suala lililopo katika mahakama ya juu ya Afrika Kusini''
Anadai kauli ya Waziri inampa hofu kubwa kuwa hatapata kesi ya haki nchini Afrika Kusini.
Anasema anataka kesi yake na mkewe ifanyike nchini Malawi :''Ninaimani na Katiba ya Malawi kwasababu inawalinda raia wake wote ikiwa ni pamoja na mimi na mke wangu''.
Kukamatwa kwa Nabii Bushiri
Maafisa walimkamata yeye na mke wake mwezi Oktoba , 2020 na kumtuhumu kwa makosa ya wizi wa mamilioni ya dola na kuhusika katika sakata ya ufisadi.
Baadaye Novemba walimpatia yeye na mke wake dhamana ambayo ilikuwa na sharti kwamba lazima wasalimishe paspoti zao kwa mamlaka za Afrika Kusini.
Kuna hofu kuwa kesi hii inaweza kusababisha mzozo wa kidiplomasia kati ya Malawi na Afrika Kusini kwani watu wameanza kujiuliza maswali kuhusu hali za Bw Bushiri na mke wake na vipi waliweza kuingia nchini humo.
Shepherd Bushiri ni nani ?

Chanzo cha picha, Twitter
Nabii Mchungaji Shepherd Bushiri ni mzaliwa wa Malawi ambaye huendesha shughuli zake za "unabii" katika makanisa mbalimbali kuanzia Ghana hadi Afrika Kusini.
Anadai kuwa anatibu virusi vya Ukimwi/HIV na kuwafufua watu, kwa mujibu wa magazeti ya Afrika Ksuini ya Mail & Guardian yaliyotolewa 2018.
Bushiri aliwahi kubashiri kuwa Uingereza itagawanyika, "majimbo" na itaingia vitani na kuwa katika "vurugu", jarida la Maravi Post lilisema katika moja ya ripoti zake.
Na katika moja ya video zake alionekana akitembea hewani, video ambayo ilisambaa sana katika mitandao ya kijamii .
Bushiri alimwambia mwanasiasa wa Zimbabwe Kembo Mohadi kuwa atapata "madaraka " hata kabla ya kutangazwa kuwa makamu wa rais, kulingana taarifa ya New Zimbabwe.
Nabii Shepherd Bushiri ni muanzilishi wa kanisa Afrika Kusini lenye matawi yake katika nchi nyingine.
Wengi husema Mchungaji milionea ndiye kiongozi wa kidini tajiri zaidi barani Afrika.
Anadai kuwatibu watu wenye virusi vya HIV, kuwafanya vipofu waone njia, anawabadilisha masikini kuwa matajiri, na hata wakati mmoja aliwahi kusema kuwa yeye anaweza kurejesha pumzi ya uhai ndani ya mtu aliyekufa.
Mchungaji Bushiri alikulia katika mji wa Mzuzu, uliopo Malawi kabla ya kwenda Pretoria nchini Afrika Kusini.
Taarifa zinasema kuwa alipigwa marufuku kukanyaga katika ardhi ya Botwana kwasababu ya "pesa za miujiza".
Amekuwa maarufu sana kutokana na mikusanyiko mikubwa ya wafuasi wake wanaojaa katika viwanja vikubwa vya michezo.
Lakini watu wanamshutumu kuwa anawatumia vibaya masikini wanaotaka kubadili hali zao za maisha kwa kuwauzia "mafuta ya muujiza" .
Kesi yake imefikia wapi?

Chanzo cha picha, ECG MINISTRIES
Bushiri, na mke wake na watu wengine wawili wanakabiliwa na shutuma za kutakatisha fedha na mashitaka mengine 419.
Wapelelezi wa uhalifu wanasema kesi hiyo inahusu ina thamani ya randi ya Afrika kusini milioni 102 ($6.6m).
Alifikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi ya Pretoria tarehe 21 Oktoba na kesi yake ilitarajiwa kuanza Mei.
Akifahamika kama Major 1 au Nabii Shepherd , Bushiri alizaliwa tarehe 20 Februari, 1983.
Mamlaka za Botwana zilifunga kanisa lake baada ya madai kuwa alikuwa anawataka watu wampatie pesa bila huduma yoyote, kitu ambacho kilikuwa ni kinyume na sheria za fedha nchini humo.












