Wanafunzi wa Iran waandamana kwa siku ya pili katika baadhi ya vyuo vikuu

Chanzo cha picha, Reuters
Wanafunzi wamefanya maandamano katika vyuo vikuu kadhaa vya Iran kwa siku ya pili siku ya Jumapili, kulingana na mashirika ya habari ya ndani na machapisho ya mitandao ya kijamii, huku Iran ikikabiliwa na ongezeko la uwepo wa jeshi la Marekani wakati wa mazungumzo kuhusu nyuklia.
Machafuko mapya yanafuatia maandamano ya kupinga serikali mwezi uliopita ambapo maelfu ya watu waliuawa katika machafuko mabaya zaidi ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ya 1979.
Televisheni ya serikali ya Iran ilionyesha video za kile ilichosema ni watu "wanaojifanya wanafunzi" wakiwashambulia wanafunzi wanaounga mkono serikali huko Tehran ambao walikuwa wakishiriki katika maandamano ya kulaani ghasia za Januari.
Maandamano pia yalifanyika katika vyuo vikuu huko Mashhad kaskazini mashariki, kulingana na video zilizochapishwa na kundi la haki za binadamu lenye makao yake Marekani la HRANA.
Siku ya Jumamosi video inayodaiwa ya waandamanaji katika Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Sharif cha Tehran inaonesha wakimlaani Kiongozi Mkuu Ayatollah Ali Khamenei kama "kiongozi muuaji", na wakimtaka Reza Pahlavi, mwana wa Shah aliyepinduliwa wa Iran, awe mfalme mpya.
Maandamano ya hivi karibuni, ambayo yalianza Desemba kuhusu ugumu wa kiuchumi na haraka yakageuka kuwa ya kisiasa.



