Moja kwa moja, Mwanaume mwenye silaha auawa baada ya kukaribia makazi ya Trump

Mwanaume huyo alikuwa amebeba bunduki na kopo la mafuta aliposimamishwa kabla ya kupigwa risasi na maafisa wa Secret Service na polisi

Muhtasari

Moja kwa moja

Rashid Abdallah

  1. Wanafunzi wa Iran waandamana kwa siku ya pili katika baadhi ya vyuo vikuu

    l

    Chanzo cha picha, Reuters

    Wanafunzi wamefanya maandamano katika vyuo vikuu kadhaa vya Iran kwa siku ya pili siku ya Jumapili, kulingana na mashirika ya habari ya ndani na machapisho ya mitandao ya kijamii, huku Iran ikikabiliwa na ongezeko la uwepo wa jeshi la Marekani wakati wa mazungumzo kuhusu nyuklia.

    Machafuko mapya yanafuatia maandamano ya kupinga serikali mwezi uliopita ambapo maelfu ya watu waliuawa katika machafuko mabaya zaidi ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ya 1979.

    Televisheni ya serikali ya Iran ilionyesha video za kile ilichosema ni watu "wanaojifanya wanafunzi" wakiwashambulia wanafunzi wanaounga mkono serikali huko Tehran ambao walikuwa wakishiriki katika maandamano ya kulaani ghasia za Januari.

    Maandamano pia yalifanyika katika vyuo vikuu huko Mashhad kaskazini mashariki, kulingana na video zilizochapishwa na kundi la haki za binadamu lenye makao yake Marekani la HRANA.

    Siku ya Jumamosi video inayodaiwa ya waandamanaji katika Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Sharif cha Tehran inaonesha wakimlaani Kiongozi Mkuu Ayatollah Ali Khamenei kama "kiongozi muuaji", na wakimtaka Reza Pahlavi, mwana wa Shah aliyepinduliwa wa Iran, awe mfalme mpya.

    Maandamano ya hivi karibuni, ambayo yalianza Desemba kuhusu ugumu wa kiuchumi na haraka yakageuka kuwa ya kisiasa.

  2. Trump ashangaa kwa nini Iran 'haijasalimu amri'

    l

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais wa Marekani Donald Trump anahoji kwa nini Iran bado "haijasalimu amri" licha ya ongezeko la shughuli za kijeshi la Washington huko Mashariki ya Kati, amesema mjumbe maalum wa rais wa Marekani Steve Witkoff.

    Witkoff ameiambia Fox News siku ya Jumamosi kwamba Trump ana “hamu ya kujua" msimamo wa Iran baada ya kutishia kufanya shambulio dogo la kijeshi ikiwa makubaliano hayatafikiwa kuhusu mpango wa nyuklia wa Tehran.

    Marekani na washirika wake wa Ulaya wanashuku Iran inaelekea kutengeneza silaha ya nyuklia, jambo ambalo inakanusha.

    Ndani ya Iran, maandamano ya kupinga serikali yalifanyika katika vyuo vikuu kadhaa mwishoni mwa juma - maandamano ya kwanza ya kiwango hicho tangu yale ya Januari, ambapo maelfu ya watu wakiuawa.

    Katika mahojiano yake na Fox News, Witkoff amesema: "Sitaki kutumia neno 'kuchanganyikiwa'... kwa sababu yeye [Trump] anaelewa ana njia mbadala nyingi, lakini ana hamu ya kujua kwa nini hawajafanya hivyo... yaani kwa nini hawajasalimu amri."

    "Kwa nini, chini ya shinikizo la aina hii, nguvu za majini tulizonazo, kwa nini hawajatwambia, 'Hatutaki silaha za nyukilia."

    "Bado ni vigumu kuwafikisha mahali hapo," mjumbe wa Trump aliongeza.

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi alisema Jumapili anaamini bado kuna uwezekano kwamba mzozo huo unaweza kutatuliwa kidiplomasia.

    Katika maoni tofauti siku mbili zilizopita, Araghchi alisema Tehran ikiandaa "rasimu ya makubaliano" na itaikabidhi kwa Witkoff katika siku chache zijazo.

    Maafisa wa Marekani na Iran walijadili mpango wa nyuklia wa Iran katika mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja huko Geneva, Uswisi, tarehe 17 Februari. Walisema maendeleo yamepatikana.

    Oman - ambaye ndiye mpatanishi wa mazungumzo hayo - alitangaza Jumapili kwamba duru inayofuata ya mazungumzo "imepangwa kufanyika Geneva Alhamisi hii".

  3. Greenland yakataa meli ya matibabu ya Trump

    p

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Marekani ina meli mbili maalum zenye hospitali, ikiwa ni pamoja na USNS Mercy

    Waziri mkuu wa Greenland amemwomba Rais wa Marekani Donald Trump kuzungumza naye badala ya kutoa "matamshi katika mitandao ya kijamii," baada ya Trump kusema Marekani imetuma meli ya matibabu ili kutoa "huduma" kwa watu kisiwa hicho.

    Trump aliandika kwenye Truth Social kwamba anatuma meli iliyojaa vifaa vya matibabu, akidai "watu wengi" kisiwani humo ni wagonjwa na "hawatunzwi".

    Jens-Frederik Nielsen alijibu "tunakataa," na akasema Greenland hutoa huduma ya afya bila malipo kwa raia wote, tofauti na Marekani.

    Trump amekuwa akikitaka kisiwa kikubwa cha arctic kwa muda mrefu - lakini alikubali mwezi Januari kwamba hatokichukua.

  4. Mwanaume mwenye silaha auawa baada ya kukaribia makazi ya Trump

    o

    Chanzo cha picha, Facebook

    Mwanaume mwenye silaha ameuawa kwa kupigwa risasi baada ya kukaribia eneo la makazi ya Rais wa Marekani Donald Trump huko Mar-a-Lago, Florida, imesema Idara ya Usalama wa rais.

    Mwanaume huyo alikuwa amebeba bunduki na kopo la mafuta aliposimamishwa kabla ya kupigwa risasi na maafisa wa Secret Service na polisi, imesema Idara hiyo.

    Tukio hilo lilitokea Jumapili asubuhi, wakati rais alipokuwa Washington DC.

    Mshukiwa ametajwa kama Austin T Martin kutoka Cameron, North Carolina, kulingana na CBS.

    Familia yake huko North Carolina iliripoti kupotea kwake mapema Jumapili asubuhi, Ofisi ya Polisi ya Kaunti ya Moore imesema katika taarifa kwa BBC.

    Ofisi hiyo imesema haina historia yoyote ya uhalifu inayomhusu Martin.

    Mwanaume huyo alipigwa risasi baada ya kukataa amri, amesema mkuu wa polisi wa kaunti ya Palm Beach, Ric Bradshaw.

    "Maneno pekee tuliyomwambia yalikuwa 'acha vitu hivyo' ikimaanisha kopo na bunduki," Bradshaw aliuambia mkutano na waandishi wa habari.

    "Aliweka chini kopo la gesi, akainua bunduki yake hadi mahali pa kufyatua risasi," alisema.

    Maafisa walimpiga risasi.

    Aliongeza kuwa maafisa hao walikuwa wamevaa kamera za mwili na hakuna maafisa waliojeruhiwa.

    Usalama huko Mar-a-Lago ni mkali sana, ukiwa na uzio wa nje wa polisi wa Palm Beach na ule wa ndani unaosimamiwa na Idara ya Usalama wa rais.

    Trump amekuwa shabaha na majaribio kadhaa ya mauaji.

    Julai 2024, Trump alipigwa risasi sikioni alipokuwa amesimama mbele ya umati wa watu huko Butler, Pennsylvania.

    Pia unaweza kusoma:

  5. Hujamboa na karibu

    Nakukaribisha katika taarifa zetu za moja kwa moja, leo Jumatatu tarehe 23/2/2026