Unywaji pombe kwa wajawazito: Unywaji wa akina baba pia unaweza kuathiri mtoto?

Chanzo cha picha, Getty Images/BBC
- Author, Amanda Ruggeri
- Nafasi, BBC
- Muda wa kusoma: Dakika 4
Kwa zaidi ya miaka 50, wanasayansi wameonya juu ya hatari za kunywa pombe wakati wa ujauzito. Utafiti wa hivi karibuni umegundua kuwa unywaji pombe hata mara moja kwa wiki, unaweza kuathiri ukuaji wa ubongo wa mtoto, ufahamu na tabia zake, na sura ya uso.
Wataalamu wanasema hakuna kiwango salama cha pombe kwa mwanamke kunywa wakati wa ujauzito. Pia kuna madhara ya kuharibika kwa mfumo wa neva, mtoto kuwa na uwezo mdogo wa kujifunza na kuchelewa kusema.
Kadiri hatari za unywaji pombe kwa mama zinavyoweza kumwathiri mtoto tumboni, athari za unywaji pombe kwa baba zinapuuzwa.
"Kwa miaka sasa, tumekuwa tukisikia hadithi kutoka kwa wanawake ambao husema, 'sikuwahi kunywa wakati wa ujauzito, lakini sasa nina mtoto mwenye matatizo - na mpenzi wangu wa kiume alikuwa mnywaji wa pombe kwa muda mrefu'," anasema Michael Golding, mwanafiziolojia katika Chuo Kikuu cha Texas, A&M ambaye anatafiti juu ya pombe kwa mjamzito.
Tatifi zinasemaje?

Chanzo cha picha, Serenity Strull/Getty Images/BBC)
Taarifa kama hizo kutoka kwa wanawake mara nyingi hupuuzwa. Lakini tafiti za hivi karibuni zimegundua kuwa watoto ambao baba zao hunywa pombe wako kwenye hatari kubwa ya kupata matatizo ya kiafya.
Utafiti mmoja wa 2021 ulichunguza zaidi ya wanandoa nusu milioni nchini China, uligundua hatari ya mtoto kuzaliwa na mdomo uliopasuka, ugonjwa wa moyo wa kuzaliwa, na matatizo ya njia ya utumbo - ni kubwa ikiwa baba atakunywa pombe kabla ya mimba, hata kama mama hakunywa.
Utafiti mwingine kutoka China uliangazia watoto 5,000 wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa na wengine 5,000 wasio na matatizo.
Iligundulika kuwa watoto walikuwa na hatari mara tatu zaidi ya kuwa na matatizo ya moyo ya kuzaliwa ikiwa baba ni mnywaji katika kipindi cha miezi mitatu kabla ya ujauzito - kuliko ikiwa baba si mnywaji.
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
"Utafiti wetu unapendekeza kwamba akina baba wanapaswa kurekebisha unywaji wao wa pombe kabla ya kushika mimba kwa mama ili kupunguza hatari ya mtoto kuzaliwa na matatizo, kwa kuzingatia kuwa kiwango cha unywaji wa baba cha 31.0% huongeza hatari ya mtoto kuzaliwa na kasoro," watafiti waliandika.
Watu wenye matatizo yaliyotokana na mzazi kunywa pombe hulazwa mara nyingi hospitalini kuliko wale wasio kuwa na matatizo hayo, na wana umri wa kuishi ambao ni 42% ya idadi ya watu kwa ujumla.
Unywaji pombe kwa wanaume hautakuwa na athari ya ndiyo/hapana kwa watoto; lakini kadiri unavyokunywa ndivyo unavyoongeza hatari kwa mtoto na matokeo yanavyozidi kuwa mabaya.
Kama ilivyo kwa sigara, kuna uthibitisho mzuri kuwa kuvuta sigara kunatoa athari kwenye chembe za urithi. Watoto wa akina baba wanaovuta sigara wana uwezekano mkubwa wa kuwa na kasoro za kuzaliwa, kupata saratani ya damu, na kuwa na mafuta mengi mwilini.
Licha ya unywaji pombe wa wanaume unaonekana pia kuathiri watoto, watafiti wengi wanakubali unywaji pombe wa mama huathiri zaidi katika ukuaji wa mtoto kuliko unywaji pombe wa baba.
Pombe katika damu ya mwanamke hupitishwa moja kwa moja kwenye kondo (plasenta) hadi kwenye kijusi, kwa hivyo, hiyo ni athari ya moja kwa moja katika ukuaji.
Athari zaidi zaelezwa

Chanzo cha picha, Serenity Strull/Getty Images/BBC
Elizabeth Elliott, daktari wa watoto na profesa wa afya ya watoto na vijana katika Chuo Kikuu cha Australia cha Sydney, ametafiti kwa muda mrefu athari za pombe kwa vijusi na anasema:
“Pombe inaathiri ubongo na sehemu ya ubongo ambayo huamua maendeleo ya uso, na inaathiri maendeleo ya mifumo yote ya viungo kama mapafu, moyo, masikio na macho, na kadhalika."
Elliott na wengine wanasema, ni wakati wa kampeni za afya ya umma kushughulikia suala la unywaji pombe kwa akina baba moja kwa moja. Na anajibu ikiwa kuna kiasi cha pombe salama ambacho baba anaweza kunywa.
“Hatuna data za hilo. Kuna mambo mengi ambayo tunajua yanaweza kuboresha afya kwa watoto, kama vile kufanya mazoezi na kula vizuri. Kama wangekuwa wanangu, ningewaambia waache kabisa pombe,” anasema.
"Kuna mzigo mkubwa ambao hutwishwa wanawake. Lakini afya ya mwanaume ni muhimu kwa ukuaji wa kijusi. Kuna jukumu la pande zote mbili hapa kusaidia na kutoa afya ya mtoto."
Imetafsiriwa na Rashid Abdallah na kuhaririwa na Seif Abdalla












